HABARI

Theme images by kelvinjay. Powered by Blogger.

MATUKIO

MICHEZO

SIASA

Jeshi la Polisi Lasema Linawashikilia Watu 3 Kwa Kuvamia Mkutano wa CUF na Kuwapiga Watu

Saa  tatu baada ya viongozi wa CUF kukutana na Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Simon Sirro, kuhoji sababu za kutokamatwa watu waliofanya vurugu kwenye mkutano wa waandishi wa habari na viongozi wa chama hicho wa wilaya ya Kinondoni, Jeshi la Polisi limetangaza kushikilia watu watatu.

Wakiongozwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi ya Chama hicho Julius Mtatiro, viongozi hao waliwaeleza wanahabari kuwa ni ajabu kuona  Polisi haijachukua hatua huku ikijulikana wazi kuwa watu hao walijeruhi wanahabari na viongozi wa chama hicho katika tukio ambalo liliripotiwa na vyombo vya habari.

Viongozi hao walikutana na Sirro jana saa 5 asubuhi na kuzungumza kwa takribani saa moja, na kisha saa 8 mchana Kamanda huyo alizungumza na waandishi wa habari na kueleza kukamatwa kwa watu hao, wakituhumiwa kuhusika katika tukio hilo.

Jumamosi iliyopita takribani watu watano wakiwa kwenye gari lenye nembo na bendera za CUF, walivamia mkutano huo uliokuwa ukifanyika kwenye hoteli ya Vinna, Mabibo wilayani Kinondoni na kufanya vurugu.

Miongoni mwa watu hao, mmoja aliyekuwa amejifunika uso kininja alichomoa bastola na kutishia huku mwingine akishindwa kuondoka baada ya kuachwa na wenzake, jambo lililosababisha wananchi wamzingire na kumshushia kipigo.

Katika ufafanuzi wake, Mtatiro alisema tukio hilo ni la 13 dhidi ya upande unaomwunga mkono Katibu Mkuu wa Chama hicho, Maalim Seif Sharif Hamad lakini vyombo vya Dola viko kimya.

“Baada ya tukio la juzi (Jumamosi) tulikaa kimya ili kuona kama polisi watasema chochote ila imekuwa tofauti. Wako kimya tu,” alisema Mtatiro.

Akieleza kilichowapeleka kituoni hapo, alisema: “Tulitaka kujua yule mvamizi aliyekuwa na bastola mpaka sasa yuko wapi. Mvamizi mmoja tunajua alikamatwa na wananchi, akapigwa kidogo na kuokolewa. Tulitaka kujua alitoa maelezo gani.”

Alisema baada ya tukio hilo, Mkuu wa Upelelezi aliwapigia simu viongozi waliovamiwa akiomba waende kituo cha Polisi Magomeni  wakapatanishwe.

“Tulishangazwa na taarifa hiyo, kwa watu waliovamiwa kwenda kupatanishwa. Tulijihoji kama Jeshi la Polisi linaweza kupatanisha watu wenye makosa ya jinai, kwani mtu wa makosa hayo upelelezi unapokamilika hupelekwa mahakamani,” alisema Mtatiro.

Alisema sababu nyingine ya kwenda kituoni hapo ni kutaka kufahamu kama watu wanaofanya matukio hayo wako juu ya sheria.

“Tulimwonya Kamanda Sirro kwamba sisi (upande wa Maalim) tuna nguvu kuliko Lipumba na kuiomba Polisi kutekeleza majukumu yake kwa kuchukua hatua dhidi ya wavamizi hao,” alisema.

Katika mkutano wake na wanahabari, Sirro alisema Polisi inashikilia watu watatu wakituhumiwa kufanya vurugu kwenye mkutano huo.

“Tulipata taarifa ya kuvamiwa kwa mkutano wa wanachama wa CUF na watu wasiofahamika wakiwa na silaha. Baada ya taarifa hizo kupokewa askari walifuatilia na kukamata watu watatu,” alisema Sirro.

Alisema watuhumiwa hao wanaendelea kuhojiwa na upelelezi ukikamilika hatua za kisheria zitafuatwa.

Alisema hakuna mtu aliye juu ya sheria na kusisitiza kuwa waliohusika watasakwa kokote watakokuwa.

KAMANDA SIRRO AWATAKA WANANCHI KUTOJICHUKULIA SHERIA MIKONONI

Kamanda wa Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam, Kamishna Simon Sirro amewataka wananchi kuacha kujichukulia sheria mikononi badala yake waviachie vyombo husika ili viweze kufanya kazi yake.

Ameyasema hayo Jijini Dar es salaam wakati akizungumza na waandishi wa habari. Amesema kuwa wananchi kujichukulia sheria mikononi pindi wawakamatapo watuhumiwa ni kinyume cha sheria hivyo wanatakiwa kuacha mara moja tabia hiyo.

“Ni vyema wananchi wakaacha  tabia ya kujichukulia sheria mikononi ili vyombo usika vifanye kazi yake,”amesema Sirro.

Aidha, amesema kuwa wananchi kuwauwa watuhumiwa ni kosa kisheria kwani watakao bainika kufanya hivyo sheria kali dhidi yao zitachukuliwa.

Hata hivyo, ameongeza kuwa ni bora wananchi waache tabia hiyo ya kujichukulia sheria mikononi kwani vyombo husika kama Polisi na Mahakama vipo kwa ajili ya shughuli hiyo.

WAZIRI NCHEMBA AWASILI ENEO YALIPOTOKEA MAUAJI YA POLISI WANANE

Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba amewasili eneo yalipotokea mauaji ya askari wanane katika kijiji cha Jaribu, Wilayani Kibiti.
Waziri Nchemba ameambatana na naibu wa wizara hiyo, Mhandisi Hamad Masauni.
Nchemba atatembelea kambi za askari polisi wa kanda ya Pwani na katika kata ya Bungu wilayani Kibiti.

WATU WATATU WANAODHANIWA KUWA NI MAJAMBAZI WAULIWA KWA KUPIGWA RISASI NA POLISI

Watu watatu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi  wameuwa kwa kupigwa risasi na polisi baada ya kukaidi amri ya kutakiwa kusimama eneo la kizuizi cha Mwembe Muhoro wilayani Rufiji, mkoani Pwani.

Watu hao walikuwa wamepakiana kwenye pikipiki moja huku wakiwa wamevaa hijabu.

Akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na tukio hilo, kamanda wa Polisi mkoani Pwani ,Onesmo Lyanga alisema pikipiki nyingine mbili zilifanikiwa kukimbia.

Akielezea juu ya tukio hilo alifafanua,lilitokea Aprili 2 mwaka huu majira ya mchana ,Muhoro ,Rufiji barabara kuu ya Dar es Salaam Lindi.

“Siku ya tukio askari walipata taarifa kuwa kulikuwa na pikipiki tatu zikitokea Kibiti kwenda mikoa ya Kusini zikiwa zimebeba watu watatu kila moja “

“Miongoni mwa pikipiki hizo kati yake mbili wamebebwa watu waliovaa hijabu,” alisema Lyanga.

Alisema askari wa barabarani walipewa taarifa katika kizuizi cha Mparange na kuwasimamisha ili wawahoji lakini walikataa na kupita ambapo waliwajulisha wenzao kwenye kizuizi cha Ikwiriri lakini walikaidi kusimama.

“Baada ya hapo walifika kizuizi cha Ikwiriri lakini bado walikaidi kusimama na kuendelea kukimbia ndipo walipofika kituo cha Muhoro “

“Hata hivyo hawakusimama na askari waliokuwa doria wakiwa kwenye gari waliwafuatilia na wakavuka daraja la Mkapa na waliwapa onyo kwa kupiga risasi hewani,” alisema Lyanga.

Aidha alibainisha baada ya hapo watu hao waliruka kwenye pikipiki na kuanza kukimbilia msituni na ndipo askari walipowapiga risasi za miguu na kiunoni na kufanikiwa kuwakamata.

“Majeruhi hao walijulikana ni wanaume hata hivyo majina yao hayakuweza kufahamika na walikuwa kwenye pikipiki yenye namba za usajili MC 272 BLW aina ya Boxer yenye rangi nyeusi”

“Watu hao wanaodhaniwa kuwa ni majambazi  kwa mwonekano wao walijaribu kuwawahisha hospitali ya Misheni ya Mchukwi,” alisema Lyanga.

Lyanga alisema walipofikishwa hospitali daktari alithibitisha kuwa watu hao wamefariki dunia .

Hata hivyo majina yao hayakuweza kufahamika huku pikipiki nyingine mbili zilitoroka na kuelekea mkoa wa Lindi na taarifa zimetolewa polisi ili wawakamate.

Aliwataka wananchi kuwa watulivu pale wanaposimamishwa na askari polisi badala ya kujaribu kutoroka na kwa sasa jeshi hilo limeimarisha doria katika kukabiliana na uhalifu.

WAZIRI MWIGULU AWAASA ASKARI KUTOWABAMBIKIZIA WATU KESI

Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi Mhe Mwigulu Lameck Nchemba akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao cha kazi cha Mwaka 2017 cha Maafisa waandamizi wa Polisi na Makamanda wa Mikoa/Vikosi.
Mzee John Samwel Malecela akizungumza wakati wa kikao cha kazi cha Mwaka 2017 cha Maafisa waandamizi wa Polisi na Makamanda wa Mikoa/Vikosi.
Kamanda wa Jeshi la Polisi nchini Ernest Mangu Akisisitiza jambo wakati wa kikao cha kazi cha Mwaka 2017 cha Maafisa waandamizi wa Polisi na Makamanda wa Mikoa/Vikosi


Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe Jordan Lugimbana akitoa salamu za Mkoa wa Dodoma wakati wa kikao cha kazi cha Mwaka 2017 cha Maafisa waandamizi wa Polisi na Makamanda wa Mikoa/Vikosi
 Maafisa waandamizi wa Polisi na Makamanda wa Mikoa/Vikosi
Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi Mhe Mwigulu Lameck Nchemba akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao cha kazi cha Mwaka 2017 cha Maafisa waandamizi wa Polisi na Makamanda wa Mikoa/Vikosi.
SACP Ramadhani Mungi Msimamizi wa bandari Tanzania na Kamanda wa polisi mkoa wa Lindi Renata Mzinga wakifatilia kwa makini kikao cha kazi cha Mwaka 2017 cha Maafisa waandamizi wa Polisi na Makamanda wa Mikoa/Vikosi.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi Mhe Mwigulu Lameck Nchemba akisalimiana na Makamu wa kwanza wa Rais na Waziri Mkuu Mstaafu Mzee John Samwel Malecela mara baada ya kuwasili katika ufunguzi wa kikao cha kazi cha Mwaka 2017 cha Maafisa waandamizi wa Polisi na Makamanda wa Mikoa/Vikosi
Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi Mhe Mwigulu Lameck Nchemba akisalimiana na baadhi ya Maafisa wa jeshi la Polisi mara baada ya kuwasili katika ufunguzi wa kikao cha kazi cha Mwaka 2017 cha Maafisa waandamizi wa Polisi na Makamanda wa Mikoa/Vikosi.

Na Mathias Canal, Dodoma
Askari na Maafisa wa jeshi la Polisi nchini wameaswa kutotumia madaraka yao vibaya kwa kuwabambikizia wananchi kesi kwani kufanya hivyo ni kushindwa kusimamia dhamira njema ya Mhe Rais ya kuwapatia wananchi wanyonge haki zao stahiki.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Mambo ya ndani ya nchi Mhe Mwigulu Nchemba wakati akifungua kikao cha kazi cha Siku tatu cha mwaka 2017 kwa maafisa waandamizi wa Polisi na Makamanda wa Mikoa/Vikosi kilichofanyika katika ukumbi wa Mikutano wa LAPF Mjini Dodoma.
Mhe Mwigulu amesema kuwa kumekuwa na malalamiko kutoka kwa wananchi juu ya kuwabambikizia kesi, Kuwabadilishia watu kesi zao za msingi kwa sababu ya kushindwa kutoa rushwa hivyo kikao hicho kinapaswa kuwa na maamuzi na maadhimio yenye dira na taswira njema kwa jamii na Taifa kwa ujumla.
Amesisitiza pia Askari na Maafisa wa Polisi kutotumia taarifa za watu wanaohasiana kuwa ndio chanzo pekee cha msingi wa shtaka badala yake kufanya uchunguzi kwa kina na kujiridhisha vyema ili kufikia hukumu yenye tija Na haki kwa mtuhumiwa kwani kufanya hivyo kutaimarisha amani na jeshi la Polisi kupata taarifa nyingi za uhalifu kutoka kwa wananchi endapo watajikita katika haki.
Akizungumzia Vita dhidi ya Dawa za Kulevya Mhe Nchemba alisema kuwa serikali imefanikiwa kwa kiasi kikubwa kukamata na kuziteketeza Dawa za kulevya zilizopo mashambani ambapo ametilia msisitizo zaidi kwa Askari na Maafisa wa Jeshi la Polisi kuendelea kupambana ili kuzikamata Dawa za kulevya zilizopo katika viwanda.
Amesisitiza pia Jeshi la Polisi kuendelea kupambana na kubaini uhalifu sambamba na kushirikiana na vyombo vingine ili kuhakikisha lengo mahususi la serikali ambalo ni kuzuia uhalifu linafanikiwa kwa kiasi kikubwa.
Mhe Mwigulu amesema kuwa kauli mbiu ya Mwaka 2017 inayosema "ZINGATIA MAADILI TUNAPOPAMBANA NA UADILIFU ILI KUIMARISHA USALAMA KWA MAENDELEO YA TAIFA" endapo kama itatekelezwa kwa vitendo itaijenga nchi na kuzidi kudumisha zaidi amani iliyopo kwa wananchi.
Naye Kamanda wa Jeshi la Polisi nchini Ernest Mangu alisema kuwa kikao hicho cha kazi kwa Maafisa wa Jeshi la Polisi kina dhamira kubwa ya kufanya Tathmini ya utendaji wa mwaka 2016 na kuandaa mikakati mizuri ya mwaka 2017 na kupata fursa ya kubadilika kiutendaji kwa kuzingatia dhamira ya serikali ya awamu ya Tano inayoongozwa na Mhe Rais Dkt John Pombe Magufuli.
Hata hivyo amesisitiza zaidi askari wote nchini kutofanya kazi kwa mazoea, Kuacha Urasimu na kujenga uaminifu na weledi katika kazi.
Mangu amesema matendo ya Askari Polisi nchini yanapaswa kuwa mfano bora wa kuigwa katika jamii hivyo askari Polisi hapaswi kuwa chanzo cha vurugu au kujihusisha na matendo ovu yasiyostahili katika jamii.
Ameongeza kuwa miongoni mwa mambo yatakayopewa kipaombele kwa kujadiliwa katika Kikao hicho itakuwa ni pamoja na Vita dhidi ya Dawa za Kulevya, Vita dhidi ya Magendo, Vita dhidi ya ujangili na Uvuvi sambamba na Vita dhidi ya Ubambikizaji wa kesi kwa wananchi.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe Jordan Lugimbana akitoa salamu za Mkoa wa Dodoma kabla ya kumkaribisha Waziri Mwigulu Nchemba kuzungumza na askari hao amelipongeza jeshi la Polisi kwa kazi kubwa linayofanya ambapo pia ameeleza mpango wa Mkoa katika kupambana na migogoro ya ardhi kwa kuanzisha kamati maalumu ya wataalamu wa sheria kutoka chuo kikuu cha Dodoma (UDOM) Kupitia na kushauri ili kuweza kumaliza haraka migogoro hiyo.
Naye Makamu wa kwanza wa Rais na Waziri Mkuu Mstaafu Mzee John Samwel Malecela alisema kuwa jambo la msingi ambalo askari Polisi wanapaswa kulifanya ni pamoja na kuhakikisha kila mwananchi anapata Uhuru wake na kama jambo hilo likitekelezwa ipasavyo Fikra za Hayati Mwalimu J.K Nyerere zitakuwa zimeenziwa kwa weledi.

SIRRO: MBOWE ASIPORIPOTI TUTAMFUATA

Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam limesema kama Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe hataripoti bila kutoa taarifa yoyote ya hudhuru atafuatwa kwa kuwa jeshi hilo linahitaji kumhoji.
Kamanda wa kanda hiyo, Simon Sirro amesema hayo leo muda mfupi baada ya Mbowe kueleza kuwa hataripoti polisi kutokana na wito wa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda.
Pia Sirro amesema askofu wa kanisa la ufufuo na uzima Josephat Gwajima na mfanyabiashara maarufu Yusuf Manji walilala polisi kwa kuwa bado upelelezi dhidi yao unaendelea..
"Oparesheni ya dawa za kulevya bado inaendelea na kuanzia sasa hatutaruhusu mkusanyiko wa wananchi karibu na kituo cha polisi hiki watakaoonekana watashughulikiwa na asije akalaumiwa Kamishina Sirro kwa kuwa tayari nimeshatoa taarifa."

Chanzo: Mwananchi

MSAKO DAR WANASA WATUHUMIWA 590

Ndugu wasomaji wetu tunaomba support yenu kwa kutangaza nasi hapa kwenye hii blog kwa bei nafuu ili tuweze kuendelea kutoa habari bila tatizo lolote. Wasiliana nasi kupitia namba +255713363965 / +255755274953. Tunashukuru kwa ushirikiano wenu.


JESHI la Polisi katika Kanda Maalumu Dar es Salaam limewakamata watuhumiwa 586 kwa makosa mbalimbali katika msako uliofanyika kwa siku kumi kuanzia Novemba 22 mwaka huu.

Hayo yalisemwa jijini humo na Kamishna wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Simon Sirro.

Alisema watuhumiwa hao wamekamatwa maeneo mbalimbali kwa nyakati tofauti kwa makosa ya unyang’anyi wa kutumia nguvu, kuvunja nyumba usiku na kuiba, wizi kutoka maungoni, kucheza kamari, kubughudhi abiria, wizi wa magari, shambulio la aibu na la kawaida, kutengeneza, kuuza na kunywa pombe haramu ya gongo pamoja na uvutaji bangi.

Aliongeza kuwa watuhumiwa hao walikamatwa baada ya operesheni iliyofanyika maeneo ya Buguruni na Magomeni ambapo walikamatwa jumla ya watuhumiwa 257, walikamatwa kwa makosa mbalimbali na jumla ya lita 405 za Pombe haramu za gongo zilikamatwa, mitambo miwili ya kutengenezea gongo na bangi.

Kamanda Sirro alisema baadhi ya watuhumiwa hao walikutwa na silaha ndogo ndogo za kufanyia uhalifu kama visu, nyembe, bisibisi. Katika tukio jingine , Polisi Kanda Maalum Dar es salaam kupitia kikosi kazi cha kupambana na ujambazi wa kutumia silaha, mnamo Novemba 29, mwaka huu majira ya saa nne na nusu Kijichi Neluka Mbagala lilifanikiwa kukamata gari lililobeba mali za wizi.

Sirro alisema gari hilo lilikamatwa baada ya majambazi watatu wakiwa na gari Toyota Noah lenye rangi ya fedha lililosajiliwa kwa namba za usajili T 129 DDS, kuvamia baa moja inayofahamika kwa jina la Whatsapp na kuvunja, kisha kuiba vitu mbalimbali vikiwemo seti ya televisheni aina ya Samsung, king’amuzi kimoja cha startimes kimoja, radio moja, spikambili aina ya Sony, na katoni tatu za glasi.

GARI LA WIZI LAMPONZA PADRI WA KANISA KATOLIKI SUMBAWANGA

Ndugu wasomaji wetu tunaomba support yenu kwa kutangaza nasi hapa kwenye hii blog kwa bei nafuu ili tuweze kuendelea kutoa habari bila tatizo lolote. Wasiliana nasi kupitia namba +255713363965 / +255755274953. Tunashukuru kwa ushirikiano wenu.


Kikosi Kazi cha Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam cha kuzuia wizi wa magari kimeendelea na kazi ya kudhibiti vitendo hivyo kwa kumkamata Padri wa Kanisa Katoliki Sumbawanga Demestrious Apolinary kwa tuhuma za kuhusika na ununuzi wa gari ya wizi.

Kamishna wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamanda Simon Sirro amesema mnamo Novemba, 11 baada ya padri huyo kununua gari aina ya Toyota L/cruiser T616 DCH mali ya Joseph Kayawaya lililoripotiwa kuibiwa Dar es Salaam na nyaraka za kughushi na kuuzwa jijini Arusha.

Amesema padri huyo anafanyiwa mahojiano na kwamba upelelezi utakapokamilika atapelekwa mahakamani ili kuona kama ni mnunuzi asiye na hatia au alishiriki kwa namna moja au nyingine katika wizi huo.

Kamanda Sirro amesema pia Jeshi la Polisi linashikilia watuhumiwa wengine wanne aliowataja kwa majina ya Aman Dickson, Exaud Martin, Rashid Haruna na Mzee Nasibu kwa tuhuma za kuhusika na wizi wa magari katika matukio mawili tofauti.

Katika tukio lingine, Kamanda Sirro amesema Jeshi la Polisi linashikilia majambazi watano na vifaa mbalimbali walivyopora maeneo ya Tuwangoma mtaa wa Masaki, Mbagala.