SAMAKI WABOVU WAIELEMEA SERIKALI

Afya za baadhi ya Watanzania ambao ni walaji wa kitoweo aina ya samaki zimeendelea kuwa hatarini kutokana na kuwapo kwa dalili kwamba Serikali imeshindwa kudhibiti uwepo wa samaki wabovu katika soko la ndani, wanaoingizwa kutoka nje ya nchi.
Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi pamoja na taasisi nyingine zinazohusika na udhibiti wa viwango na ubora wa samaki, kwa nyakati tofauti wametoa taarifa ambazo hazionyeshi hatua wanazochukua kudhibiti samaki hao, huku kukiwa na uthibitisho wa kuwapo kwa samaki wabovu katika baadhi ya kampuni zinazofanya biashara hiyo.
Itakumbukwa gazeti hili katika toleo la Jumamosi, Septemba 28, liliandika kuwapo kwa samaki hao sokoni, wakiuzwa kwa wingi na kwa bei ya chini katika Soko Kuu la Kimataifa la Feri, Dar es Salaam, lakini taarifa hiyo ilikanushwa na Katibu Mkuu wa Chama cha Waingizaji wa Samaki Tanzania, Barnabas Mapunda kupitia baadhi ya magazeti ya kila siku.

ENDELEA KUSOMA HABARI HII KWA KUBOFYA HAPA CHINI
 Mapunda huku akitetea vyombo vya Serikali vinavyohusika na ukaguzi, alisema: "Napenda kuchukua fursa hii kukanusha taarifa hiyo (Samaki hatari waingizwa nchini) na kuufahamisha umma wa Watanzania si kweli kuwa samaki wanaoingizwa kutoka nje ya nchi hawakidhi ubora na usalama kwa matumizi ya binadamu."
Hata hivyo, siku chache baadaye Mamlaka ya Chakula na Dawa Tanzania (TFDA), ilikamata kilo 7,500 za samaki aina ya vibua walioharibika ambao waliingizwa nchini Julai mwaka huu na Kampuni ya Sais Boutique kutoka China.
Kadhalika maelezo ya Mapunda yanatofautiana na kile ambacho gazeti hili limekibaini ndani ya Kampuni ya Alpha Krust Ltd ya Dar es Salaam ambayo taarifa zake za ndani zinathibitisha kuwapo kwa samaki walioingizwa nchini ambao hawafai kwa matumizi ya binadamu.
Uchunguzi ulibaini kuwa samaki hao (Frozen Pacific Mackerel W/R (Scomber Japonicus) waliingizwa nchini Agosti 29, 2013 kutoka Korea Kusini na Kampuni ya Wookyung Co. Ltd: 1851 Jangheung –don, Nam-gu ya jijini Pohang na waliagizwa na Kampuni ya Alphakrust Ltd ya Dar es Salaam.
Taarifa zaidi zinaonyesha kuwa mzigo huo ulibebwa na Kampuni ya Mediterranean Shipping (T) Ltd. Taarifa zaidi zinaonyesha kuwa samaki hao walizalishwa Juni 4, 2013 na tarehe ya mwisho kutumika ilitakiwa kuwa Juni 3, 2014. Hata hivyo, chanzo cha kuaminika katika kampuni hiyo kimebainisha kuwa tarehe hizo hazina uhalisia kwani samaki hao walikuwa wameshaharibika na kuwa hizo 'sticker' huwa wanabandika tu, lakini ukweli ni kwamba samaki wanakuja wakiwa wameshaharibika ndiyo maana huwa wanauzwa kwa bei ya chini, kilibainisha chanzo hicho na kuongeza:
"Kuna samaki walioharibika wa aina mbili, kwanza kuna walioathiriwa na mionzi na kuna wale waliokaa muda mrefu. Hawa waliopo ni waliokaa muda mrefu na ukitaka kuwajua hao samaki, watoe katika barafu na kuwaloweka, utaona wanapasuka na ukitia kidole wanabonyea. Athari yake kubwa ni ugonjwa wa saratani ya matumbo," kilieleza chanzo chetu.
Katika taarifa ya ukaguzi wa kitengo cha ubora cha kampuni hiyo (Organoleptic Assessment) uliofanyika Septemba 12, 2013 (nakala tumeiona), sampuli nne za samaki zilithibitika kutofaa kabisa kwa matumizi ya binadamu.
Uongozi wa Alphakrust
Mkurugenzi wa Kampuni ya Alphakrust, Veda Gire alisema kabla ya kuuza samaki wanapitia kwenye taratibu zote za Serikali ikiwemo ukaguzi wa kina kutoka kwa mamlaka husika.
"Hao ambao wamepata samaki wabovu na wanaamini wametoka kwangu walete ushahidi, lakini mimi ninachojua mamlaka husika zimethibitisha kuwa wapo safi na ndiyo maana nauza na watu wanakula," alisema Gire.
Alipoelezwa kuhusu taarifa ya ukaguzi wa ndani ya kampuni yake, Gire alisema: "Taarifa ya ukaguzi ya ndani ni siri ya kampuni, kwa hiyo huwezi kufahamu aina ya vigezo tunavyotumia kufanya ukaguzi wetu wa ndani, hiyo ni siri ya kampuni. "Kama unataka kufahamu tunavyofanya kazi, wewe njoo hapa kwenye kampuni yetu, tutakuonyesha kila kitu, hata wale wenzako (waandishi wa Mwananchi) walionipigia simu wiki iliyopita niliwaalika waje hapa waone, hakuna siri," aliongeza.
Msemaji wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Roida Andusamile amekiri kuwa shirika hilo lilikutana na samaki hao kabla hawajaletwa nchini.
"Ni kweli tulifanya ukaguzi wa samaki wa Alpha Krust Agosti 6 mwaka huu kabla ya kuingia nchini na tuliwapa cheti cha ubora. Sasa labda kama walikuja kuharibikia nchini baada ya kuingizwa," alisema na kuongeza:
"Tuna utaratibu ulioanza mwaka jana wa kukagua mizigo kabla haijaingizwa nchini (Pre-shipment verification of conformity to standard) na tunashirikiana na kampuni za kimataifa kama vile SBS la Uswisi, Bureauveritas la Ufaransa na Intertec la Uingereza. Mwagizaji akishakaguliwa hupewa 'conformity certificate', hata akifika nchini tunaangalia cheti tu".
Kwa upande wake, Mkaguzi wa Kanda wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA), Emmanuel Alfonse amebainisha kuwemo kwa udhaifu katika ukaguzi hasa bandarini wakati alipokuwa akieleza uingizwaji wa bidhaa za vyakula nchini.
"Pale bandarini kuna idara tano zinazokagua, wapo watu wa bandari, tupo TFDA, wapo TBS, wakala wa mionzi na Idara ya Usalama wa Taifa. Wote tunafanya kazi chini ya baba yetu mmoja," alisema huku akisita kumtaja huyo 'baba'.
"Hata hivyo bado mizigo bado inaweza kupenya bila kukaguliwa, ndiyo maana tulikamata samaki kule Tabata," aliongeza. Akizungumzia kampuni inayotajwa kuingiza samaki hao, Alfonse alisema, hata kama samaki hao waliharibikia kiwandani hapo, bado kampuni hiyo ilipaswa kufuata utaratibu.
"Kama hao samaki waliingizwa Agosti 29 na Septemba 12 wakabainika kuharibika, mmiliki alipaswa kuwasiliana na Ofisa Afya wa Manispaa ili apewe kibali cha kuwateketeza. Tutafuatilia walikopelekwa, isije ikawa waliepelekwa sokoni," alisema.
Msemaji wa TFDA, Gaudensia Simwanza alisema kabla ya mzigo kuingizwa nchini, mwingizaji anapaswa kuomba kibali.
Hata hivyo, alisema kuna changamoto kubwa ya wafanyabiashara hao kukwepa ukaguzi hasa wanapoingiza mzigo.
"Hiyo ni changamoto kubwa, kwa sababu mzigo ukishaingia mwingizaji anatakiwa atujulishe na wakaguzi huchukua samaki na kwenda nao maabara kuwapima. Kama yule tuliyemkamata wiki iliyopita, Sais Boutique hakukaguliwa wakati wa kuingiza," alisema Simwanza.
Kwa upande wake, Ofisa Afya wa Manispaa ya Ilala, Ali Adinan alikiri kuwa kiwanda hicho kipo eneo la Ilala lakini akasema hana taarifa ya kuwepo kwa samaki wabovu.
"Hatuna taarifa ya kuwepo samaki hao... tunafanya ukaguzi kila mara na hata tuliposikia taarifa za kuwepo samaki wabovu sokoni tulifanya ukaguzi katika kiwanda hicho lakini hatukukuta kitu. Labda kwa kuwa umetupa taarifa tufuatilie tena," alisema Adinan.
Kauli ya TPA, Waziri
Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) kupitia taarifa yake ya Septemba 22 mwaka huu, imekanusha kuhusika na uingizwaji wa samaki wabovu nchini na kwamba haina jukumu la kukagua mizigo bandarini.
Kaimu Meneja Mawasiliano wa TPA, Janeth Ruzangi, alisema jukumu la mamlaka hiyo ni kupakua na kupakia mizigo melini na kwamba mizigo inayopakuliwa huhifadhiwa sehemu maalumu kusubiri wahusika ambao hukabidhiwa baada ya kukamilisha taratibu zinazotakiwa.
"Kwa mizigo kama hii ya chakula chenye kukaa kwenye barafu au baridi, kawaida huwa inapakiwa kwenye makontena maalumu ya baridi (refrigerated containters).
"Mara inapokuwa imeshushwa bandarini huwekwa kwenye sehemu ya umeme kwa kiwango cha baridi (reefer points) ambacho mwenye meli ataagiza kiwekwe kulingana na vile ilivyokuwa ndani ya meli kabla ya kushushwa na Maafisa wa Bandari kukagua kila baada ya saa mbili ili kuhakikisha hakuna mabadiliko ya kiwango cha baridi na endapo patatokea hitilafu ya umeme, majenerata yataendelea kutoa umeme," alieleza Ruzangi.
Alisema baada ya mwenye mizigo kupata nyaraka zote husika ndipo TPA itaruhusu mzigo huo kutoka kupitia katika milango yake iliyopo bandarini na si vinginevyo.
Naye Waziri wa Maendeleo ya Uvuvi na Mifugo, Dk David Mathayo David, amekuwa akisita kuzungumza na gazeti hili kila anapotafutwa kwa njia ya simu.
Septemba 13, mwaka huu alipotafutwa alisema: "Niko njiani naendesha hivyo siwezi kutolea ufafanuzi suala hilo". Oktoba 10 alipopigiwa tena simu alisema: "Kwa sasa siwezi kuzungumzia suala hili, ila kesho (Oktoba 11) nitakuwa na press conference (mkutano na waandishi wa habari), nitaeleza kwa kirefu".
Alipopigiwa simu, Oktoba 11 na kuulizwa kuhusu wapi mkutano huo utafanyika alijibu kuwa mkutano huo umeahirishwa.
Hata hivyo siku hiyo hiyo alifanya mkutano huo na waandishi wengine ofisini kwake jijini Dar es Salaam, ambapo pamoja na mambo mengine alizungumia uingizwaji wa samaki hatarishi kutoka nje ya nchi.
"Baadhi ya wafanyabiashara wa samaki hawazingatii kanuni za uvuvi hususan katika usafirishaji wa samaki. Kuna wengine magari wanayotumia hayana majokofu na mengine huwa wazi kwa hiyo samaki huwa wanaingia vumbi na moja kwa moja hukosa matunzo mazuri.
"Pia uuzaji wa samaki kwa njia ya mnada unachangia uharibifu kwa kuwa mara nyingi huchomwa na jua kali wakati samaki muda mwingi wanahitaji baridi kutokana na kuwa na protini nyingi,"alisema Dk Mathayo.
Aliongeza Serikali haiwezi kuacha kuagiza samaki kutoka nje ikizingatiwa ni sehemu ya uchangiaji wa pato la taifa lakini pia huwapa faida kubwa wafanyabiashara wa ndani.
Alisema samaki wanapowasili nchini serikali kwa kushirikiana na TFDA, huwathibitisha kabla ya kuwaruhusu kuingizwa sokoni.

No comments

Powered by Blogger.