HABARI

Theme images by kelvinjay. Powered by Blogger.

MATUKIO

MICHEZO

SIASA

NBAA YAREJESHA KWA JAMII KUPITIA UCHANGIAJI DAMU NA MISAADA MOROGORO


Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) imeendelea kuonesha dhamira yake ya kurejesha kwa jamii kwa kushiriki katika zoezi la uchangiaji damu pamoja na kutoa misaada mbalimbali kwa wagonjwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro.

Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo, Mkurugenzi Mtendaji wa NBAA, CPA Prof. Siasa I. Mzenzi, amesema kuwa hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za Bodi kurudisha kwa jamii kupitia ushirikiano kati ya NBAA, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro, pamoja na wahasibu waliokuwa kwenye mafunzo yanayoratibiwa na Bodi hiyo.

Alieleza kuwa wahasibu hao walijitokeza kwa wingi kushiriki katika uchangiaji wa damu salama kwa ajili ya kusaidia wagonjwa wanaohitaji huduma hiyo muhimu.

“Katika kuendeleza juhudi za kuwafikia wananchi, NBAA imetoa msaada wa vifaa muhimu ikiwemo pampers na mahitaji mengine kwa ajili ya watoto wanaopatiwa matibabu hospitalini hapa. Hatua hii inalenga kuboresha huduma na kuwafariji wagonjwa pamoja na walezi wao,” alisema CPA Prof. Mzenzi.

Aidha, wahasibu waliokuwa wakihudhuria mafunzo, wakiwemo washiriki wa Warsha ya Uendelevu ya IPSAS, walichangia fedha kwa ajili ya kusaidia kugharamia vipimo na dawa kwa wagonjwa wasiokuwa na uwezo wa kumudu gharama hizo.

Mchango huo uliwakilishwa na CPA Sura Sabas Kimboka, ambaye ni Mkurugenzi wa Huduma za Usaidizi katika Mahakama ya Rufani za Kodi (TRAT), kwa kushirikiana na washiriki wengine wa mafunzo hayo.

Kwa upande wake, Dkt. Zaid Kihando, Mratibu wa Huduma za Tiba aliyemwakilisha Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro, aliishukuru NBAA pamoja na wahasibu kwa kuendelea kuona umuhimu wa kusaidia jamii kupitia utoaji wa misaada na uchangiaji damu.

Hatua hiyo imeelezwa kuwa ni sehemu ya dhamira ya NBAA ya kuchangia maendeleo ya jamii na kusaidia sekta ya afya sambamba na majukumu yake ya kitaaluma. Wananchi na wadau mbalimbali wameipongeza Bodi hiyo kwa moyo wa kujitolea na mshikamano uliooneshwa, wakieleza kuwa ni mfano bora wa taasisi kushiriki katika shughuli za kijamii.

Kupitia juhudi hizi, NBAA inaendelea kudhihirisha kuwa mchango wake hauishii kwenye taaluma pekee, bali pia unalenga kuboresha maisha ya jamii kwa ujumla.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) CPA Prof. Siasa I. Mzenzi akishuhudia makabidhiano ya misaada kati ya Mkurugenzi wa Huduma za Viwango vya Kiuhasibu, Utafiti na Huduma za Ufundi wa NBAA, Angyelile Tende pamoja na Dkt. Zaid Kihando, Mratibu wa Huduma za Tiba aliyemwakilisha Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro.
Baadhi ya watumishi wa NBAA, wahasibu pamoja na madakatari wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro wakiwa kwenye picha ya pamoja mara baada ya kukabidhi misaada hiyo katika hospitali hiyo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) CPA Prof. Siasa I. Mzenzi akizungumza kuhusu namna walivyoguswa kuja kutoa misaada katika 
Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro
Dkt. Zaid Kihando, Mratibu wa Huduma za Tiba aliyemwakilisha Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro akiwakaribisha wageni kutoka NBAA wakiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi hiyo CPA Prof. Siasa I. Mzenzi pamoja na Wahasibu waliofika katika hospitali hiyo kwa ajili ya kutoa misaada.
Mkurugenzi wa Huduma za Usaidizi katika Mahakama ya Rufani za Kodi (TRAT), CPA Sura Sabas Kimboka ambaye aliwawakilisha washiriki wengine wa mafunzo ya NBAA akizungumza namna walivyoweza kufanya malipo ya matibabu kwa ajili ya baadhi ya wagonjwa wanaotibiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro.


MAHAFALI YA 48 YA BODI YA NBAA YAFANA


Wahitimu wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu (NBAA) wakiwa kwenye maadamano ya kitaaluma wakati wa mahafali ya 48 ya Bodi hiyo yaliyofanyika katika hoteli ya APC Bunju, Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA. Prof. Sylvia S. Temu akipokea maadamano ya kitaaluma pamoja na viongozi wa Bodi pamoja na wajumbe wa Bodi hiyo wakati wa mahafali ya 48 ya Bodi hiyo.

Mwenyekiti wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA. Prof. Sylvia S. Temu akizungumza kuhusu namna Bodi hiyo ilivyofanikisha kuongeza idadi ya wahitimu kwa mwaka huu wakati wa mahafali ya 48 ya NBAA.

Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA Pius A. Maneno akisoma hotuba yake kuhusu mafanikio yaliyopatikana kwenye kipindi chake cha uongoziwake wakati wa mahafali ya 48 ya Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA).
Baadhi ya Wahitimu pamoja na wageni waalikwa wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi Mwenyekiti wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA. Prof. Sylvia S. Temu  kwenye mahafali ya 48 ya Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA).
Wahitimu wa ngazi ya CPA wakisoma viapo vyao wakati wa mahafali ya 48 ya Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA).
Mwenyekiti wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA. Prof. Sylvia S. Temu akiwatunuku wahitimu kwenye mahafali ya 48 ya Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA).
Wahitimu wakishangilia mara baada ya kutunukiwa CPA wakati wa mahafali ya 48 ya Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA)
Mwenyekiti wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA. Prof. Sylvia S. Temu akitoa vyeti kwa wahitimu waliofanya vizuri kwenye mitihani ya Bodi wakati wa mahafali ya 48.
Mwenyekiti wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), CPA. Prof. Sylvia S. Temu akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya wafanyakazi wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu (NBAA) wakati wa mahafali ya 48 ya Bodi hiyo.

Ecobank Group Yaweka Rekodi ya Ongezeko la Mikopo kwa Biashara za Wanawake Afrika




Ecobank Group imetangaza ukuaji mkubwa wa mikopo, likilenga kuimarisha ujasiriamali wa wanawake barani Afrika. Ecobank imerekodi ongezeko kubwa la asilimia 194 katika utoaji wa mikopo kwa biashara zinazoongozwa na wanawake, likifikia dola za Marekani milioni 780 mwaka 2025 kutoka dola milioni 265 mwaka 2024. Hatua hii inaashiria mafanikio ya juhudi za benki hiyo katika kukuza usawa wa kijinsia na kuimarisha uchumi wa ndani barani Afrika.

Taarifa hiyo ilitolewa wakati wa uzinduzi wa Ripoti ya Programu ya Jinsia ya Ecobank, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya International Women’s Day 2026.

Wataalamu wa uchumi wanaeleza kuwa wanawake wajasiriamali wana mchango mkubwa katika kukuza ajira, kusaidia familia na kuimarisha minyororo ya thamani ya ndani. Hata hivyo, biashara nyingi zinazoongozwa na wanawake bado zinakabiliwa na changamoto ya upatikanaji wa mitaji, huku pengo la ufadhili likikadiriwa kufikia dola bilioni 42 barani Afrika.

Ili kukabiliana na changamoto hiyo, Ecobank imeendelea kuwekeza katika mipango maalum inayolenga wanawake kwa kutoa mikopo rafiki, mafunzo ya biashara, ushauri na fursa za kuunganishwa na masoko ya kikanda. Lengo ni kuwasaidia wanawake kukuza biashara endelevu na zenye ushindani.

Moja ya mipango hiyo ni programu ya Ellevate, iliyoanzishwa mwaka 2020 kusaidia biashara za wanawake zilizoathiriwa na janga la COVID-19. Programu hiyo sasa imekua na kuwa moja ya miradi mikubwa zaidi barani Afrika, ikihudumia zaidi ya wanawake wajasiriamali 103,000 katika nchi 26. Zaidi ya wanawake 21,000 wamejiunga na mpango huo mwaka 2025 pekee, huku zaidi ya 24,000 wakinufaika na mafunzo na ushauri wa kibiashara.

Aidha, Ecobank imezindua programu ya MAMA inayolenga kuwasaidia wanawake wanaofanya biashara katika sekta isiyo rasmi, kwa kuwapatia mikopo nafuu na kuwasaidia kuingia katika mfumo rasmi wa kifedha. Mpango huo tayari umewafikia zaidi ya wanawake 10,000, huku zaidi ya 2,000 wakipata mikopo yenye thamani ya zaidi ya dola milioni 1.8.

Katika juhudi za kuongeza upatikanaji wa mtaji, Ecobank pia ilizindua hati fungani maalum ya jinsia nchini Côte d’Ivoire mwaka 2025, iliyokusanya zaidi ya faranga za CFA bilioni 11 ndani ya saa 48. Fedha hizo zinatarajiwa kusaidia kutoa mikopo kwa zaidi ya biashara 1,200 ndogo na za kati zinazomilikiwa na wanawake.

Akizungumza kuhusu mafanikio hayo, Mkurugenzi Mtendaji Mkuu wa Kundi la Ecobank, Jeremy Awori alisema wanawake wajasiriamali ni mhimili muhimu wa ukuaji wa uchumi wa Afrika, lakini bado wanakumbana na changamoto za upatikanaji wa fedha.

“Ecobank inaendelea kushughulikia changamoto hiyo kwa kuunganisha mitaji, ujuzi na fursa za masoko kupitia mtandao wake wa bara zima. Ongezeko hili linaonyesha wazi mahitaji makubwa ya huduma hizi na mafanikio ya programu zetu,” alisema.

Kwa siku zijazo, Ecobank inapanga kupanua zaidi programu ya Ellevate katika masoko yote inayofanya kazi, kuimarisha huduma zisizo za kifedha kama zana za kidijitali, pamoja na kuanzisha bidhaa mpya zitakazolenga wanawake ili kuongeza ushiriki wao katika uchumi wa Afrika.