MKURUGENZI WA THE GUARDIAN NA MHARIRI WA NIPASHE, WAITWA POLISI

Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai, Kanda Maalum ya Dar es Salaam, (ZCO), Jafar Ibrahim, (Kulia), akizungumza na Mwanasheria wa kampuni ya The Guardian, Gladis Frimbari (Wapili kulia), Mkurugenzi Mtendaji wa The Guardian, Kiondo Mshana, (Wa pili kushoto) na Mhariri Mtendaji wa Nipashe, Jesse Kwayu, (Wa kwanza kushoto), ofisini kwake jijini. Kachero huyo aliwaomba radhi viongozi hao wa The Guardian, kutokana na makosa ya kuwaita polisi kwa mahojiano kuhusiana na habari iliyochapishwa na Nipashe ikiwahusisha polisi wa pikipiki na vitendo vya rushwa, na kwamba Polisi haina tatizo na habari hiyo. (Picha kwa Hisani ya The Guardian)
Mkurugenzi Mtendaji wa The Guardian Limited, Kiondo Mshana, (Katikati), Mhariri Mtendaji wa Nipashe, Jesse Kwayu, wakiwa kwenye Ofisi ya Mkuu wa Upelelezi Makosa ya Jinai, Kanda Maalum ya Dar es Salaam, ZCO, Jafar Ibrahim jijini. Hata hivyo Mkuu huyo wa upelelezi, aliomba radhi kwa vile wito huo ulitolewa kimakosa, ukiwataka wakuu hao kufika polisi kwa mahojiano kuhusu habari iliyochapishwa na Nipashe, ikiwahusisha polisi wa pikipiki na ulaji rushwa.

ENDELEA KUSOMA HABARI HII KWA KUBOFYA HAPA CHINI




RAMADHANI  TEMBO  NA ZAWADI  CHOGOGWE


ASKARI wa Jeshi la Polisi Kikosi  cha Pikipiki (Tigo), wamezua  sintofahamu  baada ya wananchi kutoa malalamiko yao juu ya  askari hao kuonekana sehemu mbalimbali wakikamata magari na Pikipiki na kudaiwa  kuomba na kupokea rushwa  kutoka kwa madereva .

Wananchi  wamekuwa wakilalamika juu ya askari hao kuhusika  kuomba na kupokea rushwa   na kuvunja  sheria  za Jeshi hilo na kulidhalilisha na kushindwa kuwajibika katika kulinda usalama wa raia na mali zao.

Kutokana na malalamiko hayo, gazeti la Nipashe liliandika kuhusiana na malalamiko hayo katika toleo la Julai  8, mwaka huu katika ukurasa wa kwanza, gazeti  hilo lilieleza matukio mbalimbali yanayofanywa na kikosi hicho huku wakiliomba Jeshi la Polisi kulifanyia kazi suala hilo.

 Kutolewa kwa taarifa hiyo, Jeshi  hilo  mnamo  Julai 21 mwaka  huu lilituma  barua ya  wito kwa Mhariri Mtendaji  wa  gazeti  hilo, Jesse  Kwayu  iliyomtaka afike jana saa nne asubuhi  Ofisi ya Mkuu wa Upelelezi  Kanda Maalum ya Dar es Salaam kwa mahojiano kuhusiana  na toleo  hilo.

Baada ya kupata barua hiyo, Mkurugenzi wa gazeti hilo, Kiondo Mshana akiongozana na Mhariri mtendaji Jesse Kwayu pamoja na mwanasheria wao Gladiys Fimbari ,  waliitikia wito huo na kufika ofisini hapo kwa ajili ya mahojiano hayo.

Kabla ya kuanza kwa mahojiano hayo, Kamishna Msaidizi wa Jeshi la Polisi ambaye pia ni Mkuu wa Upelelezi Kanda Maalum ya Dar es Salaam Jafari Mohamed,alisema kuwa barua hiyo iliandikwa kimakosa kwa kuwa hakuna tuhuma zozote kuhusiana na toleo lililotolewa na gazeti hilo.

Alisema kuwa lengo la barua hiyo ilikuwa ni kutaka ufafanuzi dhidi ya  malalamiko ya Wananchi yanayohusiana  na vitendo vya kuomba na kupokea rushwa vinavyofanywa na kikosi hicho.

“Tunawaomba radhi kwa usumbufu uliyojitokeza na kuacha majukumu yenu ya kazi na suala hili litashugulikiwa na ofisi na kuwachukulia hatua za kisheria askari hao”alisema.

Kwa upande wake Mhariri Mtendaji wa gazeti hilo alisema kuwa kutokana na utendaji mbovu wa askari hao iliwalazimu waandike taarifa hizo, lakini cha kushangaza Julai 21 walipata barua hiyo inayowataka wafike kwa mahojiano na baada ya kufika hapo ilionekana barua hiyo imekosewa,hivyo wamekubali kuombwa radhi na watashiriakiana na Jeshi hilo kutoa taarifa zozote za uhalifu.

No comments

Powered by Blogger.