Kiongozi wa Uamsho ashtakiwa, ulinzi mkali watanda, apelekwa rumande

 Sheikh Farid Hadi Ahmed Viongozi sita wa UAMSHO mbaroni kwa tuhuma za kuchochea ghasia Zanzibar
Sheikh Amir Farid Hadi Ahmed; Kiongozi wa UAMSHO

KIONGOZI wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kislamu, Sheikh Faridi Hadi Ahmed, na wenzake sita jana walipandishwa katika Mahakama ya Wilaya Manakwerekwe visiwani hapa, wakikabiliawa na tuhuma za kufanya uchochezi na kusababisha vurugu.
Mwendesha Mashtaka wa Serikali kutoka ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), Maulid Ame, aliwataja viongozi wengine kuwa ni Sheikh Mselem Ali Mselem (Kwamtipua), Sheikh Musa Juma Issa (Makadara) na Sheikh Azani Khalid Hamdani (Mfenesini).
Wengine ni Sheikh Suleiman Juma Suleiman (Makadara), Sheikh Khamis Ali Suleiman (Mwanakwerekwe) na Hasan Bakari Suleiman mkazi wa Tomondo.
Wote kwa pamoja walidaiwa kuwa Agosti 17, mwaka huu, majira ya saa 11 jioni huko kiwanja cha Magogoni Msumbiji katika Wilaya ya Magharibi Unguja wakiwa wahadhiri kutoka Jumuiya ya Uamsho na mihadhara ya Kiislamu walitoa matamko ya uchochezi.
Kwamba maneno hayo yaliashiria uvunjifu wa amani na kusababisha fujo na maafa mbalimbali na mtafaruku kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ).
Mwendesha mashtaka huyo alisema kitendo hicho kilikwenda kinyume na kifungu cha 45 (1) (a) (b) sheria na 6 ya mwaka 2004 sheria za Zanzibar.
Hata hivyo wakili wa washtakiwa hao, Abdalla Juma, alisema kuwa makosa ya wateja wake si miongoni mwa yale yanayopaswa kunyimwa dhamana, hivyo aliomba mahakama kuwapatia dhamana kwa masharti mepesi.
Alisema kuwa kitendo cha kutaka barua ya sheha na wadhamini ambao ni watumishi wa serikali kwa ajili ya dhamana ni kuwakwamisha wateja wake kwani watu hao ni vigumu kuwapata.
Hata hivyo, mwendesha mashtaka wa serikali hakuwa na pingamizi na ombi la dhamana hiyo na kusema anaiachia mahakama itoe uamuzi.
Naye hakimu anayesikiliza kesi hiyo, Ame Msaraka Pinja, alisema wa kuwa dhamana ni haki yao haitakuwa busara kwa mahakama yake kutoa uamuzi wa haraka wala kuchelewesha dhamana za washtakiwa hao.
Aliiahirisha kesi hiyo hadi Oktoba 25 mwaka huu ambapo itakuja kusikizwa uamuzi wa dhamana zao, na hivyo watuhumiwa wote walirudishwa rumande.
Hata hivyo, wakati wote kesi hiyo ikiendelea, ulinzi mkali wa polisi ulitanda kuzunguka mahakama hiyo, huku watu wakizuiwa kuingia ndani.
Sheikh Faridi na wenzake walifikishwa mahakamani hapo majira ya saa 5:00 asubuhi chini ya ulinzi mkali wa polisi wenye magari saba aina ya Landrover.

Dk. Slaa amkaba JK

Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Willibrod Slaa, amemtaka Rais Jakaya Kikwete kuvunja ukimya wake na kuchukua hatua sahihi kumaliza chokochoko za udini zinazolielemea taifa.
Dk. Slaa alisema kuwa yanayoendelea ndani ya nchi yametengenezwa na watawala wenyewa, hivyo amemtaka Rais Kikwete kujifunza kwa Rais mstaafu Alli Hassan Mwinyi.
Alisema kuwa kiongozi huyo aliweza kuchukua hatua za kitaasisi kumaliza mizozo iliyoanzishwa na makundi ya Wakristo wenye imani kali na Waislamu miaka ya 90, ambayo yalikuwa yakishambuliana kwa mahubiri na hotuba kalikali.
Akihutubia mkutano wa kampeni za uchaguzi mdogo wa udiwani kata ya Bugarama, Kahama juzi, Dk. Slaa alisema kuwa hatua hiyo ni moja ya vitu vinavyomfanya Rais Mwinyi akumbukwe na Watanzania.
“Hali ya sasa hivi ni tofauti kwani matatizo yanayoendelea nchini yamezalishwa na viongozi wenyewe, wanaotafuta visingizio vya kuvuruga nchi baada ya kushindwa kuongoza na kuweka fursa za wananchi kujipatia maendeleo,” alisema.
Dk. Slaa aliongeza kuwa yanayoendelea sasa ni kama vile nchi haina kiongozi, haina serikali na hakuna chama kinachoongoza serikali, kwani wote wanaowajibika kukemea na kuchukua hatua sahihi kumaliza tatizo wamekaa kimya.
Alisema kuwa Watanzania wote wema, bila kujali itikadi zao za dini wala siasa, wanaoipenda nchi yao, wanapaswa kupaza sauti zao kabla nchi haijatumbukia katika matatizo.
Kwamba hali hii imetokana na watawala walioko madarakani kuwatumia viongozi wa dini kuwagawanya Watanzania ili wasiwe na muda wa kuhoji masuala ya msingi.
“Sasa tunamtaka Kikwete kama nchi imemshinda atangaze kuwa ameshindwa ili asaidiwe. Na CCM yao hawana tena uwezo wa kuhubiri amani, maana nilishawaambia amani haihubiriwi majukwaani,” alisema.

TANZANIA DAIMA

No comments

Powered by Blogger.