HABARI

Theme images by kelvinjay. Powered by Blogger.

MATUKIO

MICHEZO

SIASA

Wafanyakazi wa Mochwari Watiwa Mbaroni kwa Kuiba Kete 32 za Dawa za Kulevya

Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Simon Sirro amefunguka kuwa wahudumu wa mochwari ya Mwananyamala wameiba jumla ya kete 32 za dawa za kulevya zilizokuwa kwenye mwili wa Raia wa Ghana aliyefariki dunia akiwa katika nyumba ya wageni.

Kamanda Sirro amesema wahudumu hao wanne wote wamekamatwa na kukiri kwamba  baada ya kifo cha raia huyo wa Ghana aliyefariki ndani ya 'Red Carpet' iliyopo Sinza Dar es Salaam walipasua mwili wa raia huyo na kutoa kete hizo kisha kuziuza, na kuongeza wametaja watu ambao wamewauzia ambao nao wamekamatwa na wapo chini ya ulinzi wa polisi

"Yule Mghana ambaye alikutwa amefariki dunia tarehe 14/ 03/ 2017 kwenye nyumba ya wageni ya 'Red Carpet' na alichukuliwa na kupelekwa mochwari Mwananyamala lakini inaonekana wale wahudumu wali[pata taarifa kuwa ule mwili una dawa za kulevya, kimsingi walikula njama wakampasua na kutoa kete 32 za madawa ya kulevya na baada ya kuyapata waliyauza hayo madawa" alisema Sirro

Kamanda Sirro aliendelea kusema kuwa mpaka sasa wanawashikilia watu wanne ambayo wamehusika katika jambo hilo.

"Mpaka sasa tunawashikilia watu wanne ambao wanakiri kupasua mwili huo ambao ni wahusika wakuu na ni wahudumu wa mochwari ya Mwananyamala lakini tumekwenda mbali zaidi baada ya kufanya upasuaji wamemuuzia nani naye amekatwa pia na anaeleza kuwa alinunua hayo madawa, lakini pia naye alichukua na kumuuzia mtu mwingine anayefahamika kwa jina la Ally Nyundo, huyu Nyundo tulishamkataga na kumpeleka kwa Mkemia Mkuu yeye alionekana ni mtumiaji, kimsingi tuna hao watuhumiwa wanne na huyo wa tano aliyekamatwa sasa tunaandaa jalada" alisisitiza Sirro

Binti wa miaka 15 abakwa na vijana wanne Jijini Mwanza

Watu watatu wanashikiliwa na jeshi la polisi huku mwingine mmoja akiendelea kutafutwa kwa tuhuma za kumbaka binti mmoja mwenye umri wa miaka 15 wilayani Ilemela, mkoani Mwanza.

Akitoa taarifa hiyo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza DCP Ahmed Msangi amesema kwamba tukio hilo limetokea tarehe 21/05/2017 majira ya saa moja kamili jioni katika maeneo ya mamlaka ya pamba, kata ya Kirumba ambapo inadaiwa kuwa binti huyo ambaye pia ni mkazi wa Kirumba alikuwa na mahusiano ya kimapenzi na mtuhumiwa aliyejulikana kwa jina moja la Phili na walipanga wakutane katika maeneo hayo.

Inasemekana kuwa binti huyo alikutana na mpenzi wake mahali hapo kisha walikwenda sehemu yenye jumba bovu kuzungumza, wakiwa kwenye eneo hilo ghafla walitokea vijana wengine watatu wakishirikiana na Phili na kuanza kumfanyia ukatili kwa kumbaka.

Inasemekana kuwa wakati wakiendelea na ukatili huo binti alipiga yowe akiomba msaada kutoka kwa wananchi, wananchi walifika eneo la tukio na kumuokoa binti na kufanikiwa kumkamata mtuhumiwa mmoja aitwaye Fredy Remigius kisha walitoa taarifa polisi kuhusiana na tukio hilo.

Askari walifika katika eneo la tukio na kufanya msako mkali wa kuwatafuta watuhumiwa wengine huku wakishirikiana na wananchi na kufanikiwa kuwakamata watuhumiwa wengine wawili huku mmoja aliyekuwa na mahusiano ya kimapenzi na binti akifanikiwa kutoroka.

Amewataja watuhumiwa hao kuwa ni Fredy Remigius miaka 20, mkazi wa Kitangiri, Jackson Joseph miaka 17, mkazi wa Mlimani B na Frank Haruni miaka 18.

Kamanda Msangi amesema mahojiano na watuhumiwa waliokamatwa yanaendelea na pindi uchunguzi ukikamilika watafikishwa mahakamani na kwamba majeruhi aliyebakwa amepelekwa hospitali ya mkoa wa Mwanza Sekou Toure kwa ajili ya matibabu na hali yake inaendelea vizuri.

VIDEO: POLISI WAUA MAJAMBAZI JIJINI MWANZA.

Jeshi la polisi mkoani Mwanza limepambana na watu wanaosadikika kuwa ni majambazi ambapo katika mapambano hayo, wapo waliouawa.
Tazama video hapo chini

WATU WATATU WANAOTUHUMIWA KUHUSIKA NA MAUAJI YA VIONGOZI WA VIJIJI NA ASKARI MKOANI PWANI WAMEUAWA.

Jeshi la polisi mkoani Pwani limewaua kwa kuwapiga risasi watu watatu wanaodhaniwa kuwa wali husika na mauaji ya viongozi wa vijiji na vitongoji na askari polisi katika wilaya za Mkuranga,Kibiti na Rufiji.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Pwani ONESMO LYANGA amesema katika taarifa yake kuwa watu hao wamefariki dunia wakati wakipelekwa hospitali ya Mission ya Mchukwi kwa matibabu baada ya kujeruhiwa kwa risasi miguuni na kiunoni walipojaribu kukimbilia porini wakiwa kwnye pikipiki baada ya kukaidi amri halali ya polisi iliyowata ka  wasimame kutokana na kuwatilia mashaka.

Amesema polisi waliokuwa katika doria walipata taarifa kutoka kwa wa safiri  kuwa waliona pikipiki tatu zilizokuwa zinatokea Kibiti kupitia barabara kuu ya Dar es salaam -Lindi zinepakia watu watatu kila mmoja na pikipiki mbili kati ya hizo ziliwabeba waliovalia hijabu ndipo walipowapa taarifa askari wa usalam barabararni walioko katika kizuizi cha Mparange ili wawasimamishe na kuwatambua lakini hawakutii.

Amesema askari wa kituo cha Mwembe,Muhoro waliwasinamisha lakini hawakutii amri na kuongeza kasi,ndipo askari waliwafuatilia hadi kuvuka daraja la Mkapa  na wakatoa onyo kwa kufyatua risasi hewani lakini waliendelea kukaidi.

Amesema baadaye watu hao waliamua kuruka kutoka kwenye pikipiki  zao na kukimbilia msituni,kitendo kilichowafanya polisi kuwafyatulua risasi za miguuni na kiunoni na kuwakamata lakini walifariki dunia wakati wakikimbizwa hospitali ya Mission ya Mchukwi ambako daktari alithibitisha watu hao walikuwa wameshafariki.

Kamanda amesema majeruhi hao waliovalia hijabu baadaye walitambukiw kuwa walikuwa wanaune waliotumia pikipiki aina ya BOXER yenye namba za usajili MC 272 BLW.

CHANZO: ITV TANZANIA

KAMANDA SIRRO AWATAKA WANANCHI KUTOJICHUKULIA SHERIA MIKONONI

Kamanda wa Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam, Kamishna Simon Sirro amewataka wananchi kuacha kujichukulia sheria mikononi badala yake waviachie vyombo husika ili viweze kufanya kazi yake.

Ameyasema hayo Jijini Dar es salaam wakati akizungumza na waandishi wa habari. Amesema kuwa wananchi kujichukulia sheria mikononi pindi wawakamatapo watuhumiwa ni kinyume cha sheria hivyo wanatakiwa kuacha mara moja tabia hiyo.

“Ni vyema wananchi wakaacha  tabia ya kujichukulia sheria mikononi ili vyombo usika vifanye kazi yake,”amesema Sirro.

Aidha, amesema kuwa wananchi kuwauwa watuhumiwa ni kosa kisheria kwani watakao bainika kufanya hivyo sheria kali dhidi yao zitachukuliwa.

Hata hivyo, ameongeza kuwa ni bora wananchi waache tabia hiyo ya kujichukulia sheria mikononi kwani vyombo husika kama Polisi na Mahakama vipo kwa ajili ya shughuli hiyo.

EKA 17 ZA MASHAMBA YA BANGI ZAFYEKWA

Polisi Mkoa wa Arusha wameteketeza eka 17 za mashamba ya bangi katika Kata ya Kisimiri, wilayani Arumeru.
 
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Charles Mkumbo alisema mashamba hayo yalitekelezwa wakati wa msako maalumu.
 
Mkumbo alitoa onyo kwa wananchi wanauzunguka Mlima Meru ambao wamekuwa wakilima bangi kwa kisingizio kuwa, polisi hawawezi kufika.
 
“Kuna mtindo wa kulima bangi milimani hasa Mlima Meru, tunasema tutaendelea na msako kubaini wote wanaohusika,” alisema.
 
Aliwataka viongozi wa mitaa na madiwani kuwa makini na kudhibiti kilimo hicho haramu kwenye maeneo yao. Kamanda Mkumbo alisema kwa sasa umeanzishwa mtindo wa baadhi ya wananchi kuchanganya bangi na mazao mengine ili kupoteza ushahidi.
 
“Wanachokifanya sasa wanachanganya miche ya mazao na bangi, kwa hiyo inakua pamoja tutaendelea na msako huo kila kona lengo ni kuhakikisha kunakuwa na ukomo wa kilimo hicho cha dawa za kulevya mkoani hapa,” alisema Mkumbo.

MIILI YA ASKARI NANE WALIOUAWA NA MAJAMBAZI MKOANI PWANI YAAGWA RASMI,WAZIRI MWIGULU ATANGAZA KIAMA KWA WATUHUMIWA

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchini, Mwigulu Nchemba, akitoa heshima za mwisho Dar es Salaam mbele ya majeneza yenye miili ya askari nane waliouawa na majambazi Kibiti wilayani Mkuranga mkoani Pwani juzi jioni.Kulia kwake ni Naibu Waziri wa wizara hiyo, Masauni.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchini, Mwigulu Nchemba, akitoa pole kwa wafiwa.
Ndugu,jamaa na marafiki wa wafiwa wakiwa katika shughuli hiyo ya kuaga miili ya wapendwa wao.
Maofisa wa Uhamiaji wakiwa kwenye shughuli hiyo.
Wananchi wakiwa katika shughuli hiyo ya uagaji wa miili hiyo.
Maofisa wa Polisi wakishiriki kuaga miili ya wenzao hao.
Foleni ya kuaga miili hiyo.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchini, Mwigulu Nchemba (kulia), akiteta jambo na Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Ernest Mangu wakati wa kuaga miili hiyo.
Mmoja wa ndugu za askari hao akilia kwa uchungu.






Ni kilio kwa kuwapoteza wapendwa wao.
Ni huzuni.


Na Dotto Mwaibale 

WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba amewatangazia kiama watu wote waliohusika kuwaua askari polisi nane Kibiti wilayani Mkuranga mkoani 
Pwani.

Akizungumza wakati wa kuaga miili ya askari hao jijini Dar es Salaam Mwigulu alisema watu hao watakamatwa  wote na kufikishwa kwenye mkono wa sheria.

"Kitendo hiki cha mauaji kilichofanyika dhidi ya askari wetu hakivumiliki hata kidogo waliohusika tutawatafuta na kuwakamata" alisema Mwigulu.

Aliwaomba wananchi wa maeneo husika kutoa ushirikiano kwa jeshi la polisi ili kuwapata wahusika wa tukio hilo.

Katika hatua nyingine Mwigulu ameitaka wizara husika kuhakikisha inatoa fidia kwa ndugu wa askari hao na majeruhi badala ya kuchukua muda mrefu kuitoa.

"Naomba fidia kwa askari hawa tuliowapoteza wakitumikia taifa itolewa haraka bila kucheleweshwa" aliongeza Mwigulu.

Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini (IGP), Ernest Mangu alisema watuhumiwa wote waliohusika kufanya mauaji hayo ni lazima watafikiwa na mkono wa dola.

Alisema wananchi wa eneo hilo wanawafahamu wahusika hivyo amewaomba washirikiane na polisi ili kuwapata vinginevyo nguvu itatumika.

Alisema linapotokea tukio kama hilo kuna baadhi ya watu wamekuwa wakishabikia kupitia mitandao ya kijamii hivyo akatoa onyo kuwa watakao bainika na wao watakamatwa kwa kutenda kosa.

Askari waliopoteza maisha katika tukio hilo la kinyama wametajwa kuwa ni pamoja na Mkaguzi Msaidizi Peter Kiguu, Koplo Francis, PC Haruna, PC Jackson, PC Zakaria, PC Siwale, PC Maswi na PC Ayoub


Jinsi mauaji ya kutisha ya polisi nane yalivyofanyika

Wakati Taifa likiwa katika simanzi na taharuki baada ya askari wanane kupoteza maisha katika shambulizi lisilo la kawaida dhidi ya Jeshi la Polisi, mashuhuda wa tukio hilo wanasema wauaji walijipanga katika maeneo matatu tofauti katika eneo la tukio kabla ya kufanya shambulizi hilo.
Habari za shambulio hilo la aina yake lililotokea juzi ziliripotiwa na gazeti hili pekee jana na hali ya simanzi ilitawala jana wakati Jeshi la Polisi likitoa taarifa kuhusu tukio hilo, huku Rais John Magufuli akiongoza waombolezaji.
“Baada ya kusikia hili tukio nilikaa kama dakika kumi natafakari bila kupata majibu. Hivi haya matukio yanafanywa na kina nani? Wanafanya kwa malengo gani?” alihoji Othman Juma, aliyekuwa anafuatilia mkutano huo wa Jeshi la Polisi katika ukurasa wa Mwananchi.
Wauaji hao walimshambulia kwa risasi tano dereva wa gari aina ya Toyota Landcruiser (pickup) na wakati askari walipokuwa wanajariku kuruka kujinusuru, watu hao waliwatungua kwa risasi wakati gari likienda kunasa pembeni ya barabara.
Watu hao walilifuata gari hilo liliposimama na kuwavua fulana za kuzuia risasi kisha kuwamalizia tena kwa risasi kabla ya kuchukua silaha saba walizokuta, tatu zikiwa za masafa marefu.
Waandishi wetu waliofika eneo la tukio wamesema hofu imezidi kutanda kwenye vijiji vya Wilaya ya Kibiti, na hasa Kijiji cha Jaribu ambako viongozi wao hawaonekani na wakazi hupotea inapofika nyakati za usiku kuhofia maisha yao.
Mmoja wa mashuhuda wa tukio hilo, aliyeomba jina lake lihifadhiwe, aliiambia Mwananchi kuwa washambuliaji hao walikuwa watatu na walijificha katika maeneo matatu kando ya Barabara ya Dar-Kibiti kuhakikisha hawawezi kulikosa kwa risasi gari hilo la Jeshi la Polisi.
Alisema wakati gari hilo likipita kwa mwendo wa kasi majira ya saa 12 jioni eneo la Mkengeni, Kata ya Mjawa, likiwa limetokea Jaribu Mpakani, kijiji kilichopo takriban kilomita tatu kutoka eneo la tukio, washambuliaji hao walianza kufyatua risasi mfululizo, hasa kumlenga dereva.
“Wauaji hao walifanya mashambulizi hayo wakitokea vichakani kwa kuwa eneo hilo ni pori. Lakini eneo walipouawa askari hao lilikuwa limefyekwa vizuri kwa miti yote na majani kukatwa,” alisema.
Alisema baada ya dereva kushambuliwa, gari lilianza kuyumba na kupoteza mwelekeo na askari waliokuwa ndani walianza kuruka nje ya gari ili kujiokoa au kurudisha mashambulizi na kila waliporuka walikumbana na risasi.
Shuhuda huyo alieleza kuwa baada ya gari kusimama, watu hao walienda kwenye gari hilo lililokuwa limeegemea kwenye ukingo ulio kando ya barabara na kuwamalizia kwa risasi askari hao wanane na mmoja alijeruhiwa mkono wake wa kushoto.
Askari huyo alimudu kuwatoroka wavamizi hao baada ya kutambaa kupanda gema lililokuwa karibu na eneo ambalo gari liligota na kuibukia upande wa pili ambao una mtaro.
“Sielewi. Ni Mungu tu,” alisema askari huyo aliyetambulishwa kwa jina la PC Fredrick ambaye amejeruhiwa mkono wa kushoto.
Lakini dereva wa gari hilo, ambaye pia alijaribu kutoroka eneo hilo, alionekana kirahisi na washambuliaji kwa kuwa alikimbia kunyoosha njia kulingana na mwelekeo wa barabara hiyo na hivyo kushambuliwa kwa risasi nyingine.
Waandishi wetu waliofika eneo la tukio kuanzia jana asubuhi wameeleza kuwa wananchi walisikia milio ya silaha nzito majira ya saa 12:15 jioni, lakini walishindwa kusogelea kutokana na vitendo vya mauaji vinavyoendelea maeneo yao.
Wakazi wa eneo la Mkengeni, Kata ya Mjawa walisema walisikia milio ya silaha nzito tofauti na milio ya bunduki za kawaida na hivyo kuamua kutotoka nje.
Mkazi wa Mkengeni, Rashid Mohamed alisema hofu imezidi kijijini hapo na wanashindwa kufanya biashara zao kama walivyokuwa wakifanya awali, na hivyo maisha yanazidi kuwa magumu.
Mohamed alisema juzi walisikia milio ya bunduki na risasi moja iliangukia kwenye paa la duka lake. Alisema ana hofu kwa sababu biashara yake haiendi vizuri kwa kuwa watu hawaendi kazini kwa kuhofia usalama wao.
“Leo watu wengi hawajaenda kabisa mashambani. Kila mtu ana hofu. Unaweza kwenda halafu ukakutana na hao wauaji. Hali si nzuri kabisa, sijui hatima yangu ni nini,” alisema mfanyabiashara huyo.
Mkazi mwingine wa Kijiji cha Bungu, ambako kuna kambi maalumu ya polisi, Mwajuma Said alisema kwa sasa hawana viongozi kwa kuwa wote wamekimbia baada ya kutishiwa maisha.
Alisema kutokana na kukosa serikali tangu Februari mwaka huu, walianza kupeleka matatizo yao Kituo cha Polisi cha Bungu. Alisema baada ya tukio la juzi hawajui watapeleka wapi shida zao kwa sababu polisi ambao wanawategemea nao wanauawa.
“Walikuja wakatupa vipeperushi kwenye ofisi ambavyo waliandika kwamba wamefika kijiji chetu kwa ajili ya kumuua mwenyekiti, mjumbe na mtendaji wa kijiji. Baada ya vitisho hivyo, viongozi hao walikimbia kijiji hiki, mpaka sasa hatuna serikali,” alisema mwanamke huyo.
Mwalimu mmoja ambaye hakutaka kutaja jina lake, alisema wauaji hao wamekuwa wakielekeza mashambulizi yao kwa watumishi wa umma, jambo ambalo linampa hofu.
“Hatujui hatima yetu itakuwaje. Baadhi ya walimu wanaomba uhamisho ili waondoke eneo hili. Polisi tunao wa kutosha lakini yanapotokea mauaji kama haya tunashindwa kujua ni nguvu gani waliyonayo wauaji hao,” alisema mwalimu huyo mkazi wa Kijiji cha Bungu.
Hali ilivyokuwa jana
Mwananchi ilikuta polisi wakiwa eneo la tukio majira ya saa 4:30 asubuhi, wakichukua vipimo, huku baadhi yao wakiwa wameficha sura kwa kuvaa kinyago kinachoruhusu macho pekee kuonekana.
Eneo hilo ni kilomita tatu kutoka kituo cha ulinzi ambako askari hao walibadilishana lindo na kuanza safari ya kurudi kambini Bungu.
Eneo la tukio hilo ni mteremko uliopo Kijiji cha Mkengeni kilichopo kati ya Mkuranga na Rufiji.
Askari mmoja wa kambi maalumu iliyopo Bungu aliiambia Mwananchi kuwa risasi tano zilipigwa mfululizo upande wa dereva kabla gari hilo halijaacha njia na kwenda kuegemea kwenye ukingo wa bonde dogo lililo pembeni ya barabara.
“Sehemu lilipotokea tukio ni kama ina kichaka na askari aliyenusurika alitambaa kwa tumbo kwenye kichaka cha upande wa kulia kama unaelekea Rufiji na kufanikiwa kujinusuru, ingawa alikuwa ameshapigwa risasi ya mkono,” alisema askari huyo.
Alieleza zaidi kuwa baada ya gari kupinduka na askari hao kupigwa risasi, bado walivuliwa vikinga risasi na kupigwa risasi nyingine.
Akizungumza eneo la tukio Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Evarist Ndikilo alimwambia Waziri wa Mambo ya Ndani Mwigulu Nchemba kuwa washambuliaji hao walijipanga maeneo matatu na walikuwa wanafahamu wanachofanya.
“Wangemkosa hapa, wangempata pale au pale. Lengo lao ilikuwa kumshambulia dereva,” alisema Ndikilo huku akionyesha kwa mikono aliposimama mshambuliaji mmoja baada ya mwingine.
Wananchi katika kijiji cha Mkengeni walikuwa wamesimama katika makundi na wengine wakiwa kwenye vibanda vya kahawa wakijadiliana kuhusu tukio hilo na wengi hawakutaka kuongea na waandishi wakionekana kuhofia maisha yao.
Baada ya Waziri Mwigulu kuwasili eneo la tukio na kupokea maelezo kutoka kwa Kamanda wa Polisi mkoa wa Pwani, Onesmo Lyanga, msafara huo ulielekea Kijiji cha Bungu kuona kambi hiyo maalumu.
Kambi hiyo imetengenezwa kwa maturubai sita ambayo wanaishi askari hao.
Shambulio hilo ni mwendelezo wa matukio kadhaa dhidi ya askari wa Jeshi la Polisi ambayo yamekuwa yakitokea tangu mwaka juzi. Januari 20, 2015, watu wasiojulikana walivamia Kituo cha Polisi cha Ikwiriri wilayani Rufiji na kuua askari wawili waliokuwepo kituoni hapo na kuondoka na silaha walizokuta.
Uvamizi kama huo ulifanyika Februari 3, 2015 wakati kundi la watu wasiojulikana lilipovamia Kituo cha Polisi cha Mgeta wilayani Kilombero na kuchukua bunduki aina ya SMG iliyokuwa na risasi 30.
Tukio jingine lilitokea Julai mwaka juzi wakati watu wasiojulikana walipovamia Kituo cha Polisi Sitakishari, Ukonga, Dar es Salaam na kuua askari wanne na raia watatu na baadaye kupora silaha ambazo idadi yake haikuwekwa bayana.
Katika shambulizi jingine lililofanyika Agosti mwaka jana, polisi wanne waliuawa wakiwa Benki ya CRDB, Mbagala, Dar es Salaam ambako walikuwa wakibadilishana lindo. Watu wasiojulikana waliowasili eneo hilo kwa pikipiki tatu, waliwafyatulia risasi askari hao na kuwaua baadaye kuondoka na bunduki mbili.
Polisi pia wameuawa katika matukio ambayo walijaribu kupambana na watu hao, likiwamo la Vikindu ambako ofisa wa polisi wa cheo cha ASP, Thomas Njuki alipigwa risasi wakati polisi ilipoenda kukamata watuhumiwa wa ujambazi.
“Tumeshapoteza askari zaidi ya 10. Ninaamini wanatosha. Sasa tunaenda kwenye operesheni maalumu, hatutakuwa na mzaha wala msamaha,” alisema kamishna wa operesheni na mafunzo wa Polisi, Nsato Marijani alipoongea na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana.
“Tutawapata popote walipo, tutawashughulikia kikamilifu hakuna atakayebaki. Mapambano haya hayana mwisho, huu ni mwanzo usio na mwisho,”alisema.
Alisema baada ya mauaji hayo ya polisi, operesheni kali ilifanikisha kubaini maficho ya muda ya watu hao.
Kamishna Marijani aliwataja askari waliouwawa katika shambulio hilo kuwa ni Peter Kigugu, ambaye ni mkaguzi msaidizi wa polisi, Koplo Francis, PC Haruna, PC Jackson, PC Zacharia, PC Siwale, PC Maswi na PC Ayoub.
Alisema katika msako huo, polisi waliwaua watu wanne wanaosadikiwa kuwa ni majambazi na kukamata bunduki nne, mbili zikiwa zile zilizoporwa kwa askari.
Alisema watu hao walifanikiwa kuua askari wengi kwa sababu walikuwa pamoja ndani ya gari, na si kwa sababu wana ujuzi wa kipekee.
Alipoulizwa kuhusu uhusiano wa shambulio hilo na ugaidi, Kamishna Marijani alisema: “Wale ni majambazi, hawana lolote. Si chochote. Hatuwezi kuweka kanda maalum kwa sababu yao. Wameamua kupambana na Jeshi la Polisi kwa sababu tunawazuia. Huu si ugaidi, ni ujambazi.”
Alisema matukio ya uhalifu yametawala mkoani Pwani kutokana na kuwa na mapori yanayowavutia wahalifu na kuweka maficho yao.
Kamishna Marijani aliwataka wananchi kuliunga mkono Jeshi la Polisi katika operesheni hiyo, ikiwa ni pamoja na kutoa taarifa.
Kamishna pia alipiga marufuku pikipiki kuonekana Kibiti, Mkuranga na Rufiji kuanzia saa 12:00 jioni.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Pwani, Onesmo Lyanga alisema watu hao waliiba silaha saba, nne zikiwa ni bunduki aina ya SMG na bunduki tatu za masafa marefu.
Alisema bunduki nyingine mbili aina ya SMG zilizokuwa sehemu ya mbele ya gari la polisi zilipatikana kwa kuwa washambuliaji hao hawakuziona.
Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba alitembelea eneo hilo na kusema wanaofanya mauaji hayo watashughulikiwa.
“Hatukubaliani na jambo hilo, halina nafasi. Mkuu wa Mkoa pokeeni pole na fungeni mikanda upya ili tuunganishe nguvu kukabiliana na uhalifu huu,” alisema Mwigulu akiwa katika kambi maalumu ya Bungu muda mfupi baada ya kuwasili eneo la tukio saa 7:00 mchana.
Waziri Mwigulu aliwapa pole polisi na kuwataka kusonga mbele ili kuhakikisha silaha zilizoibwa zinarudishwa.
Akizungumzia zaidi tukio hilo, Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Ndikilo alisema ni tukio zito kwa mkoa kupoteza askari wanane wakati mmoja. “Ni tukio zito na mtihani mkubwa kwa wananchi, hasa wanapoona askari walioletwa kuwalinda nao wamefariki,” alisema Ndikilo.
Aliwataka wananchi wawe na subira wakati serikali ya mkoa ikiendelea kulifanyia kazi suala hilo.


Chanzo: Mwananchi

WAZIRI NCHEMBA AWASILI ENEO YALIPOTOKEA MAUAJI YA POLISI WANANE

Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba amewasili eneo yalipotokea mauaji ya askari wanane katika kijiji cha Jaribu, Wilayani Kibiti.
Waziri Nchemba ameambatana na naibu wa wizara hiyo, Mhandisi Hamad Masauni.
Nchemba atatembelea kambi za askari polisi wa kanda ya Pwani na katika kata ya Bungu wilayani Kibiti.

MAJAMBAZI YALIYOUA POLISI 8 KWA RISASI NAYO YAMEUAWA

Jeshi la Polisi Tanzania limesema limewaua majambazi wanne ambao walikuwa ni sehemu ya kundi la majambazi lililowashambulia na kuwaua askari 8 wilayani Kibiti mkoani Pwana jana usiku.

Akizungumza na wanahabari leo, Kamishna wa Oparesheni na Mafunzo wa jeshi hilo, Nsato Marijani amesema kuwa mara baada ya kundi hilo kuwashambulia askari, kikosi kingine cha askari kilifanya msako na kubaini maficho ya majambazi hao.

Amesema baada ya kuwabaini, yalifanyika mashambulizi ya kurushiana risasi, ambapo majambazi wanne waliuawa pamoja na kukamata bunduki 4 zikiwemo SMG mbili zilibainika kuwa kati ya zile zilizoporwa na majambazi hao.

Akielezea tukio hilo lilivyokuwa, Kamishna Marijani amesema kundi la waharifu walikuwa na silaha za moto na ambao idadi yao haikujulikana liliweka mtego na kufanikiwa kuishambulia kwa risasi gari iliyokuwa na askari 9 waliokuwa wakitoka katika malindo kurudi kambini, na kuwaua askari 8 kati yao huku mmoja akijeruhiwa mkononi.

Amewataja askari waliuawa kuwa ni pamoja na Mkaguzi Msaidizi Peter Kiguu, Koplo Francis, PC Haruna, PC Jackson, PC Zakaria, PC Siwale, PC Maswi na PC Ayoub, ambapo pia walipora bunduki 7 zikiwemo SMG 4.

Kufuatia tukio hilo, Kamishna Marijani ametangaza vita na waharifu wote katika maeneo hayo, ambapo amesema vyombo vya ulinzi na usalama vinaanza oparesheni maalum katika mkoa wa Pwani, kuhakikisha vinawasaka na kukomesha mauaji hayo ikiwa ni pamoja na kuwachukulia hatua.

"Mpaka sasa jeshi limekwisha poteza skari zaidi ya 10, inatosha…. Tunakwenda kwenye oparesheni maalum, hatutakuwa na mzaha, tutawasaka popote walipo na kuwashughulikia kikamilifu, ,,, watajua tofauti ya moto na maji… mpaka jana idadi ilikuwa ni 8 kwa nne, lakini nawahakikishia kuwa ndani ya wiki moja idadi hiyo itakuwa imebadilika, na tutakuwa na hesabu tofati” amesema Marijani

Kuhusu hofu ya ugaidi, Kamishna Marijani amesema tukio hilo siyo la kigaidi bali ni uhalifu wa kawaida, huku akibainisha kuwa Tanzania hakuna ugaidi

Katika hatua nyingine, jeshi hilo limepiga marufuku uendeshaji wa pikipiki katika maeneo yote ya Kibiti, Mkuranga na Rufiji zaidi ya saa 12:00 jioni. Amesema usafiri wa boda boda utaruhusiwa kati ya saa 12:00 asubuhi hadi saa 12:00 jioni.

CHANZO: EATV 

JESHI LA POLISI LATOA TAHADHARI MSIMU HUU WA SIKUKUU YA PASAKA




WATU WATATU WANAODHANIWA KUWA NI MAJAMBAZI WAULIWA KWA KUPIGWA RISASI NA POLISI

Watu watatu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi  wameuwa kwa kupigwa risasi na polisi baada ya kukaidi amri ya kutakiwa kusimama eneo la kizuizi cha Mwembe Muhoro wilayani Rufiji, mkoani Pwani.

Watu hao walikuwa wamepakiana kwenye pikipiki moja huku wakiwa wamevaa hijabu.

Akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na tukio hilo, kamanda wa Polisi mkoani Pwani ,Onesmo Lyanga alisema pikipiki nyingine mbili zilifanikiwa kukimbia.

Akielezea juu ya tukio hilo alifafanua,lilitokea Aprili 2 mwaka huu majira ya mchana ,Muhoro ,Rufiji barabara kuu ya Dar es Salaam Lindi.

“Siku ya tukio askari walipata taarifa kuwa kulikuwa na pikipiki tatu zikitokea Kibiti kwenda mikoa ya Kusini zikiwa zimebeba watu watatu kila moja “

“Miongoni mwa pikipiki hizo kati yake mbili wamebebwa watu waliovaa hijabu,” alisema Lyanga.

Alisema askari wa barabarani walipewa taarifa katika kizuizi cha Mparange na kuwasimamisha ili wawahoji lakini walikataa na kupita ambapo waliwajulisha wenzao kwenye kizuizi cha Ikwiriri lakini walikaidi kusimama.

“Baada ya hapo walifika kizuizi cha Ikwiriri lakini bado walikaidi kusimama na kuendelea kukimbia ndipo walipofika kituo cha Muhoro “

“Hata hivyo hawakusimama na askari waliokuwa doria wakiwa kwenye gari waliwafuatilia na wakavuka daraja la Mkapa na waliwapa onyo kwa kupiga risasi hewani,” alisema Lyanga.

Aidha alibainisha baada ya hapo watu hao waliruka kwenye pikipiki na kuanza kukimbilia msituni na ndipo askari walipowapiga risasi za miguu na kiunoni na kufanikiwa kuwakamata.

“Majeruhi hao walijulikana ni wanaume hata hivyo majina yao hayakuweza kufahamika na walikuwa kwenye pikipiki yenye namba za usajili MC 272 BLW aina ya Boxer yenye rangi nyeusi”

“Watu hao wanaodhaniwa kuwa ni majambazi  kwa mwonekano wao walijaribu kuwawahisha hospitali ya Misheni ya Mchukwi,” alisema Lyanga.

Lyanga alisema walipofikishwa hospitali daktari alithibitisha kuwa watu hao wamefariki dunia .

Hata hivyo majina yao hayakuweza kufahamika huku pikipiki nyingine mbili zilitoroka na kuelekea mkoa wa Lindi na taarifa zimetolewa polisi ili wawakamate.

Aliwataka wananchi kuwa watulivu pale wanaposimamishwa na askari polisi badala ya kujaribu kutoroka na kwa sasa jeshi hilo limeimarisha doria katika kukabiliana na uhalifu.

WAZIRI MWIGULU AWAASA ASKARI KUTOWABAMBIKIZIA WATU KESI

Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi Mhe Mwigulu Lameck Nchemba akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao cha kazi cha Mwaka 2017 cha Maafisa waandamizi wa Polisi na Makamanda wa Mikoa/Vikosi.
Mzee John Samwel Malecela akizungumza wakati wa kikao cha kazi cha Mwaka 2017 cha Maafisa waandamizi wa Polisi na Makamanda wa Mikoa/Vikosi.
Kamanda wa Jeshi la Polisi nchini Ernest Mangu Akisisitiza jambo wakati wa kikao cha kazi cha Mwaka 2017 cha Maafisa waandamizi wa Polisi na Makamanda wa Mikoa/Vikosi


Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe Jordan Lugimbana akitoa salamu za Mkoa wa Dodoma wakati wa kikao cha kazi cha Mwaka 2017 cha Maafisa waandamizi wa Polisi na Makamanda wa Mikoa/Vikosi
 Maafisa waandamizi wa Polisi na Makamanda wa Mikoa/Vikosi
Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi Mhe Mwigulu Lameck Nchemba akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao cha kazi cha Mwaka 2017 cha Maafisa waandamizi wa Polisi na Makamanda wa Mikoa/Vikosi.
SACP Ramadhani Mungi Msimamizi wa bandari Tanzania na Kamanda wa polisi mkoa wa Lindi Renata Mzinga wakifatilia kwa makini kikao cha kazi cha Mwaka 2017 cha Maafisa waandamizi wa Polisi na Makamanda wa Mikoa/Vikosi.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi Mhe Mwigulu Lameck Nchemba akisalimiana na Makamu wa kwanza wa Rais na Waziri Mkuu Mstaafu Mzee John Samwel Malecela mara baada ya kuwasili katika ufunguzi wa kikao cha kazi cha Mwaka 2017 cha Maafisa waandamizi wa Polisi na Makamanda wa Mikoa/Vikosi
Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi Mhe Mwigulu Lameck Nchemba akisalimiana na baadhi ya Maafisa wa jeshi la Polisi mara baada ya kuwasili katika ufunguzi wa kikao cha kazi cha Mwaka 2017 cha Maafisa waandamizi wa Polisi na Makamanda wa Mikoa/Vikosi.

Na Mathias Canal, Dodoma
Askari na Maafisa wa jeshi la Polisi nchini wameaswa kutotumia madaraka yao vibaya kwa kuwabambikizia wananchi kesi kwani kufanya hivyo ni kushindwa kusimamia dhamira njema ya Mhe Rais ya kuwapatia wananchi wanyonge haki zao stahiki.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Mambo ya ndani ya nchi Mhe Mwigulu Nchemba wakati akifungua kikao cha kazi cha Siku tatu cha mwaka 2017 kwa maafisa waandamizi wa Polisi na Makamanda wa Mikoa/Vikosi kilichofanyika katika ukumbi wa Mikutano wa LAPF Mjini Dodoma.
Mhe Mwigulu amesema kuwa kumekuwa na malalamiko kutoka kwa wananchi juu ya kuwabambikizia kesi, Kuwabadilishia watu kesi zao za msingi kwa sababu ya kushindwa kutoa rushwa hivyo kikao hicho kinapaswa kuwa na maamuzi na maadhimio yenye dira na taswira njema kwa jamii na Taifa kwa ujumla.
Amesisitiza pia Askari na Maafisa wa Polisi kutotumia taarifa za watu wanaohasiana kuwa ndio chanzo pekee cha msingi wa shtaka badala yake kufanya uchunguzi kwa kina na kujiridhisha vyema ili kufikia hukumu yenye tija Na haki kwa mtuhumiwa kwani kufanya hivyo kutaimarisha amani na jeshi la Polisi kupata taarifa nyingi za uhalifu kutoka kwa wananchi endapo watajikita katika haki.
Akizungumzia Vita dhidi ya Dawa za Kulevya Mhe Nchemba alisema kuwa serikali imefanikiwa kwa kiasi kikubwa kukamata na kuziteketeza Dawa za kulevya zilizopo mashambani ambapo ametilia msisitizo zaidi kwa Askari na Maafisa wa Jeshi la Polisi kuendelea kupambana ili kuzikamata Dawa za kulevya zilizopo katika viwanda.
Amesisitiza pia Jeshi la Polisi kuendelea kupambana na kubaini uhalifu sambamba na kushirikiana na vyombo vingine ili kuhakikisha lengo mahususi la serikali ambalo ni kuzuia uhalifu linafanikiwa kwa kiasi kikubwa.
Mhe Mwigulu amesema kuwa kauli mbiu ya Mwaka 2017 inayosema "ZINGATIA MAADILI TUNAPOPAMBANA NA UADILIFU ILI KUIMARISHA USALAMA KWA MAENDELEO YA TAIFA" endapo kama itatekelezwa kwa vitendo itaijenga nchi na kuzidi kudumisha zaidi amani iliyopo kwa wananchi.
Naye Kamanda wa Jeshi la Polisi nchini Ernest Mangu alisema kuwa kikao hicho cha kazi kwa Maafisa wa Jeshi la Polisi kina dhamira kubwa ya kufanya Tathmini ya utendaji wa mwaka 2016 na kuandaa mikakati mizuri ya mwaka 2017 na kupata fursa ya kubadilika kiutendaji kwa kuzingatia dhamira ya serikali ya awamu ya Tano inayoongozwa na Mhe Rais Dkt John Pombe Magufuli.
Hata hivyo amesisitiza zaidi askari wote nchini kutofanya kazi kwa mazoea, Kuacha Urasimu na kujenga uaminifu na weledi katika kazi.
Mangu amesema matendo ya Askari Polisi nchini yanapaswa kuwa mfano bora wa kuigwa katika jamii hivyo askari Polisi hapaswi kuwa chanzo cha vurugu au kujihusisha na matendo ovu yasiyostahili katika jamii.
Ameongeza kuwa miongoni mwa mambo yatakayopewa kipaombele kwa kujadiliwa katika Kikao hicho itakuwa ni pamoja na Vita dhidi ya Dawa za Kulevya, Vita dhidi ya Magendo, Vita dhidi ya ujangili na Uvuvi sambamba na Vita dhidi ya Ubambikizaji wa kesi kwa wananchi.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe Jordan Lugimbana akitoa salamu za Mkoa wa Dodoma kabla ya kumkaribisha Waziri Mwigulu Nchemba kuzungumza na askari hao amelipongeza jeshi la Polisi kwa kazi kubwa linayofanya ambapo pia ameeleza mpango wa Mkoa katika kupambana na migogoro ya ardhi kwa kuanzisha kamati maalumu ya wataalamu wa sheria kutoka chuo kikuu cha Dodoma (UDOM) Kupitia na kushauri ili kuweza kumaliza haraka migogoro hiyo.
Naye Makamu wa kwanza wa Rais na Waziri Mkuu Mstaafu Mzee John Samwel Malecela alisema kuwa jambo la msingi ambalo askari Polisi wanapaswa kulifanya ni pamoja na kuhakikisha kila mwananchi anapata Uhuru wake na kama jambo hilo likitekelezwa ipasavyo Fikra za Hayati Mwalimu J.K Nyerere zitakuwa zimeenziwa kwa weledi.