HABARI

Theme images by kelvinjay. Powered by Blogger.

MATUKIO

MICHEZO

SIASA

» »Unlabelled » Naibu Waziri aiomba Serikali kupunguza kodi


Naibu Waziri wa Fedha na Uchumi, Janet  Mbene. 
 
Naibu Waziri wa Fedha na Uchumi, Janet  Mbene ameiomba  Serikali kuwatengenezea mazingira mazuri ya kazi  wananchi  ili  waweze kulipa kodi kwa wakati ambayo itasaidia kuleta maendeleo  ya taifa.  
Waziri Mbene aliyasema hayo mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam  wakati   akifanya  ziara ya kukagua nyumba 491 zilizopo eneo la Buyuni Kata ya Majohe Wilaya ya Ilala ambazo zimejengwa na Mradi wa Mfuko wa Pensheni kwa Watumishi wa Umma (PSPF). Alisema lengo la kujengwa  kwa nyumba hizo ni  kuwanufaisha wanachama na wananchi na kwamba Serikali itakapoweka mazingira mazuri ya kazi kwa wananchi wake wataweza kulipa kodi ambayo itasaidia kuleta maendeleo katika jamii.
Aliongeza kuwa  kila mwananchi ana wajibu wa kuchangia kodi ambayo itafanya  kazi ya kuibua miradi mbalimbali ya kuleta maendeleo ya jamii  ikiwamo ujenzi wa miundombinu ya barabara
“Serikali ifanye jitihada ya kuwawekea mazingira mazuri ya kazi wananchi  ili  waweze kulipa kodi kwa wakati ambayo itapelekwa kwenye maendeleo ya jamii,” alisema Mbene.
Pia, aliwataka wanachama wa  PSPF kuchangamkia nyumba hizo waweze kununua au kukopa ili kujikwamua na adha ya kupanga ikiwamo kupata nyumba bora na za kisasa.
“Nyumba ni nzuri na zitawasaidia wananchi wa kawaida katika suala la ulipaji wa kodi,  wamehakikisha haumizwi katika ulipaji, ndiyo maana wameamua mtu awe analipa kuanzia miaka 15 hadi miaka 20,” alisema na kuongeza:
“Nawaomba PSPF kuhakikisha mahitaji muhimu yote yanayohitajika yanapatikana kama maji, umeme, usafiri na barabara iwekwe kiwango cha lami itamrahisishia mwananchi atakayehamia  kuwa na uhakika wa usalama wake,” alisema Mbene. Kaimu Mkurugenzi wa PSPF, Adamu Mayunga alisema wamejipanga kuhakikisha  miundombinu ya maji, umeme na barabara ambavyo ni kilio cha muda mrefu kwa wakazi wa eneo hilo vinapatikana.
“Tumeshapata mkandarasi wa Manispaa ya Ilala ambaye amekubali kupeleka greda kwa ajili ya kuchonga barabara na kwa upande wa maji, Shirika la Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (Dawasco) ilitujibu itachukua muda mrefu kufikisha mabomba kwenye eneo hili hivyo tumejipanga kuchimba visima vya maji,” alisema Mayunga.
Alisema nyumba hizo zimejengwa kwa awamu ya kwanza ambazo zipo kwenye mikoa ya Dar es Salaam, Morogoro Shinyanga, Tabora na Mtwara hivyo wanachama hao wanatakiwa kununua popote wanakotaka.
Kwa mujibu wa Mayunga, nyumba hizo zitaanza kuuzwa kwa Sh64 milioni hadi Sh94 milioni kulingana na mahali nyumba ilipojengwa hiyo gharama ikiwa ni pamoja na kodi ya ongezeko la VAT.


MWANANCHI

«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post

No comments: