WIZARA YA UJENZI YAKABIDHI NYUMBA 13 KWA JESHI LA POLISI MKOANI KIGOMA

 Waziri wa Ujenzi (katikati) akiongozana na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi Eng. Joseph Nyamhanga (kulia) na Eng. Mashaka Mgallah ambaye ni Meneja wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) mkoa wa Kigoma, kukagua eneo lililokuwa kambi ya ujenzi wa barabara ya Mwandiga – Manyovu mkoani Kigoma. Nyumba hizo zimetelekezwa kwa miaka 2. Wengine katika picha ni Watendaji kutoka Taasisi mbalimbali za Serikali
 Moja ya nyumba zilizotelekezwa katika kambi ya ujenzi wa barabara ya Mwandiga – Manyovu.
 ENDELEA KUSOMA HABARI HII KWA KUBOFYA HAPA CHINI



Waziri wa Ujenzi Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli akipata maelezo kutoka kwa Meneja wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) Eng. Mashaka Mgallah (wa pili kulia) wakati alipofanya ziara ya ghafla kukagua nyumba katika kambi iliyokuwa ikitumiwa na Wahandisi wakati wa ujenzi wa barabara ya Mwandiga – Manyovu mkoani Kigoma.
Waziri wa Ujenzi Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ameagiza kukabidhiwa mara moja kwa Jeshi la Polisi mkoani Kigoma nyumba zote 13 zilizoko katika kambi iliyokuwa ikitumiwa na Wahandisi waliosimamia ujenzi wa barabara ya Mwandiga hadi Manyovu ambayo ujenzi wake umekamilika kwa kiwango cha lami.
Hatua hiyo ya Waziri Magufuli imetokana na nyumba hizo kuachwa bila ya matumizi yoyote kwa muda wa miaka miwili. Akimhoji Meneja wa Wakala wa Majengo wa mkoa wa Kigoma sababu za kuachwa kwa nyumba hizo kwa kipindi chote hicho wakati yapo mahitaji makubwa ya nyumba kwa ajili ya Watumishi wa Umma na Ofisi za Serikali, Meneja wa TBA wa mkoa huo Eng. Mashaka Mgallah alibainmisha kuwa awali Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) uliarifiwa kuwa majengo hayo yamekabidhiwa kwa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Kigoma.
Katika hali ya kusikitisha wakati Mheshimiwa Magufuli alipofanya ukaguzi wa kushitukiza katika eneo hilo alikuta nyumba hizo zikiwa zimetelekezwa huku vifaa vingi vikiwa vimeibwa vikiwemo viyoyozi na samani mbali mbali. Kutokana na hali hiyo yakatolewa amelekezo kwa taasisi zote zilizo chini ya Wizara ya Ujenzi kutekeleza zoezi maalum la kuhakiki mali zote zilizo katika miradi inayoendelea ili zithaminiwe mara miradi hiyo inapokamilika tayari kwa kukabidhiwa Serikalini.
"Ninawaagiza hasa Watendaji Wakuu wa Tanroads, TBA na TEMESA na Taasisis nyingine katika Wizara ya Ujenzi mfanye ukaguzi wa mali zilizo katika kila mradi unaoendelea nchi nzima ili pale mradi unapokamilika ifanyike tathmini ya mali zinazokabidhiwa Serikalini" alisitiza Waziri Magufuli.
Naye Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Kigoma ACP Frasser Kashai kwa upande wake ameshukuru Waziri wa Ujenzi kwa uamuzi huo ambao ameuelezea kutolewa katika wakati muafaka hasa kutokana na kuwepo kwa tatizo kubwa la makazi kwa ajili ya askari wa jeshi hilo sio tu katika mji wa Kigoma bali katika mkoa mzima kwa ujumla wake.
"Nyumba hizo mnapewa bila ya malipo yoyote kwa ajili ya matumizi ya jeshi la polisi hadi hapo taarifa nyingine itakapotolewa, TBA na Tanroads wahakikishe kuwa huduma za maji na umeme zimeunganishwa katika eneo hilo" alimalizia Waziri Magufuli.

No comments

Powered by Blogger.