Taharuki ya bomu kanisa la KKKT Kunduchi, Dar

Wapitanjia wakiwa karibu na kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania(KKKT)Usharika wa Kunduchi eneo la Mtongani jijini Dar es salaam jana.
Taharuki imeikumba Dar es Salaam  na miji mingine, baada ya bomu kulipuliwa mita chache kutoka Kanisa la Kiinjili la Kilutheli la (KKKT)  lililoko Kunduchi Mtongani.
Bomu la machozi lilipuliwa jana mchana karibu na kanisa hilo wakati polisi wakiwafurumusha wahalifu waliojificha ndani ya jengo lililopo jirani na kanisa.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kinondoni, Charles Kenyela, alisema jana wakati akitoa ufafanuzi kuhusu madai ya kulipuliwa kanisa la Kunduchi.
Alisema polisi iliarifiwa na wasiri kuwa wahalifu walikuwa wakitumia jengo hilo lililo mita 150 kutoka kanisani kupanga uhalifu na  wengine waliligeuza kijiwe cha mihadarati na  kamali.
Hali hiyo ilisababisha majirani kukimbia kwa hofu wakidhani bomu limelipua kanisa wakihusisha tukio hilo na lile la Jumapili iliyopita ambapo bomu liliporushwa kwenye Kanisa Katoliki la Mtakatifu Yoseph Mfanyakazi la  Olasiti, jijini Arusha na kuua waumini watatu na kujeruhi 67.
Taharuki na hofu zilizagaa sehemu nyingi nchini kutokana na kuenea  taarifa za mlipuko.
Kamanda Kenyela, akizungumza na wanahabari alisema uvumi huo wa kanisa kulipuliwa, ulizagaa ndani na nje ya jiji na kueleza kuwa polisi  ilichukua hatua hiyo baada ya kupata taarifa za  wahalifu waliojihami ndani ya jengo hilo lisilokaliwa na watu.
Alisema polisi walipofika nje ya jengo hilo walithibitisha kuwa lilikuwa na  watu kama ilivyodaiwa na kwamba walikuwa wanavuta bangi, kucheza kamari na kupanga uhalifu.
Aliwatetea  askari wake kuwa wasingeingia moja kwa moja kwani hawakufahamu watu hao walikuwa na silaha za aina gani.
“Namna ya kuwapata haikuwa rahisi,  waliamua kurusha bomu la machozi kuwashtua , kishindo hicho kiliwatawanya watu hao ambao wengine walikimbilia baharini na wengine kanisani, “ alisema na kuongeza:
“Kanisani kulikuwa na waumini,  walitusaidia kuwakamata watu sita walikimbilia humo,”aliowataja  kuwa ni mwanafunzi wa kidato cha nne katika Sekondari  ya Boko na mtoto mwenye miaka 13 (majina yanahifadhiwa kwa sababu ya umri).
 Wengine ni  mwanafunzi wa kompyuta wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam  tawi la Mbezi Beach Japhet Nicodemas (20),  kondakta wa daladala Kasimu Seif (21) Nasir Kajembe  (25) na Hussein Sadiki (18) wakazi wa Kunduchi,  hata hivyo wengine zaidi ya 40 walitoroka.
Wahalifu hao kwa mujibu wa Kenyela walikutwa na bangi, silaha kadhaa zikiwamo nondo. Kenyela alipoulizwa sababu za kutumia bomu badala ya mbinu nyingine, alisema  ni maamuzi ya polisi  kulingana na tukio.
Alisema polisi wapo kwenye misako ambayo itawalazimu ikibidi kutumia silaha kusaka wahalifu.
CHANZO: NIPASHE

No comments

Powered by Blogger.