UPDATES: WANAFUNZI 212 WA UASKARI CHUO CHA TAALUMA YA POLISI MOSHI WAFUKUZWA BAADA YA KUBAINIKA KUTUMIA VYETI FEKI

Na Dixon Busagaga

CHUO cha mafunzo ya taaluma ya Jeshi la polisi Moshi (MPA), kimewafukuzisha mafunzo jumla ya wanafunzi wa uaskari 212, kutokana na sababu za kughushi vyeti vya elimu ya sekondari..

Hayo yamesemwa leo na Mkuu wa Taaluma na Utumishi wa jeshi la Polisi, Kamishna wa Polisi Thobias Andengenye katika kikao na waandishi wa habari kilichofanyika kwenye ukumbi wa chuo cha mafunzo ya taluma ya Polisi mjini Moshi, mkoani Kilimanjaro.

Kamishna Andengenye alisema Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na Baraza la Mitihani la Taifa (NECTA), lilifanya uhakiki wa Vyeti vya wanafunzi wote 3,415 waliojiunga na mafunzo hayo Desemba mwaka jana ambapo waligundua kuwa wanafunzi 212 kati yao hawakuwa na sifa kutokana na
sababu za kughushi vyeti.

"Katika kuhakikisha kwamba tunaendelea kuwa na askari wenye ueledi na uaminifu kwa raia na taifa kwa ujumla, tuliendelea na zoezi la kuhakiki vyeti kwa kushirikiana na baraza la mitihani la taifa, ambapo
vyeti vya wanafunzi wa uaskari 212 kati ya walioripoti vimeonekana kuwa ni vya kughushi," alisema Andengenye.

Alisema kufuatia hali hiyo pamoja na kuwaachisha mafunzo wanafunzi hao 212, Jeshi la Polisi nchini kwa kushirikiana na taasisi nyingine linaendelea kufanya upelelezi ili kuhakikisha kuwa hatua za kisheria zinachukuliwa dhidi ya wanafunzi hao na maaskari wote watakaobanika kughushi vyeti.

No comments

Powered by Blogger.