Wakulima Mtibwa wasema kilimo cha Miwa sasa basi

 Miwa ya ndani ya Kiwanda cha Sukari Mtibwa
 Usoni mwa Kiwanda cha Sukari Mtibwa
 Wafanyakazi wa Kiwanda cha Sukari Mtibwa.

Na Bryceson Mathias, Mkindo Mvomero
 
Wakulima Wadogo wa Miwa ya nje Kata ya Mtibwa, Wilaya ya Mvomero, mkoani Morogoro, wamesusia Kilimo hicho na kugeuzia nguvu zao kwenye mazao mengine kwa madai kinawapa Umaskini na hivyo kushindwa kusomesha wanafunzi na kujikimu.
 
Kauli hiyo pia ilithibitishwa jana na Mkuu wa Chuo cha Kilimo cha Mpunga Mkindo ambaye pia ni Mkufunzi wa Mafunzo ya Shamba Darasa Bw. Moses Temi, kwamba wakulima wengi wa miwa wanafurika chuoni hapo kupata ushauri.
 
Akithibitisha wakulima kuachana na Kilimo hicho Temi alisema, kumekuwa na wimbi la wakulima wa zao la Miwa wanaofurika chuoni hapo kutaka ushauri wa Kitalaamu ili waachane na kilimo cha miwa na badala yake walime mazao kama Mpunga, Mahindi na Alizeti wakidai, Miwa inawapa Umaskini wa kifamilia.
 
“Ninashangaa baadhi ya wakulima wazuri wa miwa ninaowafahamu na mashamba yao, wamefika ofisini kwangu wakitaka ushauri wa kitalaam namna watakavyolima mpunga na mazao mengine, na ninapowauliza kulikoni, wanadai miwa sasa inawapa Umaskini”.
 
Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji Kisala Msafiri Shija alisema, Kilimo hicho badala ya kuwa mkombozi kwa wananchi, sasa kimekuwa ni sindano yenye dawa ya sumu inayoua juhudi za wakulima wadogo na kuwanufaisha wenye uwezo, huku walalahoi wakifirisiwa.
 
Hatua ya Wakulima hao kufanywa maskini, ndiyo iliyomkera Diwani wa Kata ya Mtibwa Lukas Mwakambaya (CHADEMA) Bunge lililopita, kutinga Mjengoni kuwasilisha Kilio chao, jinsi ambavyo Uwekezaji wa Kiwanda cha Sukari Mtibwa ambavyo umekuwa hauwasaidii chochote pamoja na nia njema ya Serikali iliyowapora 25% ya Hisa yao (Share) kwa miaka yote ya uwkezaji na hivyo kukosa sauti.
 
Hivi majuzi, wakulima wadogo Miwa ya Nje Kiombero kama walivyo wa Mtibwa walilumbana na kuilalamikia Serikali ya Wilaya Kilombero, Mkoa na Serikali Kuu, wakidai Mwekezaji wa Kiwanda cha Sukari Kilombero (ILOVO), kufanya wawe maskini kutokana na bei ya zao hilo kuwa ndogo kiasi cha kushindwa kulipa madeni waliyokopa Taasisi za Fedha, ambapo Serikali haiwashughulikii.

No comments

Powered by Blogger.