Dar es Salaam. Kesi inayomkabili Mkurugenzi wa
Ulinzi na Usalama wa Chadema, Wilfred Lwakatare na mwenzake, Joseph
Ludovick Rwezaura, sasa imetua Mahakama ya Rufani, baada ya Mkurugenzi
wa Mashtaka (DPP) kuiomba mahakama hiyo kuingilia kati.
Lwakatare na Rwezaura, walikuwa wakikabiliwa na
kesi ya ugaidi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, lakini Mahakama
Kuu iliwafutia mashtaka hayo na kubaki na shtaka la kula njama.
Hata hivyo, DPP amewasilisha maombi ya marejeo
Mahakama ya Rufani akiomba iitishe majalada ya kesi hiyo na kuchunguza
uhalali wa uamuzi wa Mahakama Kuu wa kuwafutia mashtaka ya ugaidi.Katika maombi yaliyowasilishwa na DPP, anaiomba
Mahakama ya Rufani ifute uamuzi na amri za Mahakama Kuu, kuhusu uhalali
wa mashtaka yaliyokuwa yakiwakabili washtakiwa.
DPP, katika maombi hayo anadai washtakiwa walikuwa
hawajaitwa kujibu mashtaka na kwamba, kwa hali hiyo haikuwa sahihi
Mahakama Kuu kuamua kuwa mashtaka hayo hayakuwa halali.
Pia, anadai kuwa katika maombi ya washtakiwa
Mahakama Kuu, hapakuwapo na maombi ya kufuta mashtaka. DPP anaongeza
katika maombi hayo kuwa, hapakuwa na taarifa zilizowasilishwa dhidi ya
washtakiwa, ambazo Mahakama Kuu ingezizingatia kuamua uhalali wake, au
kuwapo kwa upungufu.
Hivyo anaomba Mahakama ya Rufani ione kuwa uamuzi
wa Mahakama Kuu kufuta baadhi ya mashtaka kwenye hati ya mashtaka ya
awali, yaliyokuwa yakiwakabili washtakiwa hao haukuwa sahihi.
Lwakatare na Rwezaura walikuwa wakikabiliwa na
mashtaka manne, matatu kati ya hayo yakiwa ya ugaidi na moja la kawaida
la jinai, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.
Walikuwa wakidaiwa kula njama na kupanga kumteka Dennis Msacky, kisha kumdhuru kwa kutumia sumu.
Hata hivyo, Mei 8, mwaka huu Jaji Lawrence Kaduri
wa Mahakama Kuu aliwafutia mashtaka ya ugaidi na kuwabakizia linalohusu
jinai ya kula njama za kutenda kosa la kumdhuru Msacky kwa kutumia sumu.
MWANANCHI
MWANANCHI
No comments:
Post a Comment