Mwandishi wa Channel Ten ashambuliwa

 
Na Burhani Yakub, Tanga
MWANDISHI wa habari wa Kituo cha Televisheni cha Chanel Ten Tanga, Linus Kamafa amejeruhiwa vibaya na vijana waliokuwa wakichoma matairi na kulipua baruti wakati wakisherehekea mkesha wa Mwaka Mpya.
Vijana hao wanadaiwa kumshambulia kwa mawe na mapanga mwandishi huyo wa habari wakidhani ni miongoni mwa askari  Polisi waliokuwa wakipita mitaani kuzuia uchomaji moto wa matairi na kulipua baruti.
Kwa mujibu wa habari zilizopatikana na kuthibitishwa na Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Tanga,Constantine Massawe ni kuwa mwandishi huyo wa habari alishambuliwa juzi saa 6.30 usiku katika Mtaa wa Mapinduzi jijini hapa wakati akipiga picha za matukio ya uchomaji wa matairi,baruti na kurusha mawe kwenye nyumba za watu.
Watu walioshuhudia tukio hilo walisema kuwa mwandishi huyo wa habari alijitokeza kwenye Mtaa wa Mapinduzi muda mfupi mara baada ya gari la polisi kupita eneo hilo kwa lengo la kuzuia uchomaji wa moto na  wakaanza kumshambulia wakimtuhumu kuwa ni askari aliyewapiga picha.
Akizungumza na Mwananchi Kamafa alisema, walianza kumshambulia kwa mawe huku wakitaka kumnyang’anya kamera ndipo akaamua kukimbia lakini alizingirwa na kushambuliwa hadi akaanguka chini na kujeruhiwa magotini,mgongoni na kichwani. Alisema aliokolewa na watoto wake waliomfuata baada ya kusikia akishambuliwa ndipo wakamkimbiza kituo cha polisi cha Mabawa kwa ajili ya kupewa PF 3 na baadaye alifikishwa hospitalini kupata matibabu.
Mwandishi huyo wa habari alisema katika kipindi cha nyuma cha mkesha wa Mwaka Mpya , vijana waliishia kuchoma moto matairi barabarani pekee.

MWANANCHI

No comments

Powered by Blogger.