Swala hili limekuwa likiwatatiza wamama wengi wanaopatwa na tatizo la mimba kuharibika.
Ni vizuri kwanza kujua vitu vinavyoweza kusababisha mimba kuharibika.
Mimba nyingi huharibika kutokana na makosa ya ukuaji wa mtoto. Sehemu
kubwa ya makosa haya huwa ni kwenye vinasaba vyake. Yanaweza kuwa ya
kurithi au yasiyo ya kurithi yaliyotokea kwa bahati mbaya kwa mtoto.
Zipo pia sababu nyingine kama vile maumbile ya viuongo vya uzazi,
magonjwa ya mama kama vile kisukari, magonjwa ya damu, magonjwa ya
vijidudu (infection).
Pamoja na sababu za mimba kuharibika kuwa
nyingi, mara nyingi linapotokea tatizo hili huwa sababu iliyosababisha
haifahamiki. Hali hii husababisha akinamama wengi na wenza wao kubaki na
maswali mengi kwanini imewatokea hivyo na hujiuliza kama inaweza
kutokea tena kwenye ujauzito mwingine.
Mara nyingi hali hii
hutokea mara moja na haijirudii. Hii ni kwa sababu makosa ya ukuaji
yanayotokea bahati mbaya huwa ni jambo lenye uwezekano mdogo sana
kujirudia. Hata hivyo iwapo ujauzito umeharibika kwa sababu nyingine
kama vile za kimaumbile au magonjwa ya damu, uwezekano wa kujirudia huwa
mkubwa iwapo hali hiyo haijagundulika na hatua stahiki kuchukuliwa.
Kujibu swali la msingi ni baada ya muda gani inafaa kubeba mimba
nyingine, inategemea kama ni mara ya kwanza ujauzito kubadilika au ni
hali iliyojorudia. Kama ni mara ya kwanza, unaweza kubeba ujauzito
mwingine mara tuu unapopata siku zako (vizuri zaidi angalau baada ya
wiki 6 baada ya ujauzito kuharibika). Kwa kipindi hiki mwili unakuwa
tayari kupokea ujauzito mwingine.
Hata hivyo kwa vile swala la
ujauzito kuharibika linapokelewa kwa hisia tofauti na linaowakuta, ni
vizuri ukabeba ujauzito baada ya kuwa umeshakuwa katika hali ya kawaida
kihisia.
Iwapo ujauzito kuharibika sio mara ya kwanza, kuna
umuhimu wa kufanyiwa vipimo na daktari ili upewe ushauri juu ya
kujiandaa na ujauzito mwingine. Aina ya ushauri inategemea na matokeo ya
vipimo atakavyoshauri daktari. Vilevile inategemea kama ujauzito
(mtoto) ulioharibika ulikutwa na tatizo lolote linalohitaji muda
kulichunguza. Vipimo hivi vinaweza kuwa pamoja na vipimo vya damu,
kipimo cha ultrasound na vingine.
Daktari anaweza kushauri utumie dawa za folic acid au vitamin wakati ukijiandaa na ujauzito mwingine.
Wanawake wengi (asilimia 70) waliopata tatizo la ujauzito kuharibika
walifanikiwa kupata ujauzito tena na kujifungua watoto wenye afya njema.
Kwahiyo usikate tamaa iwapo umekutwa na hali hii.
IMEANDALIWA NA DOCTOR JOH BLOG
No comments:
Post a Comment