Serikali kubanwa kashfa ya mabilioni

MBUNGE wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (Chadema) 

MBUNGE wa Ubungo (Chadema), John Mnyika amesema ataongeza nguvu ya wabunge wanaotaka Serikali kuchukua hatua za haraka kuwataja baadhi ya viongozi na wafanyabiashara wanaodaiwa  kuficha nje mabilioni ya fedha yanayosadikiwa kupatikana kwa njia isiyo sahihi.
Mnyika aliyasema hayo jana katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kata ya Saranga Mbezi jijini Dar es Salaam,  ambapo tayari Mbunge wa  jimbo la Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe  alishatoa kauli kama hiyo ya kuitaka Serikali kuchukua hatua za haraka kuwataja watu hao kabla ya vikao vya Bunge vya mwezi Aprili.
Akizungumza katika mkutano huo, Mnyika alisema Serikali itegemee kupata upinzani mkubwa katika vikao vya Bunge Aprili mwakani kama haita jisafisha kwa kuwataja watu hao na kuwachukulia hatua.
“Nia yetu ni kuhakikisha watu wote wanaodaiwa kuwa na akaunti mbalimbali nje ya nchi Serikali inawachukulia hatua pamoja na kuwataja kwa majina ili watanzania waeze kuwafahamu watu wanao wasababisha waishi katika hali ngumu,” alisema Mnyika na kuongeza:
“Nijambo la kushangaza kusikia kwamba Serikali ya CCM inasema wapinzani ndiyo tuwataje lakini suala hilo lipo wazi kwani kama itakumbukwa, Septemba 15 mwaka 2010 katika viwanja vya Mwembeyanga tulitaja majina hayo na wengine kwa sasa ndio Viongozi wakubwa ndani ya Bunge.”
Mnyika alibainisha kwamba Chadema itaendelea na kasi yake ile ile hadi kuhakikisha viongozi wote wanaodaiwa kuwa na akaunti nje ya nchi wanajulikana wazi ili Watanzania wawafahamu watu wanao tumia kodi zao kwa masilahi yao binafsi.
Katika hatua nyingine, Mnyika alisema suala la usafiri katika jiji la Dar es Salaam bado ni tatizo kwani hata kuwapo kwa usafiri wa treni sio suluhisho kutokana na Serikali kupata hasara ya Sh10 milioni kila baada ya siku tano kutokana na undeshaji wa usafiri huo.
Alisema kutokana na maandalizi duni Serikali inapata hasara ya Sh10 milioni jambo ambalo ni hatari kwani itafikia hatua usafiri huo wa Treni utasimama.
“Ni vyema Serikali ikajipanga vizuri kwani kwa sasa wakazi wengi wa Jiji la Dar es Salaam wanafurahia usafiri wa Treni lakini ipo siku usafiri huo utasimama kutokana na kuendeshwa kwa hasara kubwa,” alisema na kuongeza;
“Jambo hilo linatokana na kuwa na miundombinu mibovu na maandalizi duni yaliyofanywa na mawaziri wa uchukuzi waliopita.”

CHANZO: MWANANCHI

No comments

Powered by Blogger.