MWANAFUNZI AJIUA KWA SHUKA HOSPITALINI MKOANI KAGERA

KATIKA hali isiyotarajiwa, mwanafunzi wa Kidato cha Tano katika Shule ya Sekondari ya Wavulana Ihungo Manispaa ya Bukoba mkoani Kagera, Ezra Gerald (19), amejinyonga hadi kufa kwa kutumia shuka ya hospitali, alikokuwa amelazwa kwa kile kinachoeleza alikuwa anasumbuliwa na homa ya matumbo.
Hata hivyo, ujumbe ulioachwa na marehemu huyo unaonesha alichukua uamuzi huo, kutokana na kuchukizwa na uamuzi wa daktari aliyemhudumia wa kumlaza ili atibiwe ugonjwa ambao hakuwa anaumwa.
Aidha, katika ujumbe huo imeelezwa alichukizwa na kitendo cha kupotezewa muda hospitalini wakati wenzake wakiendelea na masomo.
Tukio hilo limethibitishwa na Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Kagera, Gilles Muroto aliyesema mwanafunzi huo alijinyonga Septemba 16 mwaka huu saa moja asubuhi.
Alisema mwili wake uligundulika ukining’inia kwenye mti uliopo maeneo ya hospitali hiyo na alipopekuliwa katika mifuko ya suruali yake, zilionekana karatasi mbili, moja ikiwa na ujumbe uliosomeka;
“Haiwezekani binadamu kuhudumiwa kama mbwa, yaani nafika hospitali najieleza hali yangu halafu daktari ananiandikia kulazwa bila kupima, sasa sijui wanatibu nini?
“Kwa kweli siwezi kuvumilia wenzangu wanasoma halafu mimi nimekalishwa tu hapa hospitali bila kujua wananitibu nini, inaniuma sana mpaka nafikia hatua hii ya kujiondoa duniani kwa sababu naona watu wanachezea ndoto zangu, mimi siwezi kuona ndoto yangu inazimwa wakati natakiwa niwepo shuleni nikamilishe ndoto zangu “mjitahidi tukutane mbinguni “Respect My Family and Brother Henry.”

ENDELEA KUSOMA HABARI HII KWA KUBOFYA HAPA CHINI

Kamanda Muroto amesema hakuna aliyekamatwa kuhusiana na tukio hilo, lakini polisi wanaendelea na uchunguzi.
Inaelezwa mwanafunzi huyo aliyetajwa kuwa ni mwenyeji wa mkoa wa Tabora, alilazwa hospitalini hapo tangu Septemba 11 mwaka huu.
Kwa mujibu wa Katibu wa Hospitali ya Mkoa wa Kagera, Benges Justus, tukio hilo lilitokea Septemba 16, mwaka huu, siku moja baada ya mgonjwa huyo kulazwa.
Alisema baada ya mwanafunzi huyo kupokelewa hospitalini hapo, alifanyiwa vipimo vyote vya kitabibu na kugundulika anasumbuliwa na malaria, ndipo akaanzishiwa tiba ya ugonjwa huo.


CHANZO: HABARI LEO

No comments

Powered by Blogger.