HABARI

Theme images by kelvinjay. Powered by Blogger.

MATUKIO

MICHEZO

SIASA

ECOBANK TANZANIA YADHAMINI TUZO ZA BMT 2025, WAZIRI MKUU APONGEZA MCHANGO WA SEKTA BINAFSI KUKUZA MICHEZO



Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba ameongoza zoezi la utoaji wa Tuzo za Baraza la Michezo la Taifa (BMT) zilizotolewa kwa wanamichezo na timu zilizofanya vizuri mwaka 2025, katika hafla iliyolenga kutambua mchango na mafanikio ya wadau wa michezo nchini.

Akizungumza katika hafla hiyo ambapo alikuwa mgeni rasmi, Dkt. Nchemba alitoa pongezi na shukrani za dhati kwa Ecobank Tanzania kwa mchango wake mkubwa wa kudhamini hafla hiyo muhimu ya michezo nchini.

Dkt. Nchemba alisema ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi unaendelea kuwa chachu ya maendeleo ya michezo nchini, huku akiipongeza Ecobank Tanzania kwa kuonyesha dhamira ya kweli katika kuunga mkono vipaji vya wanamichezo wa Tanzania. Alibainisha kuwa udhamini huo umeongeza hadhi ya Tuzo hizo na kutoa motisha kwa wanamichezo kuendelea kufanya vizuri katika mashindano ya kitaifa na kimataifa.

Aidha, Waziri Mkuu alisema katika kipindi kifupi yameshuhudiwa mafanikio makubwa katika sekta ya michezo, yakiwamo kuanzishwa kwa Mfuko wa Maendeleo ya Michezo unaopata asilimia tano ya mapato ya michezo ya kubashiri, hatua ambayo imewezesha timu na wanamichezo kushiriki mashindano mengi zaidi kwa ubora wa hali ya juu. Alisisitiza kuwa mchango wa wadau kama Ecobank Tanzania unaendelea kusaidia juhudi za Serikali katika kuinua sekta ya michezo na kuibua vipaji vya vijana nchini.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Ecobank Tanzania, Dkt. Charles Asiedu alisema benki hiyo inajivunia kuunga mkono juhudi za Serikali katika kutambua na kuinua vipaji vya michezo mbalimbali hapa nchini kupitia Tuzo za Baraza la Michezo la Taifa (BMT) tukio linaloadhimisha ubora, kujituma na mafanikio makubwa ya mashujaa wa michezo wa Tanzania.

Dkt. Asiedu alisema kupitia Tuzo hizo maalumu, Ecobank imedhamini kipengele cha Tuzo ya Mwamuzi Bora wa Kiume wa Mwaka, kinacholenga kutambua na kuhamasisha vipaji vinavyochipukia katika sekta ya michezo nchini. Alieleza kuwa benki hiyo itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha vijana wenye vipaji wanapata motisha na mazingira bora ya kufikia mafanikio yao.

" Ecobank Group ni benki kubwa yenye mtandao mpana zaidi barani Afrika, ikiwa na uwepo katika nchi zaidi ya 33. Nchini Tanzania, Ecobank inatoa huduma mbalimbali za kibenki kwa wateja binafsi pamoja na wafanyabiashara wadogo, wa kati na wakubwa." Alisema Dkt. Asiedu

Benki hiyo imeendelea kuwakaribisha wananchi kutumia huduma zake kupitia matawi, mawakala pamoja na ATM zilizopo Dar es Salaam, Arusha na Mwanza ili kupata huduma bora na za kisasa za kibenki. Sambamba na hilo, Ecobank pia inatoa huduma za kibenki kiganjani kupitia Ecobank Mobile, ambapo wateja wanaweza kupata huduma mbalimbali ikiwamo kufungua akaunti, kulipia bili, kupata huduma ya salary advance kwa waajiriwa pamoja na mikopo kwa watumishi wa umma.

Kwa pamoja, Serikali na wadau wa sekta binafsi wanaendelea kuibua vipaji, kuhamasisha jamii na kuwezesha kizazi kijacho kupitia michezo.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba akizungumza na viongozi pamoja na wageni  mbalimbali wakati wa utoaji wa Tuzo za BMT 2025 zililizofanyika katika ukumbi wa The Super Dome, Masaki jijini Dar es Salaam
Mkurugenzi Mtendaji wa Ecobank Tanzania, Dkt. Charles Asiedu akimtangaza mshindi Tuzo ya Mwamuzi Bora wa Kiume wa Mwaka katika Tuzo za BMT 2025 zilizotolewa katika ukumbi wa The Super Dome, Masaki jijini Dar es Salaam
Mkurugenzi Mtendaji wa Ecobank Tanzania, Dkt. Charles Asiedu(kulia) akimkabidhi Tuzo ya Mwamuzi Bora wa Kiume wa Mwaka, Shabani Mahobonya (kushoto) kwenye Tuzo za BMT 2025 zilizotolewa katika ukumbi wa The Super Dome, Masaki jijini Dar es Salaam
Wafanyakazi wa Ecobank Tanzania wakiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji, Dkt. Charles Asiedu(wa kwanza kushoto) wakiwa kwenye hafla ya utoaji wa Tuzo za BMT 2025.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba pamoja na viongozi wengine wakiwa kwenye picha ya pamoja na wadhamini wa Tuzo za BMT 2025.
Wafanyakazi wa Ecobank Tanzania wakiwa kwenye picha ya pamoja katika Tuzo za BMT 2025


WATUMISHI WA NBAA WASHIRIKI MAADHIMISHO YA MEI MOSI 2026 DAR ES SALAAM


Watumishi wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) wameshiriki katika maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi) mwaka 2026, yaliyofanyika kimkoa katika Wilaya ya Ilala, katika Viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam.

Mgeni rasmi katika maadhimisho hayo alikuwa Mhe. Albert Chalamila, Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam, ambaye alisisitiza umuhimu wa wafanyakazi kutambua nafasi yao katika kujenga taswira ya serikali. Alieleza kuwa mfanyakazi mmoja anaweza kuchangia serikali kupendwa au kuchukiwa, hivyo aliwahimiza wafanyakazi wote kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa uaminifu, weledi na kujituma, akibainisha kuwa serikali inawajali na kuthamini mchango wao.

Maadhimisho hayo ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi) yameambatana na kaulimbiu isemayo: “Kazi zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050.”

Ushiriki wa watumishi wa NBAA katika maadhimisho hayo unaonesha dhamira ya taasisi hiyo kuendelea kuunga mkono juhudi za serikali katika kukuza utamaduni wa kazi, uwajibikaji na maendeleo endelevu nchini.
Baadhi ya Watumishi wa Bodi ya Taifa ya wahasibu na wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) wakipita mbele ya Jukwaa kuu huku wakiwa na bango lenye ujumbe kuhusiana Wafanyakazi wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani yaliyofanyika katika Viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya Watumishi wa Bodi ya Taifa ya wahasibu na wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) wakiwa kwenye picha ya pamoja wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani yaliyofanyika katika Viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam.

BAOBAB WAKUTANA NA NBAA, WAPATIWA ELIMU YA UHASIBU


Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) imeendelea kuimarisha juhudi zake za kutoa elimu kwa wanafunzi mbalimbali wa Sekondari na Elimu ya Juu nchini, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kukuza Taaluma ya Uhasibu na kuongeza uelewa kuhusu majukumu ya Bodi hiyo.

Katika mwendelezo wa juhudi hizo, wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Baobab wametembelea NBAA na kupatiwa mafunzo maalum yaliyolenga kuwajengea uelewa mpana kuhusu shughuli za Bodi pamoja na fursa zilizopo katika Taaluma ya Uhasibu.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mkurugenzi Mtendaji wa NBAA, CPA Prof. Siasa I. Mzenzi , aliipongeza shule hiyo kwa jitihada za kuwawezesha wanafunzi wake kupata elimu ya vitendo nje ya darasa, hususan wale wanaosoma masomo ya biashara na Uhasibu.


Aidha, alieleza kuwa NBAA iko wazi kwa wanafunzi wanaosomea masomo ya uhasibu, na aliwasisitiza wasibadilishe taaluma kwa kuwa tayari wana msingi mzuri wa uhasibu. Pia alielezea kuwa hata wanafunzi wa michepuo wa masomo mengine ambao hawajasomea Uhasibu wanaweza kujiunga na mitihani ya Bodi hiyo kuanzia ngazi ya awali na hatimaye kufikia sifa za kuwa wahasibu kitaaluma.

CPA Prof. Siasa I. Mzenzi aliwasisitiza wanafunzi hao kufanya vizuri katika masomo yao ili kufikia malengo waliyojiwekea, alieleza kwamba Taaluma ya Uhasibu ina nafasi kubwa katika Taasisi mbalimbali kutokana na uhaba wa Wahasibu nchini.

Pia aliongeza kwa kuanzia ngazi za awali za masomo kunawasaidia wanafunzi kujengwa kitaaluma na kuwa wahasibu bora wa baadaye, huku akisisitiza umuhimu wa uadilifu, uaminifu na kufanya kazi kwa bidii bila kusimamiwa ili kuendeleza na kulinda hadhi ya Taaluma hiyo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano wa NBAA, Magreth Kageya, alisema ziara hiyo imekuwa na manufaa makubwa kwa wanafunzi hao, kwani imewapa fursa ya kupata taarifa sahihi na muhimu kuhusu majukumu ya Bodi pamoja na mwelekeo wa Taaluma ya Uhasibu.

Naye mwalimu wa Shule ya Sekondari ya Baobab, Stephen Mahundi, aliishukuru NBAA kwa kuwapatia wanafunzi elimu ya Uhasibu, akisema itawasaidia katika masomo yao ya sasa na kuwaandaa kufikia malengo yao.

Ziara hiyo ni miongoni mwa juhudi za NBAA za kuendelea kujenga kizazi cha wataalamu wa Uhasibu wenye uelewa mpana na uwezo wa kukidhi mahitaji ya soko la ajira la ndani na kimataifa na kukuza uchumi wa nchi.

Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA Prof. Siasa I. Mzenzi akizungumza na wanafunzi wa Kidato cha Tano wanaosoma masomo ya Biashara katika Shule ya Sekondari ya Baobab waliotembelea na kupata mafunzo katika ofisi za Bodi ya NBAA zilizopo jijini Dar es Salaam.
CPA. Bertha Kipangula, Mkuu wa Sehemu ya Usajili wa Wanachama, Uzingatiaji wa Sheria na Maendeleo ya Kitaaluma akitoa elimu kuhusu kazi mbalimbali zinazofanywa na Kurugenzi yake na faida ya CPA na kuwa mwanachama wa Bodi.
Magreth Kageya, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano ya Umma wa NBAA akitoa mada kuhusu kazi mbalimbali zinazofanywa na NBAA "NBAA Overview" kwa wanafunzi wa Kidato cha Tano wanaosoma masomo ya Biashara katika Shule ya Sekondari ya Baobab waliotembelea na kupata mafunzo katika ofisi za Bodi ya NBAA.
CPA George Lazaro, Mkaguzi wa ndani wa NBAA akitoa elimu kuhusu Ukaguzi na majukumu mbalimbali ya Mkaguzi kwa wanafunzi wa Kidato cha tano kutoka Shule ya Sekondari ya Baobab waliotembelea na kupata mafunzo katika ofisi za Bodi ya NBAA.
Mwalimu wa Shule ya Sekondari ya Baobab Stephen Mahundi akitoa neno la shukrani kwa uongozi wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi Hesabu Tanzania (NBAA) walipotembelea ofisi za Bodi ya NBAA.
Baadhi ya wafanyakazi wa NBAA na wanafunzi wa Kidato cha Tano wanaosoma masomo ya Biashara katika Shule ya Sekondari ya Baobab wakifuatilia mada kwa wataalam kutoka Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu (NBAA) walipotembelea ofisi za Bodi hiyo zilizopo jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa NBAA, CPA Prof. Siasa I. Mzenzi (waliokaa, katikati) kwenye picha ya pamoja na baadhi ya Wafanyakazi wa Bodi hiyo, walimu na wanafunzi wa Kidato cha Tano wanaosoma masomo ya Biashara kutoka Shule ya Sekondari ya Baobab walipotembelea ofisi za NBAA kwa ajili ya kupata elimu.

Dkt. Jabiri Akabidhiwa Ofisi Rasmi TCAA



Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Dkt. Jabiri K. Bakari amekabidhiwa rasmi ofisi na aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu Bw. Salim R. Msangi katika Makao Makuu ya TCAA, Banana, Ukonga jijini Dar es Salaam.

Makabidhiano hayo yamefanyika Aprili 27, 2026 na kuhudhuriwa na Menejimenti ya TCAA.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Dkt. Jabiri K. Bakari (kulia) akikabidhiwa rasmi ofisi na aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu Bw. Salim R. Msangi (kushoto) katika Makao Makuu ya TCAA, Banana, Ukonga jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Dkt. Jabiri K. Bakari (kulia) pamoja na aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu Bw. Salim R. Msangi (kushoto)  wakisaini makabidhiano ya ofisi yaliyofanyika katika Makao Makuu ya TCAA, Banana, Ukonga jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Dkt. Jabiri K. Bakari (kulia) akifanya mazungumzo na aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu Bw. Salim R. Msangi (kushoto) katika Makao Makuu ya TCAA, Banana, Ukonga jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Dkt. Jabiri K. Bakari akizungumza na Menejimenti ya  TCAA mara baada ya kukabidhiwa ofisi na aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu Bw. Salim R. Msangi katika Makao Makuu ya TCAA, Banana, Ukonga jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Dkt. Jabiri K. Bakari pamoja na aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu Bw. Salim R. Msangi wakiwa kwenye picha ya pamoja na Menejimenti  ya TCAA mara baada ya kumalizika kwa zoezi la makabadhiano ya ofisi yaliyofanyika katika Makao Makuu ya TCAA, Banana, Ukonga jijini Dar es Salaam.

TCAA Yatoa Msaada kwa Kituo cha Tupendane Dodoma





Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania(TCAA), kama sehemu ya kurudisha kwa jamii, imetoa msaada katika kituo cha kulelea watoto cha Tupendane kilichopo jijini Dodoma huku ikitoa wito kwa wadau mbalimbali kuendelea kuwa na moyo wa kusaidia jamii, hususan vituo vya kulelea watoto.

Akizungumza wakati wa kupokea msaada huo, Subira Yasini, mlezi wa Kituo cha Tupendane, ameishukuru TCAA kwa kuguswa na mahitaji ya kituo hicho na kueleza kuwa msaada huo utasaidia kuboresha huduma na mazingira ya malezi kwa watoto waliopo kituoni. Alisema hatua hiyo inaonesha mshikamano na kujali ustawi wa makundi yenye uhitaji maalum katika jamii.

Awali, Bi. Subira alieleza changamoto mbalimbali zinazowakabili, ikiwa ni pamoja na ukosefu wa eneo la kudumu la makazi ya watoto hao, kwani kwa sasa wanatumia eneo la mtu aliyewapatia hifadhi ya muda.

Kituo hicho cha Tupendane kina jumla ya watoto 35, ambapo 22 kati yao wanasoma katika ngazi mbalimbali kuanzia elimu ya msingi hadi sekondari.

Kwa upande wake, Ally Changwila, Meneja Uhusiano wa Mamlaka hiyo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TCAA Bw. Salim Msangi, alisema kuwa Mamlaka hiyo inaendelea kuimarisha mahusiano chanya na jamii kwa kushiriki katika shughuli za maendeleo ya kijamii. Ameeleza kuwa msaada uliotolewa katika kituo hicho unaakisi dhamira ya TCAA ya kuchangia ustawi wa jamii sambamba na majukumu yake ya msingi katika usimamizi wa usafiri wa anga.

Aidha, aliongeza kuwa Mkurugenzi Mkuu wa TCAA ameelekeza kuwa, kutokana na umuhimu wa kurejesha kwa jamii na kusaidia wenye uhitaji, kila robo ya mwaka wa fedha angalau TCAA itoe msaada katika mojawapo ya vituo vyake vya kazi nchini. TCAA ina vituo 16 nchi nzima vinavyotoa huduma ya uongozaji ndege.

Kwa upande wake, Aswile Kamendu, Meneja wa TCAA Kituo cha Dodoma, alisema kuwa TCAA itaendelea kushirikiana na Taasisi na vituo mbalimbali vya kijamii katika mkoa wa Dodoma na mikoa mingine ili kusaidia juhudi za Serikali na wadau wengine katika kuboresha maisha ya wananchi.

Msaada uliotolewa katika kituo hicho cha Tupendane ni pamoja na vyakula vya aina mbalimbali, sabuni, mafuta ya kupikia pamoja na vifaa vya shule ikiwemo mabegi na madaftari.
Meneja Uhusiano wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania(TCAA) Ally Changwila (wa pili kulia) aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa TCAA Bw. Salim Msangi pamoja na  Meneja wa TCAA Kituo cha Dodoma Aswile Kamendu wakiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya walezi na watoto wanaolelewa katika  kituo cha Tupendane kilichopo jijini Dodoma
Meneja Uhusiano wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania(TCAA) Ally Changwila akitoa salamu za Mkurugenzi Mkuu wa TCAA Bw. Salim Msangi wakati wa kutoa msaada katika kituo cha kulelea watoto cha Tupendane kilichopo jijini Dodoma
Meneja wa TCAA Kituo cha Dodoma Aswile Kamendu akizungumza kuhusu namna watakavyoendelea kushirikiana na Taasisi na vituo mbalimbali vya kijamii kwa kutoa misaada mbalimbali katika mkoa wa Dodoma