HABARI

Theme images by kelvinjay. Powered by Blogger.

MATUKIO

MICHEZO

SIASA

Ecobank Group Yaweka Rekodi ya Ongezeko la Mikopo kwa Biashara za Wanawake Afrika




Ecobank Group imetangaza ukuaji mkubwa wa mikopo, likilenga kuimarisha ujasiriamali wa wanawake barani Afrika. Ecobank imerekodi ongezeko kubwa la asilimia 194 katika utoaji wa mikopo kwa biashara zinazoongozwa na wanawake, likifikia dola za Marekani milioni 780 mwaka 2025 kutoka dola milioni 265 mwaka 2024. Hatua hii inaashiria mafanikio ya juhudi za benki hiyo katika kukuza usawa wa kijinsia na kuimarisha uchumi wa ndani barani Afrika.

Taarifa hiyo ilitolewa wakati wa uzinduzi wa Ripoti ya Programu ya Jinsia ya Ecobank, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya International Women’s Day 2026.

Wataalamu wa uchumi wanaeleza kuwa wanawake wajasiriamali wana mchango mkubwa katika kukuza ajira, kusaidia familia na kuimarisha minyororo ya thamani ya ndani. Hata hivyo, biashara nyingi zinazoongozwa na wanawake bado zinakabiliwa na changamoto ya upatikanaji wa mitaji, huku pengo la ufadhili likikadiriwa kufikia dola bilioni 42 barani Afrika.

Ili kukabiliana na changamoto hiyo, Ecobank imeendelea kuwekeza katika mipango maalum inayolenga wanawake kwa kutoa mikopo rafiki, mafunzo ya biashara, ushauri na fursa za kuunganishwa na masoko ya kikanda. Lengo ni kuwasaidia wanawake kukuza biashara endelevu na zenye ushindani.

Moja ya mipango hiyo ni programu ya Ellevate, iliyoanzishwa mwaka 2020 kusaidia biashara za wanawake zilizoathiriwa na janga la COVID-19. Programu hiyo sasa imekua na kuwa moja ya miradi mikubwa zaidi barani Afrika, ikihudumia zaidi ya wanawake wajasiriamali 103,000 katika nchi 26. Zaidi ya wanawake 21,000 wamejiunga na mpango huo mwaka 2025 pekee, huku zaidi ya 24,000 wakinufaika na mafunzo na ushauri wa kibiashara.

Aidha, Ecobank imezindua programu ya MAMA inayolenga kuwasaidia wanawake wanaofanya biashara katika sekta isiyo rasmi, kwa kuwapatia mikopo nafuu na kuwasaidia kuingia katika mfumo rasmi wa kifedha. Mpango huo tayari umewafikia zaidi ya wanawake 10,000, huku zaidi ya 2,000 wakipata mikopo yenye thamani ya zaidi ya dola milioni 1.8.

Katika juhudi za kuongeza upatikanaji wa mtaji, Ecobank pia ilizindua hati fungani maalum ya jinsia nchini Côte d’Ivoire mwaka 2025, iliyokusanya zaidi ya faranga za CFA bilioni 11 ndani ya saa 48. Fedha hizo zinatarajiwa kusaidia kutoa mikopo kwa zaidi ya biashara 1,200 ndogo na za kati zinazomilikiwa na wanawake.

Akizungumza kuhusu mafanikio hayo, Mkurugenzi Mtendaji Mkuu wa Kundi la Ecobank, Jeremy Awori alisema wanawake wajasiriamali ni mhimili muhimu wa ukuaji wa uchumi wa Afrika, lakini bado wanakumbana na changamoto za upatikanaji wa fedha.

“Ecobank inaendelea kushughulikia changamoto hiyo kwa kuunganisha mitaji, ujuzi na fursa za masoko kupitia mtandao wake wa bara zima. Ongezeko hili linaonyesha wazi mahitaji makubwa ya huduma hizi na mafanikio ya programu zetu,” alisema.

Kwa siku zijazo, Ecobank inapanga kupanua zaidi programu ya Ellevate katika masoko yote inayofanya kazi, kuimarisha huduma zisizo za kifedha kama zana za kidijitali, pamoja na kuanzisha bidhaa mpya zitakazolenga wanawake ili kuongeza ushiriki wao katika uchumi wa Afrika.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu Yakagua Maendeleo ya Ujenzi wa Chuo cha Usafiri wa Anga (CATC)

 


Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) imetembelewa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kwa lengo la kukagua eneo la mradi wa ujenzi na kujionea maendeleo ya ujenzi wa Majengo ya Kisasa ya Chuo cha Usafiri wa Anga (CATC) yaliyopo Banana–Ukonga, jijini Dar es Salaam.

Ziara hiyo ya kikazi iliongozwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, Mhe. Selemani Kakoso, ambapo wajumbe wa Kamati walipata fursa ya kukagua hatua mbalimbali za utekelezaji wa mradi na kujionea hali ya maendeleo ya ujenzi unaoendelea.

Katika ziara hiyo, Kamati ilipongeza jitihada za TCAA katika kusimamia utekelezaji wa mradi huo na kuisisitiza Mamlaka kuendelea kumsimamia kikamilifu mkandarasi anayetekeleza ujenzi ili kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati na kwa kuzingatia viwango vilivyokubalika.

Kwa upande wake, Waziri wa Uchukuzi, Mhe. Prof. Makame Mbarawa, alisema kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inaendelea kuwekeza katika sekta ya usafiri wa anga kupitia ujenzi, ukarabati na upanuzi wa miundombinu ya anga pamoja na kuimarisha mifumo ya usimamizi, akibainisha kuwa rasilimali watu yenye ujuzi wa hali ya juu ni msingi wa ukuaji na usalama wa sekta hiyo.

Akizungumza kwa niaba ya TCAA, Mkurugenzi Mkuu wa TCAA, Salim Msangi alibainisha kuwa CATC ina upekee wa kimkakati kwa kuwa ni miongoni mwa vyuo tisa barani Afrika vinavyotambuliwa katika kutoa mafunzo ya usalama wa usafiri wa anga, hali inayoliweka Taifa katika nafasi muhimu ya kikanda na kimataifa katika ukuzaji wa utaalamu wa anga.

“Mradi huu unaimarisha nafasi ya CATC kama kitovu cha ubora wa mafunzo ya usalama wa anga barani Afrika na ni uwekezaji wa moja kwa moja katika usalama na maendeleo endelevu ya sekta ya usafiri wa anga nchini,” alisema.
Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu wakitembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa mradi wa ujenzi wa Chuo cha Usafiri wa Anga (CATC) unaendelea katika eneo la Banana, jijini Dar es Salaam.
 Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu ikiongozwa na Mwenyekiti wake, Selemani Kakoso na Menejimenti ya TCAA ikiongozwa na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Bw. Salim Msangi wakisiliza maelezo kuhusu ujenzi wa mradi wa Chuo cha Usafiri wa Anga (CATC) yaliyokuwa yanatolewa na Meneja mradi wa Chuo cha CATC, Mhandisi Stephen Mwakasasa.
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, Selemani Kakoso akizungumza mara baada ya kutembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa mradi wa ujenzi wa Chuo cha Usafiri wa Anga (CATC) unaendelea katika eneo la Banana, jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Uchukuzi Mhe. Prof. Makame Mbarawa akizumgumza kuhusu namna wizara inavyosimamia mradi wa Ujenzi wa Chuo cha Usafiri wa Anga (CATC) kinachojengwa katika eneo la Banana, jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) Salim Msangi akizungumza kuhusu maendelea ya mradi wa Ujenzi wa Chuo cha Usafiri wa Anga (CATC) kinachojengwa katika eneo la Banana, jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu pamoja na watumishi wa TCAA wakiwa kwenye kikao mara baada ya kamati hiyo kutembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa mradi wa ujenzi wa Chuo cha Usafiri wa Anga (CATC) unaendelea katika eneo la Banana, jijini Dar es Salaam.
Ujenzi ukiendelea

TCAA YAANDAA IFTAR MAALUM KWA WATOTO WENYE UHITAJI


Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) imeandaa futari maalum kwa watoto wenye uhitaji kutoka Kituo cha Kulea Watoto wenye Uhitaji cha Zili, tukio lililolenga kuimarisha mshikamano wa kijamii na kuendeleza ujumuishi kwa makundi yenye mahitaji maalum.

Hafla hiyo ilifanyika katika Makao Makuu ya TCAA jijini Dar es Salaam, na kuhudhuriwa na wadau wa sekta ya usafiri wa anga, watumishi wa TCAA pamoja na watoto wenye uhitaji. Wageni walishiriki futari kwa pamoja na watoto hao, pamoja na kukabidhi zawadi kama ishara ya upendo, mshikamano na uwajibikaji wa kijamii.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mgeni Rasmi Naibu Waziri wa Uchukuzi Mhe. David Kihenzile, aliyemwakilisha Waziri wa Uchukuzi, alipongeza jitihada za TCAA katika kuchangia maendeleo ya jamii akisisitiza umuhimu wa taasisi za umma kushiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii, hususan zinazolenga kuwajali watoto wenye uhitaji.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TCAA, Salim Msangi alisisitiza kuwa pamoja na jukumu la kusimamia na kudhibiti sekta ya usafiri wa anga, mamlaka itaendelea kutekeleza miradi ya kijamii inayolenga kugusa maisha ya wananchi na kukuza maadili ya utu, mshikamano na usawa.

Kupitia futari hii maalum, TCAA imeendelea kudhihirisha kuwa sekta ya usafiri wa anga siyo tu kuhusu usimamizi na kanuni, bali pia ni chombo muhimu cha kujenga jamii jumuishi, yenye huruma na mshikamano.
Naibu Waziri wa Uchukuzi David Kihenzile pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) Salim Msangi wakikabidhi mkono wa mwezi mtukufu kwa  watoto wenye uhitaji kutoka Kituo cha Kulea Watoto wenye Uhitaji cha Zili ikiwa ni kuimarisha mshikamano wa kijamii na kuendeleza ujumuishi kwa makundi yenye mahitaji maalum.
Naibu Waziri wa Uchukuzi David Kihenzile  akitoa neno wakati wa futari iliyoandaliwa na Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA)
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) Salim Msangi akizungumza na baadhi ya wafanyakazi wa TCAA, wadau mbalimbali wa Usafiri wa Anga pamoja na watoto wenye uhitaji kutoka Kituo cha Kulea Watoto wenye Uhitaji cha Zili wakati wa hafla ya futari iliyoandaliwa na TCAA.
Baadhi ya wafanyakazi wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), wadau mbalimbali wa Usafiri wa Anga pamoja na watoto wenye uhitaji kutoka Kituo cha Kulea Watoto wenye Uhitaji cha Zili wakiwa kwenye hafla ya futari iliyoandaliwa na TCAA.
Mjumbe wa Bodi ya TCAA Vuai A. Hilal akitoa neno la shukrani  kwenye hafla ya futari iliyoandaliwa na TCAA.
Picha za pamoja

TGNP YAADHIMISHA SIKU YA WANAWAKE DUNIANI, YAHIMIZA USAWA WA KIJINSIA KUFIKIA DIRA 2050


Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) umeadhimisha Siku ya Wanawake Duniani 2026 kwa kufanya kongamano maalum lililofanyika tarehe 11 Machi 2026 katika Viwanja vya TGNP, Mabibo jijini Dar es Salaam, likilenga kuhamasisha haki na usawa kwa wanawake na wasichana kama msingi wa maendeleo jumuishi ya taifa.

Akizungumza katika maadhimisho hayo, Mwenyekiti wa Bodi ya TGNP, Gemma Akilimali, amesema maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ni fursa muhimu ya kutathmini mafanikio yaliyopatikana katika harakati za kupigania haki za wanawake pamoja na kuweka mikakati madhubuti ya kuimarisha usawa wa kijinsia nchini.

Alisema maadhimisho ya mwaka huu yanaongozwa na kauli mbiu ya kitaifa isemayo “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi Kufikia Dira 2050,” ambayo inahamasisha jamii kuhakikisha wanawake wanapata fursa sawa katika nyanja zote za maendeleo.

Akilimali alisema kauli mbiu hiyo inakuja wakati muafaka ambapo Tanzania imeanza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 iliyozinduliwa Julai 2025, akisisitiza kuwa mafanikio ya dira hiyo yanategemea ushiriki sawa wa wanawake na wanaume katika maendeleo ya taifa.

“Mwaka huu Siku ya Wanawake Duniani si maadhimisho tu, bali ni wito wa kuchukua hatua madhubuti za kuondoa vikwazo vya kimfumo vinavyozuia upatikanaji wa haki sawa kwa wanawake na wasichana,” alisema Akilimali.

Alibainisha kuwa kumekuwa na hatua mbalimbali chanya nchini katika kuimarisha usawa wa kijinsia, ikiwemo kuimarishwa kwa Bajeti yenye Mtazamo wa Kijinsia (Gender Responsive Budgeting – GRB) pamoja na utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto (MTAKUWWA II).

Kwa upande wa uwakilishi wa wanawake katika vyombo vya maamuzi, alisema kumekuwa na maendeleo ambapo kwa sasa wanawake wanashikilia takribani asilimia 39.5 ya viti vya Bunge, ikilinganishwa na asilimia 37.4 baada ya uchaguzi wa mwaka 2020.

Aidha, alisema wanawake ni zaidi ya asilimia 51.3 ya Watanzania kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022, jambo linaloonesha umuhimu wa kuwapa nafasi sawa katika maendeleo ya taifa.

Akilimali pia alikumbusha kuwa Tanzania imeridhia mikataba mbalimbali ya kimataifa na kikanda inayolenga kulinda haki za wanawake, ikiwemo Tamko la Kimataifa la Haki za Binadamu (UDHR), Mkataba wa Kutokomeza Aina Zote za Ubaguzi Dhidi ya Wanawake (CEDAW), Mpango Kazi wa Beijing, pamoja na Itifaki ya Jinsia na Maendeleo ya SADC.

Alisisitiza kuwa kuwekeza kwa wanawake ni uwekezaji wa kimkakati unaochochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

“Niwakumbushe kanuni moja muhimu: Mwanamke akiendelea, jamii nzima inapiga hatua. Kuwekeza kwa mwanamke ni msingi wa kujenga jamii jumuishi na yenye maendeleo,” alisema.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP, Clara Kalanga, alisema dunia mwaka huu inaadhimisha miaka 115 tangu kuanza kwa Siku ya Wanawake Duniani mwaka 1911, huku Tanzania ikiwa katika kipindi muhimu cha kuanza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Alisema maadhimisho ya mwaka huu yanaambatana pia na kampeni ya kimataifa ya “ToaIliUpate (Give to Gain)”, inayohamasisha watu binafsi, mashirika na jamii kushiriki kikamilifu katika kuendeleza usawa wa kijinsia kupitia utoaji wa rasilimali, maarifa, ushauri na mafunzo.

Kalanga aliongeza kuwa TGNP kwa kushirikiana na wadau mbalimbali imeandaa shughuli kadhaa katika mwezi mzima wa Machi, ikiwemo maadhimisho katika ngazi ya jamii kupitia Vituo vya Taarifa na Maarifa katika zaidi ya kata 90 kutoka mikoa 13 nchini kuanzia tarehe 1 hadi 31 Machi 2026.

Aidha, alisema tarehe 17 Machi 2026 kutafanyika Kongamano la Vijana, huku kuanzia tarehe 25 hadi 27 Machi 2026 kukifanyika maadhimisho ya kimataifa yatakayowakutanisha wadau kutoka nchi za India, Haiti, Ethiopia, Bangladesh, Canada na Tanzania.
Mwenyekiti wa Bodi ya TGNP, Gemma Akilimali akizungumza wakati wa kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani 2026 kwa kufanya kongamano maalum lililofanyika tarehe 11 Machi 2026 katika Viwanja vya TGNP, Mabibo jijini Dar es Salaam.
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP, Clara Kalanga akizungumza na baadhi ya wanawake waliofika kwenye maadhimisho Siku ya Wanawake Duniani 2026 kwa kufanya kongamano maalum lililofanyika tarehe 11 Machi 2026 katika Viwanja vya TGNP, Mabibo jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya wanawake pamoja na wadau wa maendeleo wakifuatilia mada kwenye kongamano maalum lililoandaliwa na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) na kufanyika tarehe 11 Machi 2026 katika Viwanja vya TGNP, Mabibo jijini Dar es Salaam
Mratibu wa MTAKUWWA II kutoka Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu Alex Shayo  akizungumza kuhusu mpango wa serikali ya Tanzania unaolenga kupunguza na hatimaye kutokomeza vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake na watoto katika jamii kwa wanawake waliofikika kwenye kongamano la wanawake lililoandaliwa na TGNP
Mwanaharakati wa Masuala ya Bajeti kutoka TGNP Happiness Maruchu  akizungumzia kuhusu hatua za kimkakati za kuhakikisha uwepo wa Bajeti zenye mtazamo wa Kijinsia (Tulipotoka, Tulipo na Tunakoelekea kufikia Dira 2050) wakati wa kongamano lililoandaliwa na TGNP.
Picha za pamoja