12 wafa ajalini Mwanza, Mbeya



Basi la Mkwizi linalofanya safari zake za Mwanza - Musoma ambalo jana liligongana na lori aina ya Fuso na kusababisha vifo vya watu sita mkoani Mwanza. Picha na Miguel Suleiman 
 
Mwanza na Mbeya. Watu 12 wamefariki katika ajali mbili tofauti zilizotokea katika Mikoa ya Mbeya na Mwanza.Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya, Diwani Athumani alisema kati ya hao sita waliofariki, wamo raia watano wa Malawi huku wengine 25 wakijeruhiwa baada ya basi walilokuwa wakisafiria la ‘Easy Bus’ aina ya Scania kupinduka katika Kijiji cha Igawa Wilaya ya Mbarali mkoani Mbeya.

Waliofariki na kutambuliwa katika ajali hiyo ni pamoja na Atham Bonzo, Maria, Adam, Sakwati na mtoto mdogo anayekadiriwa kuwa na mwaka mmoja ambao wote ni wakazi wa Malawi. Pia Rajabu Hassan (35), mkazi wa Tanga aliyekuwa kondakta wa basi hilo.

Kamanda Diwani alisema kuwa tukio hilo lilitokea katika Barabara ya Mbeya-Iringa saa 3:30 asubuhi. Awali ilielezwa kwamba Chanzo cha ajali hiyo ni kutokana na basi la Taqwa lililokuwa likiendeshwa na Kenneth Thomas (48) mkazi wa Kabwe jijini Mbeya.

Alisema kuwa dereva wa basi hilo la Taqwa lililokuwa likitokea Malawi kwenda Dar es Salaam alikuwa akijaribu kulipita basi la Easy na baada ya kulipita alikutana na gari lingine kwa mbele na ndipo dereva wa basi hilo alipochukua uamuzi wa kurudi nyuma.

“Dereva wa Taqwa aliporudi nyuma ndipo dereva wa basi la Easy, Ajali Mohamed (32) mkazi wa Iringa alipopoteza mwelekeo na kuacha njia na kupinduka na kusabaisha vifo vya watu hao,” alisema.

Kamanda Athumani alisema kuwa dereva wa basi la Taqwa anashikiliwa na polisi wakati taratibu za kumfikisha mahakamani zikifanyika wakati mwenzake wa Easy alikimbia baada ya tukio hilo.

Alisema kuwa miili ya marehemu wote imehifadhiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mbeya na kwamba majeruhi 25 wakiwamo wanaume 14 na wanawake 11 wamelazwa katika Hospitali ya Mission ya Ilembula na wanaendelea na matibabu.

Katika ajali nyingine, basi la Mkwizi linalofanya safari zake kati ya Mwanza na Musoma, liligongana uso kwa uso na lori aina ya Fuso lililokuwa na mchanga katika eneo la Igoma wilayani Nyamagana mkoani Mwanza na kusababisha watu sita kufariki dunia papo hapo.
Mashuhuda wa ajali hiyo walidai kuwa dereva wa basi pamoja abiria wawili waliokuwa wamekaa viti vya mbele walifariki huku ikielezwa kuwa dereva wa Fuso pamoja na watu wengine wawili waliokuwamo ndani yake nao walikufa papo hapo.Chanzo cha ajali hiyo imeelezwa kuwa ni askari wa usalama barabarani, aliyekuwa amesimamisha magari zaidi ya matatu.

“Alisimamisha lori la kwanza la Fuso wakati lori jingine la aina hiyo likiwa nyuma na ndiyo lilikutana uso kwa uso na basi na kufanya askari hao kutoweka,” alieleza Salum Bakari, ambaye alishuhudia ajali hiyo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Elias Mangu alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kusema bado anasubiri taarifa rasmi kutoka kwa maofisa wake waliokwenda eneo la tukio.“Sina taarifa kwa sasa, nasubiri maofisa wangu ambao wamekwenda eneo la tukio kufahamu zaidi kilichotokea,” alieleza Kamanda Mangu.



MWANANCHI

No comments

Powered by Blogger.