Mawaziri Watajwa Kuficha Mabilioni Benki Za Uswisi

ZITTO ASEMA YUMO KIONGOZI WA JUU WA SERIKALI YA SASA,WENGINE NI WA AWAMU YA MKAPA, ATISHIA KUWAANIKA

TUHUMA kwamba baadhi ya vigogo Serikali wameficha mabilioni ya fedha nchini Uswisi jana ziliibuka tena bungeni, huku Kambi ya Upinzani ikidai kwamba inawafahamu wahusika wa ufisadi huo na kutishia kuwataja ikiwa Serikali haitawataja.

Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Zitto Kabwe aliitaka Serikali kuwataja kwa majina viongozi na wafanyabiashara wakubwa walioficha Sh315.5 bilioni nchini Uswisi, akisema kwamba watu hao “wanafahamika”.

Juni mwaka huu, Benki Kuu ya Uswisi ilitoa taarifa inayoonyesha kuwapo kwa kiasi cha Sh315.5 bilioni zilizotoroshwa Tanzania na kufichwa nchini humo na vigogo ambao ni wanasiasa pamoja na wafanyabiashara.

Akiwasilisha hotuba ya kambi yake kuhusu Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Fedha na Uchumi bungeni jana, Zitto ambaye pia ni Waziri Kivuli wa wizara hiyo alisema mmoja wa viongozi wa juu wa Tanzania na baadhi ya mawaziri wa Serikali za awamu zilizopita ni miongoni mwa wamiliki wa fedha hizo.

“Kambi ya Upinzani bungeni imepata taarifa kuwa mmoja wa viongozi wa juu kabisa wa Tanzania na baadhi ya mawaziri wa awamu zilizopita ni miongoni mwa fedha hizi,” alisema Zitto.

Pia aliitaka Serikali kuliambia taifa ni hatua gani itakazochukua kurejesha fedha hizo pia kuwataka wamiliki wake na kama ikishindwa, wao watawataja.

“Tunaitaka Serikali kutoa taarifa rasmi ya hatua gani imechukua mara baada ya taarifa ile kutoka Benki ya Taifa ya Uswisi ilipotolewa,” alisema Zitto na kuongeza:

“Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni italazimika kuweka wazi taarifa na majina ya watu wenye umiliki wa fedha hizo iwapo Serikali haitatoa taarifa rasmi,” alisisitiza.

Fedha hizo zinadaiwa kutokana na biashara (deals) zilizofanywa na watendaji wa Serikali na wafanyabiashara kwenye Sekta za Nishati na Madini na kwamba sehemu kubwa ya fedha zililipwa na kampuni za utafutaji mafuta na gesi katika pwani ya Mkoa wa Mtwara zilizopewa mikataba kati ya mwaka 2004 na 2006.

Baada ya Zitto kumaliza kuwasilisha hotuba yake, Mbunge wa Simanjiro (CCM), Christopher Ole-Sendeka aliomba mwongozo wa Spika kuhusu suala hilo.

Sendeka alisema Zitto alisema miongoni mwa walioficha fedha hizo ni kiongozi wa juu wa Tanzania, lakini akashangaa Serikali kutohoji juu ya kauli hiyo.

“Mheshimiwa Naibu Spika, mheshimiwa Zitto amewatuhumu viongozi wa Serikali na kiongozi wa juu kabisa kuwa wameficha fedha Uswisi,” alisema.

Alisema, lakini pamoja na tuhuma hizo, hakuna kiongozi wa Serikali aliyesimama na kutolea ufafanuzi hivyo akaomba mwongozi ili Zitto aruhusiwe kuwataja.

Sendeka alisema tuhuma hizo ni nzito na zimeichafua sura ya Serikali hivyo ni vyema ijulikane ni nani kati ya Serikali na Zitto atabeba mzigo wa kuwataja.
Naibu Spika, Job Ndugai alisema angetoa mwongozo huo baada ya kuipitia hotuba hiyo ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni na kuona kama ina matatizo. Hata hivyo, hakutoa mwongozo huo.

No comments

Powered by Blogger.