Ndugu wasomaji wetu tunaomba support yenu kwa kutangaza nasi hapa kwenye hii blog kwa bei nafuu ili tuweze kuendelea kutoa habari bila tatizo lolote. Wasiliana nasi kupitia namba +255713363965 / +255755274953. Tunashukuru kwa ushirikiano wenu.
Peter haraka akataka kuhakikisha kile alichokisikia, naye akawa mmoja wa watu walioenda kushuhudia kama mbwa huyo anayetajwa kuwa mbwa wa Tinonko kama kweli alikuwa ni yule simba aliyepotea siku chache nyuma pale nyumbani.
Hivyo basi akawa mmoja wa wale watu walioenda kushuhudia walichoambiwa wakati huo Sajenti Ngowi naye haraka akawa maarufu kambini hapo kwa ugunduzi wake huo.
Simba akiwa ndani ya banda la wazi, alianza kutatanishwa na harufu mbili alizoziingiza kupitia pua zake; moja ikiwa ya Tinonko kama kawaida, lakini nyingine ilikuwa ni harufu ya adui yake mkubwa, Peter.
Japo kuwa alikuwa amefumba macho yake kwa aibu ya umati wa watu waliokuja kumtazama, lakini alipoinasa harufu hii akafumbua macho yake kutazama wapi inapotokea, alipomuona Peter akanguruma kwa ukali na kubweka mno.
Peter akiwa na mavazi yake ya Jeshi na cheo chake kikionesha ni Koplo, alikuwa karibu zaidi na baada ya kugundua ndiye simba, akajipenyeza kutoka kwenye umati ule na kupiga simu haraka kwa Suzy, akamuelezea kila kitu. Unaweza ukavuta picha mshangao wa Suzy baada ya kupewa taarifa ile.
Lakini baada ya kuongea na huyo kimada wake haraka akamtafuta Farudume; “Hallow bosi, naomba nikuone leo.”
“sawa!” ilijibu sauti ya upande wa pili na kukata simu haraka.
Siku hiyo kwa presha aliyokuwa nayo hakuwa na uoga wa kutaka kumuona Farudume, Peter alitaka kumuelezea kila kitu bosi wake huyo kuhusu mashaka yake kwa yule mbwa wa Tinonko.
Alichofikiria yeye ni kwamba huenda yule mbwa alikuwa akimwinda yeye pale Jeshini, ili amrarue hayo ni baada ya kumjeruhi Suzy na kusababisha mimba kushindikana kutolewa siku ya kwanza huku yeye akinusurika punje tu.
Farudume akiwa ndani ya mavazi yake ya
kijeshi alionekana kuingia moja kwa moja pale kambini na kuelekea ndani ya jengo lile ambalo mara ya kwanza alionekana Simba akiingia.
Akapitiliza moja kwa moja hadi ndani ya sehemu fulani ambayo hufunguliwa na kadi maalumu kisha akaingia ndani ya chumba chenye giza mno kilichokuwa na watu wengine wanne.
Watatu kati yao wakiwa ni wale wanajeshi wa kikosi cha utesaji waliowahi kumuadhibu Tinonko siku chache za nyuma na mmoja akiwa ni Peter.
Faru akiwa amechukia kwa kuitwa haraka kwenye mkutano ambao mara nyingi huwa wa siri sana na yeye mwenyewe ndiye aliyekuwa akiutisha, alistaajabu Peter atakuwa na kitu gani cha kuwaambia.
Tena akajiapiza ikiwa hatakuwa na jambo la maana atamnyoosha kwa adhabu kubwa zaidi kuwahi kutoa kwa mwanajeshi yoyote wa cheo chake.
Peter hakutaka kusubiri cha kuongea haraka akaenda kwenye pointi; “bosi kwanza samahani kwa kukuharibia shughuli zako, lakini hili jambo ni lazima nikwambie maana nahisi litatuletea matatizo.”
Wale mabedui wanne wakatulia kimya bila kusema chochote jambo lililomfanya haraka Peter aanze kujisemesha mwenyewe.
“Aaah bosi, nataka kukwambia siku zote nimekuwa nikipambana kukamilisha kazi unazonituma kwa mke wa Tinonko, lakini kuna mbwa mmoja simuelewi kabisa,” alianza Peter wenzake wakawa kama vile wamepigwa na butwaa lakini walinyamaza kimya hasa kwa kuwa Faru mwenyewe alitulia kimya.
“Ndiyo, siku ya kwanza mbwa huyu alishawahi kunivamia hospitali wakati mke wa Tinonko akiwa anataka kutoa mimba na kusababisha zoezi hilo kushindikana.
“Siku ya pili nikiwa nyumbani kwa mke wa Tinonko mbwa huyu ndiye aliyewahi kunivamia na kunifanya nilale uraiani hadi nikapewa adhabu hapa kambini,
“Mbwa huyu alimjeruhi rafiki yangu kwa kumng’ata mguuni pale alipotaka kumdhuru mke wa Tinonko, lakini mbaya zaidi mbwa huyu nasikia amefika hapa kambini, lakini kwa bahati nzuri amekamatwa na kitengo cha mbwa huko chini na hapa tunavyoongea nimehakikisha ndiye mwenyewe na hapa atakuwa amekuja kunifuata mimi anijeruhi, bosi nahisi kuna tatizo kuhusu huyu mbwa,” alisema kwa pupa Peter akionekana muoga zaidi ya kuwa mtu mwenye pointi.
“Peter upo sawa au unataka kunipima mimi ni nani?” aliuliza Farudume kwa ukali, kidogo.
“Bosi ni kweli kabisa, lakini tatizo mbwa huyu si wa kawaida bali mmiliki wake ni nani? ndilo hasa linalonichanganya,” aliongea Peter akimuacha kila mtu kwenye shauku.
“Ni nani!” alihoji Faru.
“Tinonko.”
Alipojibu hivi kila mtu akashtuka na hapo ndiyo wakamuelewa Peter, Farudume hakutaka hilo liwe jambo zito akawaondoa haraka wale majambazi wenzake na kisha akatulia ndani ya chumba hicho kwa dakika kadhaa kisha akatoka nje.
Farudume alionekana usiku akiwa kwenye chumba kidogo cha udongo chenye mwanga wa mshumaa.
Alitulia akiwa amekunja miguu juu ya majani ya mgomba akimsikiliza mtu mmoja mfupi aliyeonekana wazi ni mbirikimo kutokana na ukomavu wa sura huku kidevu chake kikisheheni ndevu ndefu na nyeupe mno.
“Mtoto amezungukwa na moto ukilazimisha mambo utaungua. Huyu mbwa amejua harufu ya bwana wake nitakupa dawa ya kumsahaulisha mara moja,” alisema mtu huyo kwa kiswahili cha Kikongo akimwambia Farudume.
Je, mtu huyo ni nani na kwanini Farudume alienda kwake?
ITAENDELEA JUMATATU
No comments:
Post a Comment