Polisi na wananchi wakiangalia mabaki ya nyumba iliyochomwa moto
Wiki iliyopita katika ukurasa huu, tuliwaletea ripoti maalumu kuhusu mauaji ya kinyama yaliyotokea mkoani Simiyu kupitia Baraza la Kimila maarufu kama Dagashida.
Wiki iliyopita katika ukurasa huu, tuliwaletea ripoti maalumu kuhusu mauaji ya kinyama yaliyotokea mkoani Simiyu kupitia Baraza la Kimila maarufu kama Dagashida.
Pamoja na mambo mengine, ripoti hiyo ilieleza hali
ilivyo mbaya na kwamba katika mwaka mmoja uliopita, wastani wa watu
watatu waliuawa na Dagashida kila wiki wakiwamo wanawake na watoto. Pia
wanavijiji wa maeneo husika wanavyoshindwa kutoa ushirikiano kwa polisi
wakihofia ukatili au kuuawa na kundi hilo.
Leo tunaendelea na ripoti hiyo ambayo pamoja na
mambo mengine inaeleza namna Dagashida linavyotumika katika jamii,
viongozi wanavyochapwa bakora, pia juhudi na msimamo wa Jeshi la Polisi
na harakati za kusambaratisha baraza hilo.
Baraza Linatumika kwa visasi
Katibu wa Umoja wa Wazazi mkoani humo, Fadhil
Murani anasimulia akisema kuwa mbaya zaidi baraza hilo limekuwa likitoa
hukumu kwa kutumia hisia na tuhuma zisizokuwa na uhakika.
“Halafu mtuhumiwa wakishamweka katikati,
haruhusiwi kujitetea wala kuzungumza chochote, matokeo yake wanamchoma
moto au wanamuua kwa mapanga,” anasema Murani.
Anasimulia kuwa asilimia kubwa ya vijana wa baraza
hilo kwa sasa wanatumiwa na watu wenye fedha katika ugomvi wa mipaka ya
ardhi na mashamba.
“Kwa mfano, kama una adui yako ukapeleka pesa
kidogo kwa wazee wa baraza hilo au ukawanunulia pombe, halafu ukamshtaki
mtu, lazima utasikia yule mtu kavamiwa usiku na kuuawa kwa mapanga au
watampigia mbiu na kamchoma moto,” anasema Murani.
Mmoja wa wanavijiji kutoka Kata ya Mahuni, Deo
Ngulyati anasema kuwa malengo halisi ya kuwepo kwa baraza hilo yamepotea
kwani limegeuka kuwa adui na hasara katika ustawi wa jamii.
“Zamani lilikuwa ni baraza linalosaidia ukuaji wa
ustawi wa jamii na kuchochea maendeleo, walidhibiti migogoro,
walihamasishana kwenye misiba na majanga, kujenga huduma za kijamii na
walizuia uhalifu,” alisema Ngulyati.
ENDELEA KUSOMA HABARI HII KWA KUBOFYA HAPA CHINI
Mwenyekiti anachapwa bakora
Taarifa nyingine kutoka ndani katika vijiji
mbalimbali mkoani humo, zinaeleza kuwa baraza hilo limekuwa likitoa
adhabu ya viboko kwa viongozi wa Serikali za Mitaa.
Baadhi ya viongozi wa kijiji (majina tunayo), wanadaiwa kukutana
na adhabu hizo hivi karibuni kabla ya Mkoa mpya wa Simiyu kuanza kazi
rasmi.
Kamanda wa Polisi mkoani humo, Salum Msangi
anasema kuwa taarifa za kuwepo kwa adhabu hiyo miongoni mwa viongozi wa
vijiji anazo na kwamba imekuwa ikiendelea, huku viongozi hao wakiona
aibu kusema.
“Sisi taarifa tunazipata, ila kuna baadhi wanaogopa kushtaki, sijui wanaona aibu?” anasema.
Hata hivyo, mmoja kati ya viongozi hao ambaye ni
mwenyekiti wa Kijiji cha Nyamiswi, Leah Muhami anakiri kuwepo kwa
unyanyasaji huo. “Wazee wa baraza hilo hivi karibuni walitaka kuniweka
katikati wakitaka kuniadhibu, lakini nilionyesha msimamo wangu
wakashindwa,” anasema Leah.
Anasema kuwa alikumbwa na mkasa huo baada ya
kuwatetea baadhi ya wanakijiji waliotaka kudhulumiwa ardhi. “Hilo ndilo
lilikuwa kosa langu, usipokuwa na msimamo watakusumbua sana,” anasema.
Ni tegemeo la Wanasiasa
Zipo pia taarifa za uhakika kwamba Dagashida
limekuwa likitumika pia kisiasa kwa baadhi ya wanasiasa kama ngao yao
kutimiza azma zao.
Ukweli wa taarifa hizo unathibitishwa na
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Itilima mkoani humo, David
Nyalamu anayesema: “Dagashida ndiyo kikao cha mwisho katika harakati za
kampeni za uchaguzi kwa viongozi wa kisiasa mkoani Simiyu.”
Nyalamu anasema kuwa kabla ya kupiga kura katika
hatua za mwisho kwenye uchaguzi, wazee wa baraza hilo ndiyo
hufahamishana nani anayetakiwa kuwa kiongozi.
“Watakayemjadili kwenye vikao vyao, ujue tayari
ameshafanikiwa kuwa kiongozi, hatua hizo hufanyika kwa mbunge, diwani au
mwenyekiti wa kijiji,” anasema Nyilamu.
Anaongeza kuwa ushindi hupatikana kutokana na ushawishi uliopo kwa baraza hilo, ukalinganisha na elimu ndogo kwa wanakijiji.
“Nikwambie, huku ni Watanzania wachache wanaojua
kusoma na kuandika kwa hiyo watakaa kila sehemu kuwapigia kura
wanakijiji kwa kiongozi wanayemtaka,” anasema.
Hata hivyo Katibu wa Chama Cha Mapinduzi(CCM), wilayani Itilima, Jumaa Iadhi amekana tuhuma hizo akisema hazina ukweli wowote.
“Dagashida ni sehemu ya wanakijiji, kwa hivyo sisi
tunafanya kampeni zetu kwa kuwajumuisha wanakijiji wote, wala hatutumii
ushawishi wa kundi hilo bali sisi ndiyo tunatengeneza ushawishi kwa
wote,”anasema Iadhi.
Changamoto kwa polisi
Moja kati ya changamoto kubwa na ya muda mrefu kwa
Jeshi la Polisi mkoani Simiyu ni hofu ya kuendelea kusambaa kwa mauaji
na hukumu hizo.
Baadhi ya askari Polisi mkoani humo wamezungumza
kwa nyakati tofauti juu ya changamoto inayoendelea kujitokeza kupitia
baraza hilo.
Mmoja kati ya askari hao aliyeomba jina lake
lihifadhiwe, anasema kuwa vijana wa baraza hilo wakishatekeleza hukumu
yao kwa raia hukimbilia msituni na kujificha mfano wa Kundi la Al-
Shabaab wakiwindana na polisi.
Anaongeza kuwa changamoto nyingine iliyopo ni viongozi wa Serikali za Mitaa na viongozi wa kisiasa kutotoa ushirikiano.
“Hakuna mwanasiasa, awe diwani au mwenyekiti wa
kijiji anayeingia bila kushirikisha baraza hilo. Kwa hivyo wanapokuwa
madarakani wanakosa ujasiri wa kuwakemea kwa maovu wanayoyafanya,”
anasema askari huyo.
Akichangia hoja hiyo, askari mwingine katika kundi
hilo anasema kuwa kwa sasa kuna baadhi ya wanakijiji wameshaanza kutoa
taarifa za matukio ya mauaji yanapofanyika.
“Tukimkamta mmoja wa vijana wa baraza hilo
changamoto nyingine inajitokeza kwenye ushahidi mahakamani. Hakuna
mwanakijiji atakayekubali kusimama mahakamani kutoa ushahidi, kwa hofu
ya kuuawa. Inabidi mtuhumiwa aachiwe huru kwa kukosa ushahidi,” anasema
askari huyo.
Mapambano ya Jeshi la Polisi
Kamishna Msaidizi wa Polisi na Kamanda wa Polisi,
Mkoa wa Simiyu, Salum Msangi anakiri kuwepo kwa baraza hilo akisema kwa
sasa baraza hilo linaongozwa na kundi la vijana matapeli wa kimila.
“Zamani lilikuwa ni baraza linalosaidia ukuaji wa ustawi wa
jamii na kuchochea maendeleo. Walidhibiti migogoro, walihamasishana
kwenye misiba na majanga, kujenga huduma za kijamii na walizuia uhalifu,
lakini kwa sasa ni kundi la wahuni,” anasema Kamanda Msangi.
Katika harakati za kupambana na baraza hilo,
Kamanda Msangi anasema kuwa baada ya kuhamishiwa mkoani humo,
walianzisha operesheni maalumu katika wilaya na vijiji vyote kupiga
marufuku Dagashida.
“Lakini pia tulianza kutoa elimu kwa kila kijiji,
hali ilikuwa ni mbaya sana ya ukatili wa baraza hilo, mfano Kijiji cha
Longolambogo,”anasema Msangi.
Kamanda Msangi anafafanua kuwa takwimu alizonazo
zinaonyesha kuwa katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita, wanakijiji
watano walikuwa wakiuawa na baraza hilo kila siku mkoani humo kwa tuhuma
mbalimbali ikiwamo visasi.
“Nilipoingia Simiyu hali ilikuwa mbaya sana.
Tulipokea ripoti za matukio kama hayo, hata ya watu watano kuuawa kwa
siku. Kuona hivyo kwa kushirikiana na Mkuu wa Mkoa tulizunguka Mkoa wa
Simiyu wote kupiga marufuku uwepo wa baraza hilo…,”anaeleza Kamanda
Msangi.
Maelezo hayo ya Kamanda Msangi yanamaanisha kuwa
katika kila siku saba za wiki watu 35 waliuawa mkoani Simiyu na katika
mwezi mmoja wastani wa watu 150 waliuawa katika matukio yaliyohusisha
kikundi cha Dagashida.
Anaongeza: “Kwa sasa tumekuwa tukipokea taarifa za matukio kama hayo baada ya mwezi mmoja.”
Anataja wilaya inayoendelea kuathirika na unyama
huo kuwa ni Itilima, lakini anasema kwamba Jeshi la Polisi limeamua
kupambana kuhakikisha Dagashida linakomesha ukatili wake..
Hata hivyo, anakiri kuwepo kwa changamoto ya kukosa ushirikiano kutoka kwa wananchi wakihofia usalama wao.
Itaendelea wiki ijayo
MWANANCHI
MWANANCHI




No comments:
Post a Comment