HABARI

Theme images by kelvinjay. Powered by Blogger.

MATUKIO

MICHEZO

SIASA

CUF KUIFIKISHA KORTINI WAKALA WA USAJILI, UFILISI NA UDHAMINI (RITA)

Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi(CUF), Maalim Seif Sharif Hamad, akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari Dar es Salaam leo, kuhusu madai ya muendelezo wa hujuma dhidi ya chama hicho zinazofanywa na ofisi ya msaji wa vyama vya siasa nchini. Kulia ni Mbunge wa Viti Maalumu wa chama hicho, Seveline Mwijage.
Maofisa wa Chama hicho wakiwa meza kuu wakati wa mkutano na wanahabari.
Wabunge wa chama hicho wakiwa kwenye mkutano huo.
Baadhi ya wanahabari wakiwa kwenye mkutano huo
Wapiga picha kutoka vyombo mbalimbali wakichukua taarifa hiyo. 

Na Dotto Mwaibale

CHAMA cha Wananchi (CUF), kinatarajia kumfikisha mahakamani Wakala wa Usajili Ufilisi na Udhamini (RITA)kwa kukiuka taratibu za sheria ya wadhamini kwa kutojiridhisha juu ya uhalali wa majina ya Bodi ya Wadhamini yaliyofikishwa kwake kama yalipitishwa na kikao halali cha chama kwa mujibu wa katiba.

Katibu Mkuu wa Chama hicho, Maalim Seif jijini Dar es Salaam leo wakati akizungumza na waandishi wa habari.

Alisema wanachukua hautua hiyo kutokana RITA kushindwa kutumia mwongozo na weledi katika kutekeleza majukumu yao na badala yake wamesukumwa na utashi binafsi kwa ajili ya hujuma dhidi ya chama hicho.

Chama chetu kimepatwa na mshituko mkubwa sana, kuona taasisi kubwa nan yeti yenye dhamana kubwa katika nchi inaweza kufanya vitendo vya ovyo. RITA ni taasisi inayobeba maisha ya watu ya kila siku. 



Licha ya kusajili Bodi za Wadhamini, inasajili vizazi na vifo, ndoa, talaka na inatunza wosia kwa ajili ya mirathi,” alisema Maalim.Alisema michakato wa kufungua kesi hiyo inaanza leo ambapo alieleza kuwa tayari wamekwisha agiza mwawakili kulishughulikia. 

Kutokana na matarajio ya ufunguzi wa kesi hiyo watawasilisha maombi mbele ya Mahakama Kuu kuitaka isimamishe kesi nyingine zote walizofungua kuhusiana na kadhia hiyo hadi hapo shauri linalohusu uhalali wa maamuzi ya RITA litakapoamuliwa.

Maalim alisema kusajiliwa kwa bodi hiyo ambayo aliiita kuwa ni bodi feki, alieleza kwamba ni mwendelezo wa kukihujumu na kukidhoofisha chama kunakofanywa dola kupitia kwa Msajili wa Vyama vya Siasa pamoja na Profesa Ibrahim Lipumba na kundi lake.

Alitaja mambo manne ambayo yalikuwa msukumo wa kusajiliwa kwa bodi hiyo. Alisema kuwa ni kwa ajili ya kufuta kesi zote zilizofunguliwa na ambazo zinawaelemea licha ya kutumia nguvu kubwa ya dola, kufungua akaunti mpya ya benki ili kumwezesha Profesa Lipumba kupata ruzuku.

Aliongeza mengine kuwa ni Bodi hiyo kuwezesha udhibiti wa Ofisi za Makao Makuu, Zanzibar pamoaja na kumwondoa madarakani Katibu Mkuu Maalim Seif Hamad na hivyo kufanikisha njama za kuwapokonya haki Wazanzibar kwa maamuzi yao ya Oktoba 25 mwaka 2015.

Hamadi alisema kamwe haki ya Wazanzibar haitapotea na kuahidi kuwa ndani ya miezi mitatu haki hiyo itakuwa imepatikana.

Wanachama wa CUF ya Lipumba ‘wawabadilikia’ waandishi

Wanachana wa CUF wanaomuunga mkono mwenyekiti anayetambuliwa na Msajili wa Vyama vya Siasa, Profesa Ibrahim Lipumba walijikuta wakizozana wao kwa wao muda mfupi baada ya mwenyekiti huyo kumaliza mkutano wake na waandishi wa habari.
Mwenyekiti huyo alikuwa akizungumza na waandishi wa habari leo (Jumamosi) kuhusu kamati mpya ya maadili ya nidhamu iliyozinduliwa katika ofisi za chama hicho Buguruni.
Baada ya kumaliza kutoa maelezo yake, mwenyekiti aliketi chini na kisha Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano ya Umma, Abdul Kambaya amesimama na kuwataka waandishi kutoka nje.
Lakini waandishi hao walisita kutii agizo hilo wakitaka kupata ufafanuzi wa baadhi ya hoja.
“ Ndugu waandishi tunaomba mtoke nje tuendelee na kikao chetu maswali mtauliza baada ya kamati kumaliza majukumu yake,” amesikika akisema Kambaya.
Hata hivyo, waandishi wameendelea kusisitiza kutaka kupata fursa ya kuuliza maswali kwa mwenyekiti ghafla kulisikika sauti toka nyuma ya ukumbi zikiwashinikiza waandishi hao watoke.
Mmoja wa mwanachama aliyekuwa amevalia fulana na kofia zenye nembo ya chama ndiye aliyeamsha zogo pale alipodai; “waondoke hawa waandishi kila siku wanakuja hapa hawaandiki habari zetu.”
Matamshi yake hayo yalidakwa na wengine waliokoleza mjadala hatua iliyofanya baadhi ya wanachama kusimama na kupinga hali hiyo.
“ Wewe ebu jiheshimu...acheni mambo yenu haya..ahaa hatutaki,” wamezozana wanachama hao.
Mzozo huo uliodumu kwa dakika tano umemalizika baada ya waandishi kutoka nje. Wakati wote wa malumbano hayo waandishi hawakuchangia neno lolote.
Mzozo huo ulihamia nje kwa dakika kadhaa huku baadhi ya wanachama wakivitaja na kuvituhumu vyombo vya habari kwa kutoandika habari zao.


Chanzo: Mwananchi

Msajili wa Vyama Azungumzia Sakata la Maalim Seif Kufungua Ofisi Mpya za CUF

Kutokana na Chama cha Wananchi (CUF) kufungua ofisi mpya za chama hicho katika eneo la Mtaa wa Idrisa Kata ya Mzimuni, Magomeni wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam, Msajili wa Vyama vya Siasa amesema anaamini chama hicho kinafanya mambo yake kwa kuzingatia sheria.

Jana  Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi, alisema hajapata taarifa yoyote ya chama hicho, kufungua ofisi mpya zaidi ya kuona katika vyombo vya habari.

“Ukiondoa taarifa za kwenye media sijapata taarifa yoyote kutoka CUF labda wawe wameleta leo (jana), lakini naamini chochote wanachofanya wanaelewa taratibu wataleta taarifa, “ alisema Jaji Mutungi.

Jaji Mutungi alisema sheria inawataka wanapofungua ofisi watoe taarifa ndani ya siku 14, ambazo hazijaisha hivyo anaamini wanajua hilo. 

Upande wa Katibu Mkuu, Maalim Seif Sharif Hamad wamefungua ofisi hizo, baada ya tukio la kuvamiwa katika Ofisi Kuu za Buguruni na kundi la Profesa Ibrahim Lipumba.

Jaji Mutungi alisema atakapopokea taarifa rasmi ataangalia kama taratibu zilifuatwa kwani ufunguaji wa ofisi mpya una taratibu zake. 

“Nikiletewa taarifa ndio nitajua kama walifata taratibu au la, ufunguaji wa ofisi una taratibu zake najua wanazijua pia, “ alisema Jaji Mutungi.

Alisema taarifa hiyo ataipata kutoka kwa mwenyekiti au msemaji wa chama, ambaye ni katibu mkuu ambao wanatambuliwa na ofisi ya msajili wa vyama vya siasa. 

Akizindua ofisi hiyo Juni 4 mwaka huu, Maalim Seif alisema ofisi hiyo imetolewa na wabunge 40 wa CUF.

Alisema uamuzi wa wabunge hao kumpatia ofisi ya kufanyia kazi hapo ni kitendo cha kiungwana na kiungwe mkono na wanachama wote. 

Alisema kwa miezi 10 sasa, wamekuwa wakishindwa kufanya kazi kwa upande wa Tanzania Bara, jambo ambalo limewaathiri hivyo kupatiwa ofisi kutamsaidia kutimiza majukumu bila hofu yoyote.

Katibu huyo alisema ana imani na mahakama kuwa itawapatia haki stahiki hivyo kuwataka wanachama kuendelea kuwa na subira.

CUF Ya Maalim Seif Yazindua Ofisi Magomeni Jijini Dar Es Salaam

IKIWA ni takribani miezi 10 sasa kwa Chama cha Wananchi (CUF), upande wa Katibu Mkuu, Maalim Seif Sharif Hamad kuvamiwa katika Ofisi Kuu za Buguruni na kundi la Profesa Ibrahim Lipumba chama hicho kimezindua ofisi mpya za chama hicho katika eneo la Mtaa wa Idrisa, Kata ya Mzimuni, wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam.

Aidha, Seif amesisitiza kuwa hatarajii kukutana na Profesa Lipumba kwa kile alichodai kuwa hatambuliki katika chama na hana sifa hizo kwa sasa.

Akizindua ofisi hiyo ambayo lengo kubwa ni kwa ajili ya wabunge 40 wa CUF, Seif alisema uamuzi wa wabunge hao kumpatia ofisi ya kufanyia kazi hapo ni cha kiungwana na kinahitajika kuungwa mkono na wanachama wote.

Alisema kwa muda wa miezi 10 sasa wamekuwa wakishindwa kufanya kazi hasa upande wa Tanzania Bara jambo ambalo limewaathiri sana hivyo kupatiwa ofisi kutamsaidia kutimiza majukumu yake vilivyo bila hofu yoyote.

Maalim Seif alisema kukosa ofisi kumewaathiri sana katika baadhi ya mambo hivyo anaamini kwa sasa akifikia Dar es Salaam anamahali pa kukutana na wakurugenzi wake.

“Nimekuwa ni kija hapa nakosa sehemu ya kukutana na wakurugenzi, viongozi mbalimbali wanachama ila hiki ambacho wabunge wamefanya ni cha kuungwa mkono sijawahi kufanya kazi na wabunge wanao kipenda chama kama kipindi hiki,” alisema.

Katibu huyo alisema atahakikisha kuwa anaanza kazi haraka iwezekanavyo kwa kukutana na wakurugenzi wake ili waweze kutekeleza majukumu ya chama.

“Hakuna shaka kuwa huu unaoitwa mgogoro umeturudisha nyuma sana hivyo naamini wakati wa kufanyakazi umerejea na hawa wabaya wetu hawata ambulia kitu kwani CUF ni chama imara hakitikisiki,” alisema.

Maalim Seif alisema jitihada zinazofanywa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kukimaliza chama ni kubwa lakini hawataweza kufikia lengo hilo kutokana na misingi ya chama hicho.

Alisema kwa sasaa atafanya kazi katika ofisi hiyo ambayo amepewa na wabunge hadi hapo muafaka wa ofisi kuu Buguruni utakapopatikana huku akisisitiza kuwa haki haipotei ila inachelewa.

Katibu huyo alisema anaimani na mahakama kuwa ita wapatia haki stahiki hivyo kuwataka wanachama kuendelea kuwa na subira.

Aidha, alisema kupitia mgogoro huo hadi sasa Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini inashikilia zaidi ya sh. bilioni 1.2 ambazo ni ruzuku ya chamahicho.

Maalim Seif alisema fedha hizo ni pamoja na zile ambazo ofisi ya msajili ilimpatia Lipumba hivyo waamini mgogoro ukiisha wata pata haki yao.

Kwa upande mwingine Katibu huyo alisema hana mpango wa kukutana naLipumba kuhusu mgogoro unaondelea ndani ya chama hicho kwa kile alichodai kuwa si kiongozi wala mwanachama wa chama hicho.

Alisema CUF haimtambui Lipumba kwa sifa yoyote tofauti na kumfukuza uanachama hivyo yeye hawezi kukukutana na mtu kamahuyo.

Maalim Seif alisema pamoja na kuwa hawamtambui Lipumba kama kiongozi au mwanachama ila akiomba msamaha wapo tayari kumsamehe.

Akizungumza baada ya kuzinduliwa ofisi hizo Mbunge wa Viti Maalum na Kiongozi wa Wabunge wa CUF bungeni, Riziki Ngwali alisema wamelazimika kufungua ofisi nyingine ili wapate mahali pa kukutana wakiwa nje ya Bunge.

Ngwali alisema kupitia ofisi hiyo wataweza kujadiliana mambo mbalimbali yanayo wahusu wabunge na wananchi na kuja na ufumbuzi.

Kwa upande wake Mbunge wa Temeke CUF, Abdallah Mtolea alisema katika ofisi hiyo wanatarajia kuajiri wataalam mbalimbali ambao watasaidia kufanya tafiti na kupitia tarifa mbalimbali za Bunge ili kuwarahisishia katika uchangiaji bungeni.

Alisema katika ofisi hizo wameingia mkataba wa kulipa sh. milioni 18 kwa mwaka ambazo zitatolewa na wabunge wenyewe kwa maslahi ya chama chao.

Profesa Lipumba: Akanusha Kutumiwa na CCM Kuivuruga CUF

Mwenyekiti wa CUF anayetambulika na msajili wa Vyama vya Siasa Prof. Ibrahim Lipumba leo May 4, 2017 kupitia kipindi cha Clouds 360 kinachorushwa na Clouds TV amesema hakuwa na namba ya Edward Lowassa wakati anajiunga UKAWA.

Aidha, kwenye mahojiano hayo Prof. Lipumba amesema kuwa amekuwa mstari wa mbele kuhakikisha anaiongoza CUF katika kudai haki za wananchi tofauti na Maalim Seif ambaye mara kadhaa ikitokea suala hilo haonekani akisema:

“Mwaka 2000 baada ya Uchaguzi Mkuu tuliingia kwenye maandamano Zanzibar, lakini Maalim Seif alikwenda Uingereza nilikuwa mstari wa mbele.

Prof. Lipumba amesema pia kuwa Maalim Seif amekuwa akidai kila anapokosana na mtu kisiasa kuwa mtu huyo anatumiwa na CCM akitolea mfano wa Ahmad Rashid, akisema:

“Ni kawaida ya Maalim Seif, akikosana na mtu kisiasa anasema anatumiwa na CCM. Rejea mgogoro na Ahmad Rashid".

Akizungumzia kuhusu kumpokea na kumtambulisha kwa viongozi wa UKAWA aliyekuwa Waziri Mkuu wa zamani wa Tanzania Edward Lowassa wakati anatoka CCM, Prof. Lipumba alisema:

“Mbatia ndiye aliyeniunganisha na Lowassa. Sikuwa na namba zake, na wakati anakuja, nilisema wazi suala la rushwa ni mfumo siyo mtu.

“Mzigo mzito anapewa Mnyamwezi, lakini huu wa kumnadi Edward Lowassa ulinizidi uzito, nisingeweza kuubeba."

Wakai huo huo Prof. Lipumba amebainisha kuwa hakuwa na nia ya kurejea katika nafasi yake ya Uenyekiti wa CUF baada ya kujiuzulu, lakini aliombwa na wanachama wa chama hicho.

“Sikuwa na nia ya kurudi kuwa Mwenyekiti CUF ila wanachama waliniomba nirudi baada ya uchaguzi kumalizika na hali kutulia”

Mtatiro: CUF haina walinzi wa chama wenye bastola

Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi, The Civic United Front (CUF) Julius Mtatiro amefunguka na kusema chama cha CUF hakina walinzi wa chama wenye bastola wala hakina walinzi wanaozunguka mitaani kufanya doria.

Julius Mtatiro ametoa ufafanuzi huo leo baada ya Mkurugenzi wa Habari CUF Taifa, ambaye anamuunga mkono Profes Ibrahim Lipumba  ndugu Abdul Kambaya kukiri kuwa ni kweli wao walituma vijana kwenda kwenye Kata ya Mabibo kufanya doria.

"Siku ambapo kikao kinafanyika Vinna Hotel, vijana wetu pia walikuwa kwenye doria, tulipozungumza na vyombo vya habari tulikiri na tunaendelea kukiri hatuna sababu ya kukataa kwamba tulituma vijana wetu na walikwenda kwenye doria" alisema Kambaya

Kufuatia taarifa hiyo ya Kambaya Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi, The Civic United Front (CUF) Julius Mtatiro amefunguka na kusema wao kama CUF hawana walinzi wa chama wenye bastola hivyo amelitaka jeshi la polisi limtumie huyu Kambaya kueleza kijana aliyekuwa na bastola yuko wapi na walikodishwa kutoka wapi.

"Leo amekiri kuwa lile Zombi lililopigwa na wananchi, Mabibo, eti lilitumwa na genge la Mungiki/Lipumba ili kufanya doria kwenye kata ya Mabibo. Yani eti Lipumba ana jeshi lake linalofanya doria na kupiga watu mitaani. Sasa Polisi wasitafute mchawi, huyu Abdul Kambaya aeleze lile zombi lililokuwa na bastola liko wapi na waliikodisha kutoka wapi? Alihoji Mtatiro

Mbali na hilo Mtatiro alizidi kusisitiza kuwa wao hawana walinzi wa chama

"Halafu, eti huyo msemaji wa Lipumba anasema "Zombi" hilo lililokamatwa ni "mlinzi wa chama". Napenda ifahamike kuwa CUF haina walinzi wa chama wenye bastola, na pia hakuna chama cha siasa chenye walinzi wanaozunguka mitaani kufanya doria, wameajiriwa na serikali ipi? Alihoji Mtatiro

PROFESA LIPUMBA ATINGA MAHAKAMANI

Mgororo wa ruzuku ndani ya Chama cha Wananchi (CUF) unazidi kupamba moto baada ya mwenyekiti wa chama hicho anayetambuliwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, Profesa Ibrahim Lipumba kwenda kuitetea mahakamani.
 
Profesa Lipumba na Mkurugenzi wa Fedha na Uchumi wa chama hicho, Thomas Malima wamefungua maombi Mahakama Kuu wakiomba waunganishwe kwenye kesi iliyofunguliwa na Bodi ya Wadhamini wa CUF, walio upande wa Katibu Mkuu, Maalim Seif Sharif Hamad.
 
Katika kesi ya msingi ya ruzuku namba 21 ya mwaka 2017, wadai wanaiomba Mahakama imzuie msajili kutoa ruzuku kwa CUF na imuamuru Sh360 milioni alizozitoa kwa kina Profesa Lipumba zirejeshwe kwenye akaunti rasmi ya chama. 

Wadaiwa katika kesi hiyo ni Msajili wa Vyama vya Siasa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, lakini Profesa Lipumba na Malima wamewasilisha maombi mahakamani nao waunganishwe kwenye kesi hiyo upande wa wadaiwa.
 
Maombi hayo yalitajwa jana na Malima aliieleza mahakama wakiwa viongozi halali wa chama hicho, wanaomba kujumuishwa kwenye shauri hilo kwa kuwa wana masilahi na shauri hilo.
 
Wakili wa CUF upande wa Katibu Mkuu, Juma Nassoro na Wakili wa Serikali, Hang Chang’a waliieleza mahakama kuwa bado hawajapewa hati za maombi hayo.
 
Jaji Wilfred Dyansobela aliamuru waombaji hao (kina Lipumba) kuwapatia nyaraka hizo na amepanga kusikiliza maombi hayo Juni 6, siku ambayo kesi ya msingi itatajwa.

Maalim Seif: Hakuna CUF ya Maalim wala CUF ya Lipumba

Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, amesema chama hicho kitaendelea kufanya mambo kiungwana kwa kuwa Tanzania ni nchi ya amani na kuwa hakuna CUF ya Maalim Seif wala CUF ya Lipumba.
Akizungumza na waandishi wa habari leo, Maalim Seif alisema CUF inatimiza wajibu wa kutunza amani na iwapo kingetaka kuleta machafuko basi kingefanya hivyo tangu zamani.
“CUF ni moja. Ni kweli sisi tumekuwa wapole na waungwana, sisi si tunaambiwa hii nchi ya amani, sisi tunatimiza wajibu wetu wa kutunza amani. Hakuna chama kinachotunza amani kama CUF” alijibu mara baada ya kuulizwa na waandishi wa habari.
“The struggle we continue, mtatia ndani Maalim Seif, mtatia ndani Mtatiro lakini there are so many Maalim Seif’s. Kuna Maalim wengine ni vichaa,” alisema
Wakati huhuo Maalim Seif aionyooshea kidole Rita
Katibu Mkuu wa CUF , Maalim Seif Sharif Hamad amezungumza na waandishi wa habari leo na kusema Wakala wa Usajili wa vizazi na vifo, (RITA) utakuwa umekiuka sheria iwapo utaisajili na kuitambua bodi ya wadhamini iliyoundwa na Mwenyekiti wa CUF, Ibrahim Lipumba.
“Sisi tumekuwa wapole sana, tunaona katiba inavunjwa, lakini niseme kwamba, kama Rita wataisajili bodi ya Lipumba, watakuwa wamekiuka sheria yao wenyewe. Bodi ipo na imesajiliwa 1993 na tunacho cheti cha kusajiliwa” alisema
Alisema ni utaratibu kuwa kila kipindi fulani marekebisho hufanywa lakini bodi haifi.
Alisema bodi ya CUF ipo na kama ofisa Mtendaji mkuu wa Rita ataisajili basi ajue anavunja sheria.

MAALIM SEIF: LIPUMBA HANA UWEZO WA KUNIVUA UKATIBU MKUU CUF

Sarakasi za kisiasa zinaendelea kutawala ndani ya chama cha CUF baada ya Katibu Mkuu wake, Maalim Seif Sharif Hamad, kudai kuwa Profesa Ibrahim Lipumba anatumiwa kukihujumu chama hicho.

Maalim Seif alimtuhumu Profesa Lipumba ambaye ni Mwenyekiti wa CUF, anayetambuliwa na ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini kuwa anakihujumu chama ili kishindwe kudai haki waliyoipata katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25 mwaka juzi.

Aliyasema hayo jana katika kijiji cha Tumbatu Mkoa wa Kaskazini Unguja alipozungumza na wanachama wa chama hicho, ikiwa ni ziara maalumu ya uimarishaji wa chama katika mikoa yote ya Kisiwa cha Unguja.

Maalim Seif alisema pamoja na Profesa Lipumba kupata nguvu kutoka vyombo vya dola na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa katika kukihujumu chama hicho, lakini hawataweza kufikia malengo hayo.

Alisema taasisi hizo kwa pamoja zimekuwa zikimuunga mkono Lipumba kwa kumpa kila nguvu anayohitaji ili kuona anafanikisha malengo ya CCM ya kuitawala nchi bila ya kuwepo kwa chama kikuu pinzani, ila nguvu zao hizo zitagonga mwamba.

“Nashangaa sana kuona Lipumba amekubali kutumika na CCM kwa kukihujumu chama kwa masilahi binafsi, lakini nataka muelewe wananchi kuwa pamoja na nguvu zao zote hizo katu hawataweza kuwakatisha tamaa Wazanzibari ya kudai haki yao waliyoipata katika uchaguzi uliopita,” alisema.

Alishangazwa kuona Ofisi ya Msajili kwa kushirikiana na vyombo vya dola badala ya kufuata Katiba na sheria za nchi, wao wamekuwa wakikihujumu chama hicho.

“Pamoja na hujuma hizi zinazofanywa na Lipumba katika chama chetu, lakini nashangaa Rais (John) Magufuli anatumbua watendaji wabovu, lakini humu mrajisi (Msajili) wa Vyama vya Siasa anamuachia,” alisema.

Kuhusu kuondolewa kwenye nafasi yake, Maalim Seif alisema kwa mujibu wa katiba ya CUF, Lipumba hana uwezo wa kumvua nyadhifa hiyo hata kama angekuwa ni mwenyekiti halali.

Alisema kwa mujibu wa katiba yao ili Katibu avuliwe wadhifa wake lazima mkutano mkuu uhudhuriwe na zaidi ya nusu ya idadi wajumbe.

Alisema kikao kilichofanyika chini ya Profesa Lipumba kilihudhuriwa na wajumbe wasiokuwa na ujumbe kihalali, ambao walipandikizwa kuonesha kama kikao hicho kilikuwa halali.

“Ikiwa mimi nimefukuzwa chama kutokana na madai kuwa sihudhurii vikao vinavyofanywa na ofisi za chama hicho jijini Dar es Salaam, mbona yeye Lipumba tangu mwaka 2015 hawajawahi kuja ofisi kuu ya chama ambayo ni mtendeni hadi leo, kwa hiyo naye alitakiwa kufukuzwa,” alihoji.

Maalim Seif alisema kuwa kinachosikitisha ni kuona Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa nayo kuidhinisha kuwa wamekubaliana na mageuzi hayo yaliyofanywa na Lipumba kwa kushirikiana na wajumbe wake.

“Ninachokifahamu mimi ndani ya katiba yetu inasema kuwa ili uamuzi wa kuvuliwa nafasi ya uongozi ni lazima anayedaiwa kufanya kosa aitwe na uongozi kujieleza, lakini mimi sijaitwa kujieleza,” alihoji Maalim Seif.

Akizungumzia madai ya kushinda Uchaguzi Mkuu uliopita, Maalim Seif alisema waliwataka wananchi wa Zanzibar kutokata tamaa na haki yao, huku akidai hivi karibuni dola ya Zanzibar itakuwa chini ya CUF.

Naibu Katibu Mkuu wa CUF Zanzibar, Nassor Ahmed Mazrui, alisema uongozi wa CUF unasikitika kuona vyombo vya dola vikiingilia mamlaka ya chama hicho na kusahau wajibu wao.

Alisema kuwa wajibu wa vyombo hivyo ni kusimamia amani ya wanachama na viongozi wake, lakini ni jambo la kushangaza kwa viongozi wa vyombo hivyo kuwa ni miongoni mwa wanaongoza kuonesha chuki dhidi ya CUF.

Alisema pamoja na hujuma hizo, lakini viongozi wakuu wa chama hicho chini ya Maalim Seif, hawatosita kudai haki yao hadi kieleweke.

Akijibu tuhuma hizo, Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho bara na anayemuunga mkono Profesa Lipumba, Magdalena Sakaya alimtuhumu Maalim Seif kuwa ndiye anakula njama za kukidhoofisha chama.

Alisema Seif amekataza ruzuku zisifike kwenye wilaya, hakuna mikutano na hakuna hata pikipiki huku wenzao Chadema waliokuja juzi wamekuwa chama kikuu cha upinzani kutokana na kuwa wamoja.

“Malalamiko anayotoa ajikite kwenye katiba, aichambue kifungu kwa kifungu atabaini anakosea wapi.

“Hii ni taasisi  ya chama, siyo kampuni ya mtu, lazima tufuate katiba tuliyojiwekea ambayo ipo wazi inatoa maelekezo ya kila kitu, anayekengeuka anafanya makusudi na sisi hatuwezi kukaa kimya bila kuchukua hatua ikiwa ni pamoja na kuteua watakaofanya kazi alizotakiwa kufanya yeye,” alisema Sakaya.

Alieleza kuwa badala ya kujenga chama, ameamua kukidhoofisha na anatumiwa kufanya hivyo akijificha kwenye mwamvuli wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).

“Amekuwa bwana kesi, kila kukicha anafungua mpya, mimi nina kesi, Lipumba ana kesi, Msajili wa Vyama ana kesi, mwanasheria ana kesi, akae kimya asubiri ziishe, ”alisema Naibu katibu mkuu huyo.

MAHAKAMA KUU YAMWAMURU MSAJILI WA VYAMA VYA SIASA KUTOTOA RUZUKU KWA PROF. LIPUMBA NA KUNDI LAKE MPAKA SHAURI LITAKAPOAMULIWA

Mahakama Kuu imemuamuru Msajili wa Vyama vya Siasa nchini kutotoa ruzuku kwa Prof. Ibrahim Lipumba wa Chama cha Wananchi, CUF, na kundi lake.

Zuio hilo ni mpaka shauri dhidi ya Msajili na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuhusu kutoa fedha za ruzuku shilingi milioni 369 kwa njia za wizi na udanganyifu litakaposikilizwa na kutolewa maamuzi.

Uamuzi huo umefikiwa na Jaji Dyansobela baada ya kukubaliana na hoja zilizowasilishwa kwa hati ya dharura.

Jopo la Mawakili wa CUF, liliiomba Mahakama Kuu kutoa amri hiyo kwa kuwa fedha zilizotolewa awali shilingi milioni 369 hazijulikani zimetumika vipi, na hazikuwa katika mikono salama wala hakuna udhibiti wowote wa chama kuhusu fedha hizo ikizingatiwa kwamba, Prof. Lipumba alishavuliwa uanachama.

Mawakili hao akiwemo Juma Nassor , wamesisitiza kwamba, mazingira yaliyopo ni vyema na busara kwa fedha za umma zilizopaswa kutolewa kama ruzuku kwa chama cha CUF kwa sasa ziendelee kubakia serikalini.

Aidha, wameiomba Mahakama Kuu kwamba amri hiyo pia ifungamane na kesi ya msingi namba 23/2016 ya kuhoji maamuzi ya msajili kumtambua Prof Lipumba kwa nafasi ya uenyekiti iliyopo mbele ya Jaji Kihijo ambayo kwa sasa imekatiwa rufani ya kufanyiwa marejeo mbele ya Mahakama ya Rufani Tanzania.

Lipumba Amtumbua Maalim Seif

Mgogoro wa Uongozi wa Chama cha Wananchi CUF umeendelea kufukuta ambapo Mwenyekiti wa Chama hicho anayetambuliwa na Ofisi ya Msajili Vyama vya Siasa nchini Prof. Ibrahim Lipumba amemteua Naibu Katibu Mkuu Bara, Magdalena Sakaya kukaimu nafasi ya Katibu Mkuu Maalim Seif Sharif Hamad baada ya Maalim Seif kukaidi wito wa Mwenyekiti wake kwenda Ofisi kuu Buguruni kwa zaidi ya mara nne

Prof. Lipumba akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es salaam pamoja na wafuasi wa chama hicho, amesema Maalim Seif amekaidi wito wa kwenda Makao Makuu Buguruni tangu Septemba 23 mwaka jana kwa ajili ya kusimamia mkutano wa kamati ya Utendaji ambao ulitakiwa kujadili mambo kadhaa ya chama hicho

Aidha, Prof. Lipumba amewavua madaraka wakurugenzi kutoka Zanzibar akiwemo Salim Bimani aliyekuwa Mkurugenzi wa Habari na Uenezi, Omar Ali Salehe Mkurugenzi Mipango na Uchaguzi, Abdalah Bakar Khamis Mkurugenzi wa Fedha na Uchumi, Pavu Juma Abdallah - Haki za Binadamu, Mahima Ali Mahima Katibu Mtendaji JUVICUF pamoja na Yusuph Salim Naibu Mkurugenzi Ulinzi na Usalama CUF wote kutoka Zanzibar.

Chama cha Wananchi CUF kimekumbwa na Mgogoro wa uongozi tangu Prof. Lipumba alipotangaza kujiuzulu uongozi wa chama hicho kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, ambapo baadaye alitangaza kurudi na kufanyika mkutano mkuu ambao ulivurugika na kusababisha mpasuko kati ya CUF bara na CUF Zanzibar.

MEYA ILALA AFUNGUA RASMI DARAJA LA BONYOKWA-KINYEREZI

Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala, Charles Kuyeko, akihutubia wananchi baada ya kufungua rasmi daraja linalounganisha Kata ya Bonyokwa na Kata ya Kinyerezi katika Manispaa ya Ilala, jijini Dar es salaam.
Mbunge wa Viti Maalumu, Anatropia Theonesti (Chadema) akihutubia wakati wa ufunguzi wa daraja hilo
Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala, Charles Kuyeko, akikiwa amekata utepe ikiwa ni ishara ya kufungua rasmi daraja linalounganisha Kata ya Bonyokwa na Kata ya Kinyerezi katika Manispaa ya Ilala, jijini Dar es salaam.

Mwandishi wetu
MSTAHIKI MEYA wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala, Charles Kuyeko jana alifungua rasmi daraja linalounganisha Kata ya Bonyokwa na Kata ya Kinyerezi katika Manispaa ya Ilala, jijini Dar es salaam.

Awali akizungumza katika hafla hiyo Mhandisi wa Manispaa ya Ilala ndugu Benjamin Maziku alisema  daraja hili limejengwa kwa takribani mwaka mmoja na kugharimu Tsh.million  478 hadi kukamilika kwake leo hii. Ujenzi wa daraja hili umesua sua kwa siku nyingi kutokana na sababu mbali mbali lakini kutokana na usimamizi imara wa Mstahiki Meya wa Ilala Mhe. Charles Kuyeko sasa historia imebadilika.

Meya Kuyeko akizungumza na umati wa wananchi waliokusanyika kushuhudia ufunguzi huo amewasitiza kulilinda na kulitunza vyema daraja hilo kwani limejengwa kwa kodi zao.

Awali, Meya akitoa historia ya daraja hilo amesema kuwa, waliokuwa wanatakiwa kujenga daraja hilo ni wakala wa Barabara Tanzania (Tanroad) lakini kutokana na kusuasua kwao, Mimi (Meya)  niamua kuingilia kati kwa Manispaa kutenga Fedha kujenga daraja la muda ili kuwasaidia wananchi wa Bonyokwa kuondokana na atha ya kuwa Kisiwa hususani wakati wa Mvua.

Kuyeko ambaye pia ni Diwani wa kata ya bonyokwa amewaambia wananchi hao waliofurika kwenye uzifunguzi huo kuwa huo ni mwanzo tu wa utekelezaji wa ahadi zake katika kutatua kero za wananchi na wapiga kura wake. "Nawahakikishia kuwa hamtajutia kunipa kura zenu kwani daraja hili imekuwa kero ya miaka nenda rudi lakini Mimi nimeimaliza kwa muda mfupi kwa kushirikiana na watendaji wangu hivyo mtarajie mengi kabla mwaka huu kuisha hata daladala zitakuwa zinafika hadi kisiwani".

Mbali na hayo,Meya amewaahidi wananchi hao muda mfupi ujao atatatua kero ya maji na barabara kama ambavyo aliahidi kutekeleza wakati wa kampeni.

Ufunguzi huo ulihudhuliwa na viongozi mbali mbali wa kiserikali na kisiasa akiwemo mbunge wa Viti Maalum Mhe. Anatropia Theonest, madiwani wa kata mbalimbali na viongozi wa vyama vya siasa.

Akitoa salam kwa niaba ya viongozi wa vyama vya siasa, Dk.Makongoro Milton Mahanga mbunge wa zamani jimbo la Segerea ambaye kwa sasa ni, Mwenyekiti wa CHADEMA Mkoa wa Ilala alisema, "Tangu niwe kiongozi sijawahi kuona kiongozi mahiri kama Meya Kuyeko. 

Ameweza kuwaunganisha viongozi wa Manispaa yake na kuwa kitu kimoja, na hadi sasa ameshafanya vitu vingi ambavyo awali vilishindikana nakupongeza sana Meya Kuyeko.

Dkt. Mahanga  aliwasisitiza wananchi kuwaamini viongozi wanaotokana na UKAWA kwani ni wazuri jifunzeni kwa Kuyeko mambo makubwa anayoyafanya. Kwa niaba ya Chadema nampongeza sana Meya Kuyeko kwa kukiwakirisha vyema  chama kwa wananchi.

Naye Mwenyekiti wa Chadema Jimbo la Segerea ndugu Gango Kidera aliwataka wananchi wa Bonyokwa  waendelee kumwamini na kumuunga mkono Meya Kuyeko, Baraza lake la Madiwani kwani amekuwa mfano bora kwa kutekeleza ahadi zake zinazotokana na ilani na Sera za Chadema/UKAWA. 

Chadema imemtuma Kuyeko kuwatumikia wananchi wa Bonyokwa na Manispaa nzima ya Ilala kwa kuhakikisha anatatua kero zao kwa spidi ya mwendokasi na leo tumeona anatenda kwa maslahi ya wananchi. Nakupongeza sana Meya Kuyeko, alisema Kidera

Viongozi wengine waliozungumza katika ufunguzi huo ni Mbunge wa Viti Maalum Mhe. Anatropia Theonest ambaye aliwapongeza wananchi wa Bonyokwa kwa kumchagua Kuyeko, wananchi wa Bonyokwa mlifanya maamuzi sahihi kuchagua Chadema kwa sababu bila Chadema Meya Kuyeko tusingempata. 

Anatropia pia alimpongeza Meya Kuyeko kwa kuendelea kutatua kero za wapiga kura wa Bonyokwa siku hadi siku na Ilala kwa ujumla. UKAWA kwa Manispaa ya Ilala chini ya Meya Kuyeko imeleta matumaini makubwa kwani wakazi wa Manispaa wapatao 1,415,443 walikuwa wamekata tamaa kabisa kwani viongozi waliopita walishindwa kutatua kero za wananchi, hivyo UKAWA chini ya Meya Kuyeko ni mfariji mkuu wa wananchi, alisema Anatropia.

Diwani wa Buguruni Mhe. Penza wa CUF akizungumza kwa niaba ya Madiwani wa Ilala alisema ilani ya UKAWA imeweka vipaumbele kwenye Barabara, maji, afya, elimu, na masoko na mitaji hivi vyote vinafanyika.

Meya Kuyeko aliwashukuru wananchi kwa kuendelea kumwamini na kumpa ushirikiano wa karibu hali ambayo inampa ari ya kuwatumikia kwa nguvu zake zote. Pia amekishukuru chama chake Chadema, viongozi, Madiwani na watendaji wote wa Manispaa ya Ilala wakiongozwa na Mkurugenzi kwa kumpa ushirikiano wa hali na Mali katika kuwatumikia wananchi.