HABARI

Theme images by kelvinjay. Powered by Blogger.

MATUKIO

MICHEZO

SIASA

» »Unlabelled » Mkutano wa JK, wabunge CCM waamsha makundi ya urais

 

Dodoma/Dar. Mkutano wa ndani baina ya Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete na wabunge wa chama hicho uliofanyika Jumapili iliyopita mjini Dodoma, ni kama umeamsha upya makundi ya kuwania urais wa 2015, Mwananchi limebaini.
Kutokana na hali hiyo, jana chama hicho kililazimika kutumia nguvu kubwa kudhibiti taarifa zinazohusu kauli iliyodaiwa kuwa ilitolewa na Rais Kikwete, kwamba “Wanaoutaka urais kupitia CCM waanze kujipitisha ilimradi wasiwagawe wanachama kwa misingi ya makundi.”
Taarifa kuhusu ruksa hiyo inayodaiwa kutolewa na Rais, ndizo zilizotikisa vichwa vya habari katika magazeti ya juzi na jana lakini Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye anasema siyo za kweli na kwamba Rais alilishwa maneno.
Nape jana katika mkutano na Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam alisema: “Wamemlisha maneno mwenyekiti wetu...inaelekea kuna kikundi cha watu wana mgombea wao wa kuchonga ambaye bila shaka anapungukiwa na sifa, hivyo wanajaribu kumwongezea sifa kwa kumlisha mwenyekiti maneno na kuwapa baadhi ya waandishi, uhuni huo haukubaliki.”
Wakati Nape akitoa kauli hiyo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Steven Wassira akizungumza bungeni jana pia alisema taarifa kuhusu mkutano wa Rais Kikwete na wabunge zilipotoshwa, huku akitaka suala hilo lifafanuliwe na watendaji wa CCM.

JK na wabunge
Nape alisisitiza katika mkutano huo Rais Kikwete alisema ni marufuku kwa mwanachama anayetaka kugombea kwenye uchaguzi wa dola kujipitishapitisha na kufanya kampeni kabla ya wakati.
Habari kutoka ndani ya mkutano huo zinasema chimbuko la hoja ya watu wanaotaka kujinadi kwa ajili ya uongozi iliibuliwa na Mbunge wa Same Mashariki, Anna Killango Malecela na Mbunge wa Lupa, Victor Mwambalaswa ambao walihoji juu vikao vinavyofanywa na watu wanaosaka urais kupitia CCM kwa kuwashirikisha watendaji wa chama na Serikali.

Majibu ya Kikwete
Baadhi ya wabunge wameliambia gazeti hili kuwa Rais Kikwete katika mkutano huo alieleza kusikitishwa na kampeni za urais ambazo alisema zinakigawa chama.
“Sisi tunashangazwa na taarifa ambazo magazeti mmeziandika, ukweli ni kwamba mheshimiwa Rais alituasa kwamba tusikigawe chama na kwamba asingependa tuwe na mgombea mwenye makovu ifikapo 2015,” alisema mmoja wa wabunge.
Vyanzo vyetu hivyo vilimnukuu Rais Kikwete akisema: “Mnaumizanaa wee, sasa inaweza kufika hiyo 2015 tutajikuta tukiwa na wagombea wenye plasta, sasa ikifikia hapo sijui tutaanza kumuuza mgombea wetu au kutibu majereha kwanza?”

Sitta aja juu
Wakati hayo yakielezwa, Mbunge wa Urambo Mashariki, Samuel Sitta ameibuka na kusema kuwa kitendo cha kuruhusu wagombea wa urais kujitangaza sasa ni hatua ambayo inaweza kuwagawa Watanzania.
“Mimi sikuelewa hivyo, ni tafsiri fulani hivi tu za watu wachache wenye masilahi yao, na wanaoishabikia hiyo ni wenye mapesa mengi wanaoweza kufanya kampeni kwa muda mrefu,” alisema Sitta.
“Nimempigia Katibu Mkuu wetu atupe mwongozo katika hili, ikiwezekana kwa maandishi ili ijulikane wazi nini kinapaswa kufanyika na nini hakipaswi.”


MWANANCHI

«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post

No comments: