HABARI

Theme images by kelvinjay. Powered by Blogger.

MATUKIO

MICHEZO

SIASA

BODI YA TAFICO YARIDHISHWA KUKAMILIKA KWA BANDARI YA UVUVI KILWA MASOKO




Bodi ya Wakurugenzi ya Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO), imefanya ziara ya ukaguzi katika mradi wa Bandari ya Uvuvi Kilwa Masoko, kwa lengo la kujionea hatua ya utekelezaji wa mradi, kukagua miundombinu na maandalizi yaliyofanyika kuelekea kuanza kwa matumizi ya bandari hiyo, pamoja na kutathmini fursa zitakazotokana na uwekezaji huo katika shughuli za uvuvi na uchumi wa buluu.

Ziara hiyo imefanyika leo tarehe 20 Agosti 2026, ikiongozwa na Mwenyekiti wa Bodi hiyo Prof. Yunus D. Mgaya, ambapo Bodi hiyo imepata fursa ya kukagua maeneo mbalimbali ya bandari na kupata maelezo kuhusu hatua iliyofikiwa katika maandalizi ya kuanza kwa shughuli zake.

Akizungumza baada ya ziara hiyo, Prof. Mgaya, amesema ameridhishwa na maendeleo ya mradi huo, akieleza kuwa kukamilika na kuanza kufanya kazi kwa Bandari ya Uvuvi Kilwa Masoko kutakuwa hatua muhimu katika kuimarisha sekta ya uvuvi nchini.

"Bandari hii ina nafasi kubwa katika kuongeza ufanisi wa shughuli za uvuvi, kuongeza thamani ya mazao ya uvuvi, pamoja na kutoa fursa za ajira na biashara. Nawahimize wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi kutumia fursa zilizopo katika Bandari ya Uvuvi Kilwa Masoko kwa kuwekeza katika shughuli mbalimbali zinazohusiana na sekta ya uvuvi," aliongeza Prof. Mgaya

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa TAFICO, Dkt. Suleiman Kiula, ndc , amesema Shirika hilo linaendelea na mchakato wa kushirikisha sekta binafsi pamoja na wadau mbalimbali kuhakikisha bandari hiyo inaendeshwa kwa ufanisi, kwa kutoa huduma wezeshi kwa viwango bora na nafuu ili kuvutia Meli nyingi kutumia bandari hiyo ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Dkt. Kiula amesema TAFICO inaendelea kutekeleza mikakati ya kushiriki kikamilifu katika kuendeleza shughuli za uvuvi wa kisasa na ukuzaji viumbe maji, ikiwemo uwekezaji katika Meli za uvuvi wa bahari kuu, uanzishaji wa mashamba ya kufuga samaki, miundombinu wezeshi, pamoja na kuongeza thamani ya mazao ya uvuvi.

"Kuanza kwa shughuli za Bandari ya Uvuvi Kilwa Masoko kutafungua fursa mbalimbali kwa wavuvi, wafanyabiashara na wawekezaji, huku kukiwa na matarajio ya kuongeza ajira na kuchochea shughuli za kiuchumi katika Wilaya ya Kilwa na maeneo mengine nchini," alieleza Dkt. Kiula.

Bandari ya Uvuvi Kilwa Masoko ni mradi wa kimkakati unaolenga kuimarisha shughuli za uvuvi nchini. Miundombinu ya bandari hiyo inajumuisha gati lenye urefu wa mita 315 la kuhudumia meli za uvuvi zaidi ya kumi kwa wakati mmoja, eneo la kuhifadhi samaki, mtambo wa kizalisha barafu na eneo la matengenezo ya meli, hatua inayolenga kuongeza ufanisi katika shughuli za uvuvi na mnyororo wa thamani wa mazao ya uvuvi.










NBAA YAIMARISHA UWEZO WA WAKUFUNZI WA VITUO VYA KUFUNDISHIA WATAHINIWA

NBAA YAIMARISHA UWEZO WA WAKUFUNZI WA VITUO VYA KUFUNDISHIA WATAHINIWA

Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) imeendesha warsha kwa njia ya mtandao sambamba na mafunzo ya ana kwa ana kwa wakufunzi wa vituo vya kufundishia wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi, ikiwa na lengo la kuwaongezea ujuzi na kuimarisha mbinu za ufundishaji.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Elimu ya Taaluma na Mafunzo wa NBAA, Peter Lyimo, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mtendaji wa NBAA, CPA Prof. Siasa Mzenzi, amesema mafunzo hayo yameandaliwa kwa ajili ya kuwakumbusha wakufunzi majukumu yao pamoja na kuhakikisha wanaendana na mitaala na mahitaji ya Bodi.

Amesema NBAA imeona mafanikio makubwa katika vituo vya kufundishia, ikiwemo kuongezeka kwa idadi ya wanafunzi wanaofanya mitihani ya Bodi mwaka hadi mwaka.

“Tumeona mafanikio makubwa kwenye vituo vya kufundishia wanafunzi, ambapo idadi ya wanafunzi wanaofanya mitihani ya Bodi imeendelea kuongezeka mwaka hadi mwaka. Mwaka jana wanafunzi waliofanya mitihani walikuwa zaidi ya 8,000 na hivi sasa tunaelekea kufikia 10,000,” amesema Lyimo.

Amesema lengo la NBAA ni kuongeza kiwango cha ufaulu katika mitihani mbalimbali ya Bodi na kuhakikisha wanafunzi wanapata uelewa mpana wa masuala ya Uhasibu na Ukaguzi wa hesabu, ili wanapohitimu wawe wataalamu wenye weledi na uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa kufanya jitihada zaidi katika kuboresha huduma zinazotolewa na vituo vya kufundishia, ili wanafunzi waone thamani ya kwenda kusoma katika vituo hivyo na kuwepo kwa utofauti wa kitaaluma kati ya mwanafunzi anayepitia mafunzo katika vituo hivyo na yule anayejisomea bila kupata mafunzo hayo.

Amesema NBAA itaendelea kushirikiana na vituo vya kufundishia pamoja na wakufunzi kuhakikisha wanafunzi wanapata maandalizi bora kuelekea mitihani ya Bodi na hatimaye kujenga wataalamu wenye uwezo wa kuchangia maendeleo ya Taaluma ya Uhasibu na Ukaguzi wa hesabu nchini.
Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Elimu ya Taaluma na Mafunzo wa NBAA, Peter Lyimo akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo kwa wakufunzi waliofika katika warsha ya ana kwa ana na kwa njia ya mtandao kwa Wakufunzi wa Vituo vya Kufundishia wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi.
Mkurugenzi wa Huduma za Shirika kutoka NBAA CPA Kulwa Malendeja akizungumza na wakufunzi waliofika katika warsha ya ana kwa ana na kwa njia ya mtandao kwa Wakufunzi wa Vituo vya Kufundishia wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi.
Mkuu wa Sehemu ya Elimu na Mafunzo NBAA, Sawa Ngendabanka akiwakaribisha wakufunzi wa vituo vya Kufundishia watahiniwa wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi ambao walikuwa wakifuatilia Warsha hiyo na kwa ana na kwa njia ya mtandao.
Mdhibiti Ubora Mwandamizi kutoka NACTVET Dkt. Bonaventure Ackles akitoa mada kuhusu "ufundishaji na uwezeshaji wenye ufanisi kwa wanafunzi" mada iliyotolewa kwa wakufunzi waliofika katika warsha ya ana kwa ana na kwa njia ya mtandao kwa Wakufunzi wa Vituo vya Kufundishia wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi.
Mkufunzi CPA Simon Mangesho akitoa mada kuhusu mbinu bora za kufundisha na kufundisha kikamilifu maudhui ya mitaala ya kitaaluma kwa kutumia mfano wa B2 na C1 kwa wakufunzi waliofika katika warsha ya ana kwa ana na kwa njia ya mtandao.
Mkufunzi CPA Rashid Mganwa akitoa elimu kuhusu maboresho ya B4, C4 pamoja na IFRS 18 kwa wakufunzi waliofika katika warsha ya ana kwa ana na kwa njia ya mtandao kwa Wakufunzi wa Vituo vya Kufundishia wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi.
Baadhi ya Wafanyakazi wa NBAA na Wakufunzi wa Vituo vya Kufundishia Wanafunzi 'Tuition Providers' wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi wakifuatilia mada pamoja na wale wanaofuatilia ana kwa ana na kwa njia ya mtandao kwa Wakufunzi wa Vituo vya Kufundishia wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi.
Picha ya pamoja ya wafanyakazi wa NBAA na wakufunzi wa vituo vya kufundishia watahiniwa wa Bodi 'Tuition Providers'

NBAA YAWAPIGA MSASA WANAOTARAJIA KUFANYA MITIHANI YA BODI





Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA Prof. Siasa Mzenzi, amefungua warsha ya siku moja inayowakutanisha wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi, inayofanyika ana kwa ana na kwa njia ya mtandao.

Warsha hiyo imelenga kuwajengea wanafunzi uelewa na maandalizi bora kuelekea mitihani ya Bodi, kwa kuwapatia mwongozo kuhusu mbinu za kujisomea, maandalizi ya mitihani pamoja na kuzingatia maadili ya taaluma ya Uhasibu.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa warsha hiyo, CPA Prof. Mzenzi amesema NBAA inawathamini wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi na haitarajii kuona matokeo yasiyoridhisha. Amesema kutokana na hilo, NBAA imeanzisha mpango maalumu wa kuwaandalia wanafunzi warsha na siku maalumu za mafunzo, zitakazowasaidia kupata mbinu na uelewa wa masomo mbalimbali ili kufanya vizuri katika mitihani.

Amesema warsha hiyo pia inalenga kuwafahamisha wanafunzi kile ambacho NBAA inatarajia kutoka kwao, ikiwemo kuwa na maandalizi mazuri, weledi na kuzingatia maadili ya taaluma.

Amewataka wanafunzi kutumia fursa hiyo kuongeza uelewa, kuuliza maswali na kujifunza mbinu mbalimbali zitakazowawezesha kujiandaa kikamilifu na kufanya vizuri katika mitihani ya Bodi.
Aidha, amesema NBAA itaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wanafunzi na wataalamu wanaotarajia kujiendeleza katika taaluma ya Uhasibu na Ukaguzi wa hesabu nchini.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA Prof. Siasa Mzenzi akizungumza wakati ufunguzi wa warsha ya ana kwa ana na kwa njia ya mtandao kwa wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi.
Mkurugenzi wa Huduma za Shirika kutoka NBAA CPA Kulwa Malendeja akizungumza na wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi wakati wa warsha ya ana kwa ana na kwa njia ya mtandao kwa wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi.
Mkufunzi CPA Rashid Mganwa akitoa elimu kuhusu namna ya kujiandaa na kufanya masomo ya B4, C4 pamoja na maboresho ya IFRS 10 kwa wanafunzi wanaotegemea kufanya mitihani ya Bodi waliokuwa wanafuatilia ana kwa ana na kwa njia ya mtandao.
Mkufunzi CPA Edison Leonce akitoa elimu kuhusu namna ya kujiandaa na kufanya masomo ya B2 na C1 kwa wanafunzi wanaotegemea kufanya mitihani ya Bodi waliokuwa wanafuatilia ana kwa ana na kwa njia ya mtandao.
Mkufunzi kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, CPA Dkt. Emmanuel Christopher akitoa elimu kuhusu namna ya kujiandaa na kufanya masomo ya B1 na C3 kwa wanafunzi wanaotegemea kufanya mitihani ya Bodi waliokuwa wanafuatilia ana kwa ana na kwa njia ya mtandao.
Baadhi ya wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi wakifuatilia mada pamoja na kuuliza maswai kwa wakufunzi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA Prof. Siasa Mzenzi akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya wafanyakazi wa NBAA pamoja na Wakufunzi wa wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA Prof. Siasa Mzenzi akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya wafanyakazi wa NBAA pamoja na wanafunzi wanaotarajia kufanya mitihani ya Bodi.

TAFICO INAKWENDA KUWA INJINI YA UCHUMI WA BULUU - DKT. KIULA





Shirika la uvuvi Tanzania (TAFICO) limeelezea dhamira ya kuwa injini na nyenzo ya kimkakati katika utekelezaji wa Dira 2050, hususani kujenga uchumi wa buluu, kujenga ajira, kuleta mapato ya fedha za kigeni, kukuza viwanda vinavyotegemea rasilimali za maji na kuchochea kasi ya miundombinu ya uvuvi.

Kauli hiyo imetolewa na Afisa Mtendaji Mkuu wa TAFICO, Dkt. Suleiman Kiula, ndc , leo Agosti 12, 2026, wakati akichangia mada kuhusu “Mapinduzi katika Uvuvi na Ukuzaji Endelevu wa Viumbe Maji katika Kuchochea Utekelezaji wa Dira 2050”, kwenye Kongamano la Uchumi wa Buluu linalofanyika Kizimkazi, Zanzibar.

Dkt. Kiula alikuwa akijibu swali la Muongoza Mada, Prof. Mohammed Sheikh, ambaye ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi), aliyetaka kufahamu namna TAFICO ilivyojipanga katika kutekeleza jukumu lake la kuinua sekta ya uvuvi nchini.

Akijibu, Dkt. Kiula alisema TAFICO ni Shirika lenye uwezo wa kuchochea mnyororo mzima wa thamani wa sekta ya uvuvi, kuanzia uzalishaji hadi uchakataji na uongezaji thamani.

“TAFICO inakwenda kuwa injini ya Uchumi wa Buluu nchini. Inakwenda kuwa nyenzo muhimu katika maendeleo ya sekta ya uvuvi nchini,” alisema Dkt. Kiula.

Kauli hiyo inatokana na hatua ambazo TAFICO tayari imeanza kuchukua katika kujenga uwezo wa Taifa katika sekta hiyo, akitaja utekelezaji wa Mradi wa Bandari ya Uvuvi ya Kilwa Masoko ambao umekamilika, meli moja ya uvuvi wa bahari kuu, huku mchakato wa ununuzi wa meli nyingine nne ukiendelea, mchakato wa ujenzi wa viwanda vya uchakataji wa mazao ya uvuvi, hatua inayolenga kuongeza thamani ya mazao ya uvuvi, kukuza fursa za ajira na biashara pamoja na kuongeza mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa Taifa.

Kongamano hilo lenye kauli mbiu “Hifadhi Bahari, Changamkia Fursa za Uchumi wa Buluu” ni sehemu ya shughuli zinazoambatana na Tamasha la Kizimkazi 2026, linalolenga kujadili fursa mbalimbali zinazotokana na Uchumi wa Buluu pamoja na namna ya kuzitumia kwa maendeleo endelevu.

TAFICO inalenga kutumia uwekezaji katika miundombinu, meli za uvuvi na viwanda vya uchakataji kama msingi wa kuimarisha mnyororo wa thamani wa sekta ya uvuvi na kuongeza mchango wake katika uchumi wa Taifa, sambamba na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.








"TAFICO NI MTOTO WETU"—KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE




Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo imesema ina wajibu wa kuhakikisha Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO) linaendelea kuimarika na kufikia malengo yaliyokusudiwa na Serikali.

Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Deodatus Mwanyika (Mb), leo Agosti 07,2026, wakati wa ziara ya Kamati kwenye banda la TAFICO, katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea katika viwanja vya Dkt. John Samuel Malecela, Nzuguni jijini Dodoma.

Kamati imetembelea TAFICO kwa lengo la kujionea maendeleo ya miradi ya kimkakati inayotekelezwa na Shirika katika kuimarisha sekta ya uvuvi nchini. Akiwa katika banda la TAFICO, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, pamoja na wajumbe wa Kamati, walipokea maelezo kuhusu utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kimkakati na hatua zilizofikiwa, yaliyowasilishwa na Afisa Uvuvi Mwandamizi wa TAFICO, Bw. Mgalula Lyobah.

Baada ya kupokea maelezo hayo, Mhe. Mwanyika alieleza kuridhishwa na hatua zinazopigwa na Shirika katika kutekeleza dhamira ya Serikali ya kuendeleza sekta ya uvuvi wa kisasa na kuongeza mchango wake katika uchumi wa Taifa.

"TAFICO ni mtoto wetu. Ni wajibu wetu kuhakikisha linaendelea kuimarika na kufikia malengo yaliyokusudiwa na Serikali. Tunafurahishwa na hatua zinazoendelea kuchukuliwa katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati, ambayo itaongeza tija, ajira na mchango wa sekta ya uvuvi katika maendeleo ya nchi," alisema Mhe. Mwanyika.

Kwa upande wake, Bw. Lyobah alieleza kuwa TAFICO inaendelea kutekeleza kwa ufanisi miradi ya kimkakati inayolenga kukuza uvuvi wa bahari kuu, ikiwemo ununuzi wa meli 4 ambazo ziko katika hatua ya ununuzi na kukamilika kwa ujenzi wa miundombinu wezeshi .

Kukamilika kwa miundumbinu hii kuna kwenda sambamba na kukamilika kwa ujenzi wa bandari ya uvuvi iliyojengwa na Serikali Kilwa Masoko hizi ni jitahada za Serikali katika kuleta mapinduzi katika sekta ya uvuvi nchini.

Hatua hizi zinakwenda sambamba na malengo ya Serikali ya kuendeleza uchumi wa buluu na kuhakikisha rasilimali za uvuvi zinatumika kwa manufaa ya watanzania. Alisema Bw.Mgalula

TAFICO inaendelea kutumia Maonesho ya Nanenane kama jukwaa la kutoa elimu kwa wananchi kuhusu shughuli zake, huduma mbalimbali zinazotolewa na Shirika pamoja na fursa zinazopatikana katika sekta ya uvuvi na uchumi wa buluu.









NBAA YAENDELEA KUTOA HUDUMA ZA KITAALUMA MAONESHO YA NANENANE 2026


Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) imeendelea kusogeza huduma zake karibu na wananchi kwa kushiriki Maonesho ya Kimataifa ya Kilimo (Nanenane) 2026 yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samuel Malecela, Nzuguni, jijini Dodoma.

Kupitia banda la NBAA, wananchi, wanafunzi, wahitimu na wadau mbalimbali wanapata fursa ya kujifunza kuhusu Taaluma ya Uhasibu, pamoja na kupata huduma mbalimbali za kitaaluma zinazotolewa na Bodi.

Huduma zinazotolewa katika banda hilo ni pamoja na usajili wa mitihani kuanzia ngazi ya chini "Accounting Technician" (ATEC) hadi ngazi ya Taaluma "Profesion" yaani CPA. Pia usajili wa uhamaji wa madaraja kwenda ACPA, ACPA-PP na FCPA au FCPA - PP pamoja na hayo wanatoa elimu juu ya usajili wa kampuni za Uhasibu na Ukaguzi, kozi za muda mfupi, pamoja na ushauri kuhusu fursa mbalimbali zinazotolewa na NBAA.

Aidha, wanafunzi wanaotamani kujiunga na Taaluma ya Uhasibu watapatiwa elimu kuhusu hatua za kuanza safari ya kuwa Wahasibu na Wakaguzi wa hesabu waliosajiliwa.

Ushiriki wa NBAA katika maonesho hayo ni sehemu ya jitihada za Bodi za kuendelea kuwafikia wananchi, kuongeza uelewa kuhusu huduma zake na kuhamasisha vijana wengi zaidi kujiunga na Taaluma ya Uhasibu ili kuchangia maendeleo ya uchumi wa nchi.

Maonesho ya Nanenane 2026 yanaendelea na kaulimbiu ni "Tambua Soko, Ongeza Tija, Kuendeleza Dira ya Taifa 2050." NBAA imewahimiza wananchi kutembelea banda lake lililondani ya Banda la Wizara ya Fedha ili kupata elimu, ushauri wa kitaaluma na huduma mbalimbali zinazotolewa na Bodi.
Watumishi wa NBAA wakiwa kwenye picha ya pamoja kwenye Maonesho ya Kimataifa ya Kilimo ya Nanenane 2026 yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samuel Malecela, Nzuguni, jijini Dodoma.
Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano wa NBAA, Magreth Kageya akitoa elimu kwa mwananchi aliyetembelea Banda la Bodi hiyo katika Maonesho ya Kimataifa ya Kilimo ya Nanenane 2026.
Mfanyakazi wa NBAA Happiness Mwamwembe akitoa elimu kwa wananchi waliofika katika Banda la Bodi hiyo katika Maonesho ya Kimataifa ya Kilimo ya Nanenane 2026
Picha mbalimbali zikionyesha shughuli zinazoendelea katika banda la NBAA