URAIS UKAWA, HESABU ZINALALIA CHADEMA

Ndugu wasomaji wetu tunaomba support yenu kwa kutangaza nasi hapa kwenye hii blog kwa bei nafuu ili tuweze kuendelea kutoa habari bila tatizo lolote. Wasiliana nasi kupitia namba +255713363965 / +255755274953. Tunashukuru kwa ushirikiano wenu.



Wakati wenyeviti wa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) pamoja na kamati zake za kitaalamu wanakutana Zanzibar kutafuta suluhu kuhusu mgawanyo nafasi za kugombea katika uchaguzi mkuu ujao, kuna uwezekano mkubwa vyama hivyo kuteua mgombea urais kutoka Chadema.
Tovuti hii inaweza kuripoti kwa uhakika kuwa uwezekano huo unatokana na vigezo vinavyotumiwa na vyama hivyo kusimamisha mgombea mmoja kwa kila jimbo na kwenye nafasi ya urais ambavyo vinaipa Chadema nafasi hiyo dhidi ya vyama vingine katika umoja huo ambavyo ni CUF, NCCR-Mageuzi na NLD.
Vigezo hivyo ni matokeo ya uchaguzi 2010, idadi ya madiwani kwa kila chama, matokeo ya uchaguzi wa Serikali za Mitaa wa Desemba mwaka jana, mtandao wa chama nchini na nguvu ya mgombea iwapo Chadema kitamsimamisha katibu mkuu wake, Dk Willibrod Slaa kwa mara ya pili.
Taarifa zilizolifikia Mwananchi kutoka ndani ya kamati ya ufundi ya Ukawa zinasema pamoja na kuwapo mvutano katika baadhi majimbo Tanzania Bara, kwa upande wa Zanzibar hakuna tatizo hilo, jambo linaloipa CUF nafasi ya moja kwa moja kwenye ubunge, uwakilishi na hata urais wa visiwa hivyo.
ENDELEA KUSOMA HABARI HII KWA KUBOFYA HAPA CHINI
Kwa mujibu wa habari hizo, nafasi nzuri ya CUF kupita moja kwa moja Zanzibar bila ushindani ndani ya Ukawa, inatoa fursa kwa upande wa Bara, kwa vyama vilivyosalia kupitishwa kuwania urais wa Muungano.
Hata hivyo, kwa vigezo vilivyotajwa hapo juu, Chadema ndiyo inakuwa na nafasi isiyo na kipingamizi kutokana na rekodi vyama vilivyosalia Bara.
Katika Uchaguzi Mkuu wa 2010, Chadema kilimsimamisha Dk Slaa na aliibuka wa pili baada ya Rais Jakaya Kikwete akiwa na kura 2,271,941 (asilimia 26.34) akifuatiwa na Profesa Ibrahim Lipumba aliyepata kura 695,667 (asilimia 8.06) na Hashim Rungwe wa NCCR-Mageuzi aliyepata kura 26,388 (asilimia 0.31). NLD haikusimamisha mgombea urais.
Kwa upande wa majimbo yaliyotokana na uchaguzi wa 2010, Chadema kiliongoza kikiwa na wabunge 24 (wote kutoka Bara), CUF 23 (wawili kutoka Bara, 21 Zanzibar) na NCCR-Mageuzi wanne (wote wa Bara).
Katika rekodi za uchaguzi wa mitaa zilitolewa na Tamisemi kabla ya chaguzi za marudio, Chadema ilipata mitaa 980, ikifuatiwa na CUF (mitaa 266), NCCR Mageuzi  (28)  na NLD mtaa mmoja. Kwa upande wa vijiji, Chadema kilishinda vijiji 1,754, CUF (516), NCCR-Mageuzi (67) na NLD vijiji viwili.
Hata kwa upande wa vitongoji Chadema kiliviongoza vyama hivyo kwa kupata vijiji 9,145 kikifuatiwa na CUF (2,561), NCCR-Mageuzi (339) na NLD vitongoji viwili.
Tayari NCCR-Mageuzi kimeonyesha nia ya kumteua Dk George Kahangwa kuwania urais wakati Mwenyekiti wa NLD, Dk Emmanuel Makaidi alikaririwa na gazeti hili hivi karibuni akisema kuwa chama chake kimekwishamteua kuwania urais, hivyo jina lake litapelekwa Ukawa kushindanishwa.
Mvutano mkali
Hali ikiwa hivyo, wajumbe wa Ukawa leo watakumbana na wakati mgumu wa kufikia maridhiano ya kugawana majimbo 19 kutokana na taarifa za kuwapo mvutano mkali wa pande zote za vyama husika.
Wanaokutana leo ni wenyeviti wa vyama, makamu wenyeviti, makatibu na wajumbe wa sekretarieti kutoka vyama hivyo.
Kabla ya kuanza kikao cha leo, jana asubuhi wajumbe 16 wa Kamati ya Ufundi walikutana na baadaye jioni wenyeviti wa umoja huo wakawa na kikao cha awali, ikiwa ni sehemu ya vikao vya hatua za kugawana maeneo ya kuwania ili kutoa ushindani na hatimaye ushindi dhidi ya CCM.
Chanzo cha habari kutoka ndani kimelieleza Mwananchi kuwa NLD nayo imeongeza mvutano ikihitaji majimbo matano.
Wiki iliyopita, gazeti hili liliandika kuwa Ukawa ilikuwa imekamilisha kazi ya ugawaji wa majimbo 170 lakini ukawapo mvutano katika majimbo 19 ambayo vyama zaidi ya kimoja vilikuwa vinayataka.
Majimbo hayo ni Segerea, Kinondoni, Kigamboni na Ukonga ya Dar es Salaam, Morogoro Mjini na mengine ya mikoa ya Mwanza, Shinyanga na Kagera.
“Mvutano ni kwamba, kuna vyama vinavyotaka uwakilishi tu wa majimbo hayo lakini kiukweli yanaweza kupotea bure tu endapo vitakabidhiwa. Wengine wanataka kuangalia zaidi ushawishi wa chama ndani ya jimbo husika ila wengine wanapinga, wakisema umoja huo hautakuwa na sababu kama watakosa uwakilishi,” kilieleza chanzo hicho.
“NLD wanahitaji majimbo matano, CUF na Chadema wanavutana zaidi, ila NCCR-Mageuzi wameonekana kushtushwa sana na hali hiyo,” kilisema chanzo kingine kutoka NCCR-Mageuzi.
Chanzo kingine kilieleza kuwa kamati ya wataalamu ilishakamilisha kazi yake ya uchambuzi wa majimbo hayo na kuwasilisha taarifa zake lakini kuna upinzani mkali ambao umeendelea kuibuliwa na wajumbe wa umoja huo.
“Kikao cha leo kinaashiria kuwa na mvutano, ninaamini kuna uwezekano wa kufikia mwafaka lakini ikishindikana kabisa kwa leo lazima vitaandaliwa vikao vingine,” kilieleza chanzo kingine.
Hata hivyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Wataalamu, Benson Kigaila (Chadema) alisita kuweka wazi juu ya mvutano uliopo huku akibainisha kuwa maridhiano yatapatikana.
Kigaila alisema kikao cha leo kina nafasi kubwa ya kumaliza mvutano huo na kueleza Watanzania juu ya mwelekeo wa safari yao.
Kigaila ambaye pia ni Mkurugenzi wa Oganaizesheni ya Mafunzo na Usimamizi wa Kanda wa Chadema, alisema: “Kwa sasa siwezi kueleza chochote kwani vikao ndiyo vinafanyika kwa sasa, lakini naomba vikao vikishamalizika viongozi wetu watazunguza tu,” alisema.
Alipoulizwa juu ya NLD kuhitaji majimbo matano, Kigaila alikiri kuwa kweli wanataka mgawo wa majimbo lakini alikataa kutaja idadi yake.
“NLD wanayo haki kama vyama vingine, kwa nini wasipate? Watapata, lakini kuna taarifa sahihi zitakazoelezwa baada ya kikao cha leo.”
Jumanne wiki hii, Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Bara, Magdalena Sakaya alilieleza gazeti hili kuwa kikao hicho kitakuwa na ajenda ya kukusanya maoni na mapendekezo ya wanachama, kujadiliana kwa pamoja ili kufikia muafaka wa majimbo hayo.
Katibu Mkuu wa NCCR-Mageuzi, Mosena Nyambabe alisema katika hatua za kutafuta maridhiano ya majimbo hayo, vyama vyote vinapaswa kutambua kila nafasi ya chama kilichoshiriki kwenye makubaliano ya Ukawa.
“Tukifuata kanuni, nadhani kuna vyama ambavyo havitakuwa na nafasi Ukawa na haitakuwa na maana ya kuungana, kwa hivyo lazima busara itumike zaidi. Haiwezekani chama fulani kilazimishe kuchukua majimbo mengi kuliko kingine,” alisema Nyambabe.
Alipoulizwa kuhusu utata katika mgawanyo wa majimbo, Dk Slaa alisisitiza kumalizika kwa mvutano kutokana na busara za viongozi wa vyama hivyo.
MWANANCHI

No comments

Powered by Blogger.