Maafa tena, kifusi chaua Arusha



 
 Mussa Juma na Moses Mashalla, Mwananchi

Arusha. Siku tatu baada ya ghorofa kuanguka na kuua watu 36 jijini Dar es Salaam, maafa mengine yametokea jana mkoani Arusha ambako watu wapatao 20 wanahofiwa kufa baada ya kufunikwa na kifusi cha `moramu’ wakati wakifanya shughuli za uchimbaji eneo la Moshono, Arusha.

Maiti za watu 14 ndiyo zilikuwa zimeopoelewa hadi jana jioni wakati watu wawili tu ndiyo walikuwa wametoka wakiwa hai na kukimbizwa katika Hospitali ya Mt Meru kwa ajili ya matibabu kutokana na kuvunjika miguu.

Waliotolewa wakiwa hai walitambuliwa kuwa ni Matei Nenano na Lushooki Laizer wote wakazi wa jijini Arusha. Mwananchi lilishuhudia vikosi vya uokoaji kutoka Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), Polisi pamoja na wananchi wakitoa msaada wa kufukua kifusi hicho kwa ajili ya kutoa watu waliofunikwa.

Maiti zilizoopolewa ni za mmiliki wa magari ya kubeba kifusi hicho, Julius Peter, Alex Mariaki, Gerald Lutakata, Hassan Hamis, Sauli Raphael, Bariki Revelian na Kababuu Ruafela.
Wengine ni Mwenda Kiboliboli, Japhet Jivaline, Benard Masai, Gerald Jacob, Fredy Losileani, Julius Palangyo na mtu ambaye alijulikana kwa jina moja la Christopher.

Watu walioshuhudia tukio na taarifa hizo kuthibitishwa na Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Hemed Kilonge walisema lilitokea jana saa 5.00 asubuhi wakati shughuli za uchimbaji zikiendelea.

Kamanda Kilonge alisema wakati wachimbaji hao wakiwa ndani ya shimo wakiendelea na kuchimba ‘moramu’, ghafla gema liliporomoka na kuwafunika.

Mashuhuda walisema wachimbaji hao walikuwa wakifanya shughuli zao huku mvua kubwa ikinyesha na kwamba kuna uwezekano hiyo ni sababu ya kuanguka kwa kifusi hicho.
Mvua ilikuwa ikiendelea hata wakati wa uokoaji, hali iliyofanya kazi hiyo kuwa ngumu.

“Inasadikiwa kuwa zaidi ya wachimbaji 20 pamoja na magari mawili kwa ajili ya kubeba mzigo huo yalikuwapo ndani ya shimo hilo ambayo nayo yalifunikwa na kifusi hicho,”alisimulia Kamanda Kilonge.

Uhaba wa mafuta
Mwananchi lilishuhudia magari ya uokoaji kutoka jijini Arusha yakiwa yameishiwa mafuta na kusababisha uokoaji kuzorota.

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magesa Mulongo amelazimika kusitisha safari yake mkoani Tanga baada ya kupata taarifa ya tukio hilo na baadaye alitangaza kwamba Serikali imeamua kufunga machimbo yote ya `moramu’ hadi pale itakapotoa tamko lingine.

Akizungumza eneo la tukio, Mulongo alisema tukio hilo ni la kusikitisha kwa kuwa vijana waliokufa ni wengi.
Kwa upande wake mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema aliitaka Serikali kuweka utaratibu wa kukabiliana na matukio ya aina hiyo ikiwa ni pamoja na kuweka viashiria vya usalama maeneo ya machimbo.

Kiongozi mwingine aliyefika katika eneo hilo ni Meya wa Jiji la Arusha, Gaudence Lyimo ambaye alisema kwa sasa ni muda mwafaka wa kufunga mgodi huo kwa kuwa mwaka 1997 tukio kama hilo lilitokea na kuua watu saba kwa kufukiwa na kifusi.

Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nasari aliilamikia Serikali kwa kutokuwa na ofisi ndogo za vitengo vya maafa mikoani na kudai kuwa endapo ofisi hizo zingekuwapo uokoaji ungekuwa rahisi.

Wananchi wafurika

Wananchi kutoka viunga mbalimbali vya Jiji la Arusha walijitokeza kwa wingi kushuhudia kazi za uokoaji zikiendelea bila kujali mvua kubwa iliyokuwa ikinyesha.
Wananchi hao walionekana kushirikiana katika uokoaji ambapo ilipofika saa 10.00 jioni, wanajeshi zaidi kutoka Kambi ya 977KJ na Sopa Monduli walifika kuongeza nguvu.

Wakizungumzia tukio hilo, baadhi ya wananchi waliitupia lawama Serikali kwa kushindwa kuweka usimamizi mzuri wa machimbo hayo licha ya tukio kama hilo kuwahi kutokea siku za nyuma.

“Hii ni mara ya pili kwa machimbo haya kusababisha vifo. Mwaka 1997 tulishuhudia machimbo haya yakiporomoka na watu kufunikwa ndani lakini hakuna hatua iliyochukuliwa mpaka leo tunashuhudia haya tena. Ni lazima Serikali iwajibike kutokana na mauaji haya,”alisema mzee aliyejitambulisha kwa jina la Christoper Laizer.



MWANANCHI

No comments

Powered by Blogger.