HABARI

Theme images by kelvinjay. Powered by Blogger.

MATUKIO

MICHEZO

SIASA

NBAA YAENDESHA WARSHA YA IPSAS MOROGORO



Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), Septemba 8, 2026, imeendesha Warsha ya Mafunzo kuhusu Uandaaji wa Hesabu kwa kuzingatia Viwango vya Kimataifa vya Uhasibu kwa Sekta ya Umma (IPSAS), mkoani Morogoro.

‎Akizungumza wakati wa ufunguzi wa warsha hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa NBAA, CPA Prof. Siasa I. Mzenzi, amesema Tanzania imepiga hatua kubwa katika utekelezaji wa IPSAS, hatua ambayo imeiwezesha nchi kujenga uwezo na kupata uzoefu unaoweza kuwa mfano kwa mataifa mengine.

CPA ‎Prof. Siasa amesema Tanzania kwa sasa imevuka hatua ya msingi ya kujenga uwezo katika eneo la IPSAS, tofauti na baadhi ya nchi ambazo bado zinaendelea kutafuta namna ya kuimarisha uwezo wa wataalamu wao katika utekelezaji wa viwango hivyo. Amesema mafanikio hayo yameifanya Tanzania kuwa na nafasi ya kushirikisha uzoefu wake na nchi nyingine.

‎“Tumefanikiwa sana kwenye IPSAS, mkazo huo kwa sasa tunauelekeza pia kwenye Sustainability Reporting na tayari tumeshatoa Technical Pronouncement No. 1 ya mwaka 2024 ambayo inazitaka taasisi kuanza kutoa taarifa za Sustainability.

CPA ‎Prof. Siasa amesisitiza umuhimu wa Taasisi za Umma kutumia mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa IPSAS kama msingi wa kuimarisha utoaji wa taarifa za uendelevu, akieleza kuwa maeneo hayo yanapaswa kwenda sambamba katika kukuza uwazi, uwajibikaji na uendelevu wa taasisi za umma.

‎Katika hatua nyingine, amewahamasisha washiriki wa warsha hiyo kuweka kipaumbele katika uandaaji na uwasilishaji bora wa vitabu vya hesabu kwa ajili ya "Best Presented Financial Statements Awards", akieleza kuwa idadi ya washindi itaongezwa kutoka watatu hadi watano.

‎Warsha hii ya IPSAS inalenga kuwawezesha washiriki kuongeza uelewa na ujuzi kuhusu matumizi sahihi ya IPSAS katika uandaaji wa taarifa za fedha za sekta ya umma, pamoja na kuimarisha weledi wa wataalamu katika eneo la Uhasibu na Ukaguzi wa hesabu.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) CPA Prof. Siasa I. Mzenzi akizungumza wakati wa ufunguzi wa warsha ya Mafunzo kuhusu Uandaaji wa Hesabu kwa kuzingatia Viwango vya Kimataifa vya Uhasibu kwa Sekta ya Umma (IPSAS), mkoani Morogoro.
Mkurugenzi wa Huduma za Viwango vya Kiuhasibu, Utafiti na Huduma za Ufundi wa NBAA, Angyelile Tende akizungumza kwenye warsha ya Mafunzo kuhusu Uandaaji wa Hesabu kwa kuzingatia Viwango vya Kimataifa vya Uhasibu kwa Sekta ya Umma (IPSAS), mkoani Morogoro.
Baadhi ya washiriki pamoja na watumishi wa NBAA wakifuatlia ufunguzi wa warsha ya Mafunzo kuhusu Uandaaji wa Hesabu kwa kuzingatia Viwango vya Kimataifa vya Uhasibu kwa Sekta ya Umma (IPSAS), mkoani Morogoro.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) CPA Prof. Siasa I. Mzenzi  katikati waliokaa) akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya washiriki pamoja na watumishi wa NBAA kwenye warsha ya Mafunzo kuhusu Uandaaji wa Hesabu kwa kuzingatia Viwango vya Kimataifa vya Uhasibu kwa Sekta ya Umma (IPSAS)

TANZANIA BLOGGERS NETWORK (TBN) NA PSSSF WAJENGA USHIRIKIANO MKAKATI WA KUONGEZA ELIMU YA HIFADHI YA JAMII


Dar es Salaam
Katika kile kinachoelezwa kuwa ni hatua madhubuti ya kupanua wigo wa utoaji wa elimu kwa umma, timu ya maofisa wa juu kutoka Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) imefanya ziara rasmi katika Makao Makuu ya Tanzania Bloggers Network (TBN) yaliyopo Dar es Salaam, Kijitonyama na kufanya mazungumzo ya kimkakati na viongozi wakuu wa mtandao huo.

Mazungumzo hayo yaliyolenga kujenga ushirikiano wa manufaa ya pande zote mbili yamejikita katika kuimarisha uhusiano wa kisekta kwenye masuala ya habari, uelimishaji wa umma, na usambazaji wa maarifa sahihi kuhusu mifumo ya pensheni na uwekezaji nchini.

Akizungumza wakati wa mkutano huo, Mwenyekiti wa TBN, Beda Msimbe, alieleza utayari wa mtandao huo kusimama kidete kama chombo cha kutoa elimu na kusambaza maarifa sahihi kwa umma na katika nyanja za kidijitali.

Hata hivyo, alisisitiza kuwa ili kufikia malengo hayo kwa ufanisi zaidi, ni muhimu wanachama wa TBN wenyewe wakapatiwa kwanza mafunzo ya kina na ya kutosha kuhusu shughuli na uendeshaji wa mfuko huo.

Ushirikiano huo unatazamiwa kufungua ukurasa mpya katika matumizi ya vyombo vya habari vya mtandaoni kufikisha elimu ya hifadhi ya jamii kwa wananchi wengi zaidi nchini.

Kwa upande wake, Mkuu wa msafara huo kutoka PSSSF, Abdul Njaidi, alieleza kuwa ziara hiyo inalenga kujenga uhusiano wa karibu na wadau wa sekta ya habari pamoja na kutoa elimu kwa jamii.

Aliwahakikishia viongozi wa TBN kuwa maombi na hoja zote zilizowasilishwa zitafanyiwa kazi, akisisitiza kuwa ushirikiano huo mpya unalenga kuhakikisha wananchi wanapata uelewa mpana na sahihi kuhusu masuala ya pensheni na uwekezaji unaofanywa na PSSSF.

Naye Mdhamini wa TBN, Issa Michuzi, ambaye alishiriki katika mkutano huo, alieleza kuwa mtandao huo wenye historia kubwa unajivunia weledi na ufanisi mkubwa.

Alisema TBN ipo kwa ajili ya kuhakikisha Tanzania inasomeka vyema katika medani za kidijitali ili kuchochea na kutanua zaidi gurudumu la maendeleo ya taifa.

Katibu wa TBN, Rahel Pallangyo, aliongeza kuwa mtandao huo upo tayari kutoa waandishi wake mahiri na kutumia majukwaa yake mbalimbali kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi na za kuaminika zitakazowezesha kufanikiwa kwa utekelezaji wa majukumu ya wananchi na wadau wa maendeleo.

Katika mkutano huo, ujumbe wa PSSSF ulioongozwa na Abdul Njaidi, ulijumuisha maofisa wengine akiwemo Regina Kumba, Grayson Mgunda, na Doreen Lyimo.

Kwa upande wa TBN, viongozi waliohudhuria ni pamoja na Mwenyekiti Beda Msimbe, Katibu Rahel Pallangyo, mtaalamu wa mawasiliano, Cathbert Kajuna na Mdhamini wa TBN, Issa Michuzi.

NAIBU KATIBU MKUU WIZARA YA UCHUKUZI ATEMBELEA TCAA



Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Mhe. Abdallah Mitawi, ametembelea Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) kwa lengo la kufahamu kwa kina majukumu ya Mamlaka pamoja na utekelezaji wa shughuli mbalimbali zinazolenga kusimamia na kuendeleza sekta ya usafiri wa anga nchini.

Katika ziara hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa TCAA, Dkt. Jabiri Bakari, alimueleza Naibu Katibu Mkuu kuhusu majukumu na shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na Mamlaka, ikiwemo usimamizi na udhibiti wa shughuli za usafiri wa anga, usalama na ulinzi wa anga, pamoja na utoaji wa huduma kwa watumiaji wa sekta hiyo.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mhe. Mitawi ameipongeza TCAA kwa juhudi inazofanya katika kuhakikisha usalama na ufanisi wa shughuli za usafiri wa anga nchini, akisisitiza umuhimu wa kuendelea kuimarisha usalama wa Usafiri wa anga kwa kuwa sekta hiyo ni kichocheo muhimu cha ukuaji wa uchumi na maendeleo ya Taifa.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa Tanzania kutumia kikamilifu fursa zilizopo katika sekta ya usafiri wa anga, huku akihimiza kuendelea kuboresha huduma na miundombinu, kuimarisha ushirikiano na wadau pamoja na kutumia ubunifu na teknolojia za kisasa ili kuongeza mchango wa sekta hiyo katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Katika ziara hiyo, Mhe. Mitawi pia alitembelea maeneo mbalimbali ya TCAA na kujionea shughuli zinazotekelezwa na Mamlaka, ikiwemo Kituo cha TCAA cha Uongozaji Ndege katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA).

Imeelezwa ziara hiyo ni sehemu ya jitihada za Wizara ya Uchukuzi za kufuatilia utekelezaji wa majukumu na miradi ya kimkakati katika sekta ya usafiri wa anga, kwa lengo la kuhakikisha sekta hiyo inaendelea kukua, kuwa salama na kutoa huduma zenye ufanisi kwa wananchi na wadau mbalimbali.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Bw. Abdallah Mitawi akipokea zawadi kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Dkt. Jabiri K. Bakari alipotembea katika ofisi za Mamlaka zilizopo eneo la Banana, jijini Dar es Salaam.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Bw. Abdallah Mitawi akizungumza na baadhi ya watumishi wa TCAA wakiongozwa na Mkurugenzi Mkuu wa TCAA, Dkt. Jabiri K. Bakari alipotembea ofisi za Mamlaka hiyo eneo la Banana, jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Dkt. Jabiri K. Bakari akitoa taarifa kuhusu kazi zinazofanywa na Mamlaka hiyo kwa Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Bw. Abdallah Mitawi alipotembea katika ofisi za Mamlaka zilizopo eneo la Banana, jijini Dar es Salaam.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Bw. Abdallah Mitawi akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya Menejimenti ya TCAA ikiongozwa na Mkurugenzi Mkuu TCAA, Dkt. Jabiri K. Bakari pamoja na baadhi ya watumishi wa wizara ya Uchukuzi.

BODI YA TAFICO YARIDHISHWA KUKAMILIKA KWA BANDARI YA UVUVI KILWA MASOKO




Bodi ya Wakurugenzi ya Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO), imefanya ziara ya ukaguzi katika mradi wa Bandari ya Uvuvi Kilwa Masoko, kwa lengo la kujionea hatua ya utekelezaji wa mradi, kukagua miundombinu na maandalizi yaliyofanyika kuelekea kuanza kwa matumizi ya bandari hiyo, pamoja na kutathmini fursa zitakazotokana na uwekezaji huo katika shughuli za uvuvi na uchumi wa buluu.

Ziara hiyo imefanyika leo tarehe 20 Agosti 2026, ikiongozwa na Mwenyekiti wa Bodi hiyo Prof. Yunus D. Mgaya, ambapo Bodi hiyo imepata fursa ya kukagua maeneo mbalimbali ya bandari na kupata maelezo kuhusu hatua iliyofikiwa katika maandalizi ya kuanza kwa shughuli zake.

Akizungumza baada ya ziara hiyo, Prof. Mgaya, amesema ameridhishwa na maendeleo ya mradi huo, akieleza kuwa kukamilika na kuanza kufanya kazi kwa Bandari ya Uvuvi Kilwa Masoko kutakuwa hatua muhimu katika kuimarisha sekta ya uvuvi nchini.

"Bandari hii ina nafasi kubwa katika kuongeza ufanisi wa shughuli za uvuvi, kuongeza thamani ya mazao ya uvuvi, pamoja na kutoa fursa za ajira na biashara. Nawahimize wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi kutumia fursa zilizopo katika Bandari ya Uvuvi Kilwa Masoko kwa kuwekeza katika shughuli mbalimbali zinazohusiana na sekta ya uvuvi," aliongeza Prof. Mgaya

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa TAFICO, Dkt. Suleiman Kiula, ndc , amesema Shirika hilo linaendelea na mchakato wa kushirikisha sekta binafsi pamoja na wadau mbalimbali kuhakikisha bandari hiyo inaendeshwa kwa ufanisi, kwa kutoa huduma wezeshi kwa viwango bora na nafuu ili kuvutia Meli nyingi kutumia bandari hiyo ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Dkt. Kiula amesema TAFICO inaendelea kutekeleza mikakati ya kushiriki kikamilifu katika kuendeleza shughuli za uvuvi wa kisasa na ukuzaji viumbe maji, ikiwemo uwekezaji katika Meli za uvuvi wa bahari kuu, uanzishaji wa mashamba ya kufuga samaki, miundombinu wezeshi, pamoja na kuongeza thamani ya mazao ya uvuvi.

"Kuanza kwa shughuli za Bandari ya Uvuvi Kilwa Masoko kutafungua fursa mbalimbali kwa wavuvi, wafanyabiashara na wawekezaji, huku kukiwa na matarajio ya kuongeza ajira na kuchochea shughuli za kiuchumi katika Wilaya ya Kilwa na maeneo mengine nchini," alieleza Dkt. Kiula.

Bandari ya Uvuvi Kilwa Masoko ni mradi wa kimkakati unaolenga kuimarisha shughuli za uvuvi nchini. Miundombinu ya bandari hiyo inajumuisha gati lenye urefu wa mita 315 la kuhudumia meli za uvuvi zaidi ya kumi kwa wakati mmoja, eneo la kuhifadhi samaki, mtambo wa kizalisha barafu na eneo la matengenezo ya meli, hatua inayolenga kuongeza ufanisi katika shughuli za uvuvi na mnyororo wa thamani wa mazao ya uvuvi.










NBAA YAIMARISHA UWEZO WA WAKUFUNZI WA VITUO VYA KUFUNDISHIA WATAHINIWA

NBAA YAIMARISHA UWEZO WA WAKUFUNZI WA VITUO VYA KUFUNDISHIA WATAHINIWA

Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) imeendesha warsha kwa njia ya mtandao sambamba na mafunzo ya ana kwa ana kwa wakufunzi wa vituo vya kufundishia wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi, ikiwa na lengo la kuwaongezea ujuzi na kuimarisha mbinu za ufundishaji.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Elimu ya Taaluma na Mafunzo wa NBAA, Peter Lyimo, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mtendaji wa NBAA, CPA Prof. Siasa Mzenzi, amesema mafunzo hayo yameandaliwa kwa ajili ya kuwakumbusha wakufunzi majukumu yao pamoja na kuhakikisha wanaendana na mitaala na mahitaji ya Bodi.

Amesema NBAA imeona mafanikio makubwa katika vituo vya kufundishia, ikiwemo kuongezeka kwa idadi ya wanafunzi wanaofanya mitihani ya Bodi mwaka hadi mwaka.

“Tumeona mafanikio makubwa kwenye vituo vya kufundishia wanafunzi, ambapo idadi ya wanafunzi wanaofanya mitihani ya Bodi imeendelea kuongezeka mwaka hadi mwaka. Mwaka jana wanafunzi waliofanya mitihani walikuwa zaidi ya 8,000 na hivi sasa tunaelekea kufikia 10,000,” amesema Lyimo.

Amesema lengo la NBAA ni kuongeza kiwango cha ufaulu katika mitihani mbalimbali ya Bodi na kuhakikisha wanafunzi wanapata uelewa mpana wa masuala ya Uhasibu na Ukaguzi wa hesabu, ili wanapohitimu wawe wataalamu wenye weledi na uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa kufanya jitihada zaidi katika kuboresha huduma zinazotolewa na vituo vya kufundishia, ili wanafunzi waone thamani ya kwenda kusoma katika vituo hivyo na kuwepo kwa utofauti wa kitaaluma kati ya mwanafunzi anayepitia mafunzo katika vituo hivyo na yule anayejisomea bila kupata mafunzo hayo.

Amesema NBAA itaendelea kushirikiana na vituo vya kufundishia pamoja na wakufunzi kuhakikisha wanafunzi wanapata maandalizi bora kuelekea mitihani ya Bodi na hatimaye kujenga wataalamu wenye uwezo wa kuchangia maendeleo ya Taaluma ya Uhasibu na Ukaguzi wa hesabu nchini.
Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Elimu ya Taaluma na Mafunzo wa NBAA, Peter Lyimo akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo kwa wakufunzi waliofika katika warsha ya ana kwa ana na kwa njia ya mtandao kwa Wakufunzi wa Vituo vya Kufundishia wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi.
Mkurugenzi wa Huduma za Shirika kutoka NBAA CPA Kulwa Malendeja akizungumza na wakufunzi waliofika katika warsha ya ana kwa ana na kwa njia ya mtandao kwa Wakufunzi wa Vituo vya Kufundishia wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi.
Mkuu wa Sehemu ya Elimu na Mafunzo NBAA, Sawa Ngendabanka akiwakaribisha wakufunzi wa vituo vya Kufundishia watahiniwa wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi ambao walikuwa wakifuatilia Warsha hiyo na kwa ana na kwa njia ya mtandao.
Mdhibiti Ubora Mwandamizi kutoka NACTVET Dkt. Bonaventure Ackles akitoa mada kuhusu "ufundishaji na uwezeshaji wenye ufanisi kwa wanafunzi" mada iliyotolewa kwa wakufunzi waliofika katika warsha ya ana kwa ana na kwa njia ya mtandao kwa Wakufunzi wa Vituo vya Kufundishia wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi.
Mkufunzi CPA Simon Mangesho akitoa mada kuhusu mbinu bora za kufundisha na kufundisha kikamilifu maudhui ya mitaala ya kitaaluma kwa kutumia mfano wa B2 na C1 kwa wakufunzi waliofika katika warsha ya ana kwa ana na kwa njia ya mtandao.
Mkufunzi CPA Rashid Mganwa akitoa elimu kuhusu maboresho ya B4, C4 pamoja na IFRS 18 kwa wakufunzi waliofika katika warsha ya ana kwa ana na kwa njia ya mtandao kwa Wakufunzi wa Vituo vya Kufundishia wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi.
Baadhi ya Wafanyakazi wa NBAA na Wakufunzi wa Vituo vya Kufundishia Wanafunzi 'Tuition Providers' wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi wakifuatilia mada pamoja na wale wanaofuatilia ana kwa ana na kwa njia ya mtandao kwa Wakufunzi wa Vituo vya Kufundishia wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi.
Picha ya pamoja ya wafanyakazi wa NBAA na wakufunzi wa vituo vya kufundishia watahiniwa wa Bodi 'Tuition Providers'

NBAA YAWAPIGA MSASA WANAOTARAJIA KUFANYA MITIHANI YA BODI





Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA Prof. Siasa Mzenzi, amefungua warsha ya siku moja inayowakutanisha wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi, inayofanyika ana kwa ana na kwa njia ya mtandao.

Warsha hiyo imelenga kuwajengea wanafunzi uelewa na maandalizi bora kuelekea mitihani ya Bodi, kwa kuwapatia mwongozo kuhusu mbinu za kujisomea, maandalizi ya mitihani pamoja na kuzingatia maadili ya taaluma ya Uhasibu.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa warsha hiyo, CPA Prof. Mzenzi amesema NBAA inawathamini wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi na haitarajii kuona matokeo yasiyoridhisha. Amesema kutokana na hilo, NBAA imeanzisha mpango maalumu wa kuwaandalia wanafunzi warsha na siku maalumu za mafunzo, zitakazowasaidia kupata mbinu na uelewa wa masomo mbalimbali ili kufanya vizuri katika mitihani.

Amesema warsha hiyo pia inalenga kuwafahamisha wanafunzi kile ambacho NBAA inatarajia kutoka kwao, ikiwemo kuwa na maandalizi mazuri, weledi na kuzingatia maadili ya taaluma.

Amewataka wanafunzi kutumia fursa hiyo kuongeza uelewa, kuuliza maswali na kujifunza mbinu mbalimbali zitakazowawezesha kujiandaa kikamilifu na kufanya vizuri katika mitihani ya Bodi.
Aidha, amesema NBAA itaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wanafunzi na wataalamu wanaotarajia kujiendeleza katika taaluma ya Uhasibu na Ukaguzi wa hesabu nchini.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA Prof. Siasa Mzenzi akizungumza wakati ufunguzi wa warsha ya ana kwa ana na kwa njia ya mtandao kwa wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi.
Mkurugenzi wa Huduma za Shirika kutoka NBAA CPA Kulwa Malendeja akizungumza na wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi wakati wa warsha ya ana kwa ana na kwa njia ya mtandao kwa wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi.
Mkufunzi CPA Rashid Mganwa akitoa elimu kuhusu namna ya kujiandaa na kufanya masomo ya B4, C4 pamoja na maboresho ya IFRS 10 kwa wanafunzi wanaotegemea kufanya mitihani ya Bodi waliokuwa wanafuatilia ana kwa ana na kwa njia ya mtandao.
Mkufunzi CPA Edison Leonce akitoa elimu kuhusu namna ya kujiandaa na kufanya masomo ya B2 na C1 kwa wanafunzi wanaotegemea kufanya mitihani ya Bodi waliokuwa wanafuatilia ana kwa ana na kwa njia ya mtandao.
Mkufunzi kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, CPA Dkt. Emmanuel Christopher akitoa elimu kuhusu namna ya kujiandaa na kufanya masomo ya B1 na C3 kwa wanafunzi wanaotegemea kufanya mitihani ya Bodi waliokuwa wanafuatilia ana kwa ana na kwa njia ya mtandao.
Baadhi ya wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi wakifuatilia mada pamoja na kuuliza maswai kwa wakufunzi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA Prof. Siasa Mzenzi akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya wafanyakazi wa NBAA pamoja na Wakufunzi wa wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA Prof. Siasa Mzenzi akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya wafanyakazi wa NBAA pamoja na wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi.