HABARI

Theme images by kelvinjay. Powered by Blogger.

MATUKIO

MICHEZO

SIASA

» »Unlabelled » CHADEMA yailiza CCM Ubungo

WAKATI Watanzania wakisubiri kwa hamu hatima ya rufaa ya aliyekuwa Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema, Mahakama ya Rufani nchini, imetoa amri ya kuiondoa rufaa iliyokuwa imekatwa na aliyekuwa mgombea ubunge wa Jimbo la Ubungo, Hawa Ng’umbi (CCM) dhidi ya Mbunge wa jimbo hilo, John Mnyika (CHADEMA) baada ya kuridhia maombi ya pande zote mbili zilizoomba mahakama hiyo kuiondoa mahakamani.
Majaji watatu wa Mahakama ya Rufani; Natalia Kimaro, Salum Massati na Catherine Oriyo waliketi jana jijini Dar es Salaam kwa ajili ya rufaa hiyo iliyokuwa ikipinga hukumu iliyotolewa na Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, katika kesi ya kupinga ubunge wa Mnyika iliyofunguliwa na Ng’umbi.
Jaji wa Mahakama Kuu Upendo Msuya mwaka huu, katika hukumu yake alitupilia mbali kesi hiyo ya Ng’umbi kwa madai kuwa alishindwa kuleta ushahidi thabiti ambao unaonyesha taratibu na sheria za uchaguzi zilikiukwa katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 ambao ulimtangaza Mnyika kuwa ni mbunge halali wa jimbo hilo.
Jana, Jaji Kimaro alisema anaiondoa rufaa hiyo iliyokuwa ikipinga hukumu hiyo iliyotolewa na Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.
“Kwa kuwa mwomba rufaa (Ng’umbi) na mjibu rufaa (Mnyika) kabla ya leo kuja hapa mahakamani walikutana nje ya mahakama na kufikia uamuzi wa kuiondoa bila gharama rufaa hii ambayo leo ilikuja kwa ajili ya kuanza kusikilizwa, na leo mawakili wao wamewasilisha ombi hilo mbele ya mahakama hii, basi mahakama hii inakubali ombi lao hilo na inatoa amri ya kuiondoa rufaa hii chini ya 102(3) na (4) cha Kanuni za Mahakama ya Rufani nchini,” alisema Jaji Kimaro.
Awali kabla ya kutolewa kwa amri hiyo ya mahakama, wakili aliyekuwa akiwawakilisha wajibu rufaa wengine ambao ni Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Ubungo, na Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambao walikuwa wakitetewa na wakili wa serikali, Obadia Kameya wakati mjibu rufaa wa kwanza alikuwa akitetewa na Edson Mbogoro, walianza kwa kuikumbusha mahakama kuwa kesi hiyo jana ilikuja kwa ajili ya kusikilizwa rufaa na kwamba wapo tayari kwa ajili ya kuendelea.
Lakini wakili wa Ng’umbi alisimama na kujitambulisha, na kisha akaeleza kuwa siku mbili zilizopita mteja wake alikutana na Mnyika kufanya mazungumzo ambayo yalihitimishwa kwa kukubaliana kuwa rufaa hiyo waiondoe mahakamani, na kwamba amemwelekeza awasilishe ombi hilo la kuomba rufaa hiyo iondolewe mahakamani bila gharama.
Baada ya kuwasilisha ombi hilo, mawakili Kameya na Mbogoro walieleza kuwa hawana pingamizi na ombi hilo na kwamba wanaiachia mahakama iamue.
Baada ya Jaji Kimaro kumaliza kutoa amri hiyo, Mnyika ambaye jana alikuwepo mahakamani hapo huku Ng’umbi akishindwa kufika, aliwaeleza waandishi wa habari nje ya mahakama kuwa amefurahishwa na uamuzi huo.
“Ni wakili wa Ng’umbi ndiye alimpigia simu wakili wangu Mbogoro wakutane ili wazungumzie ombi la Ng’umbi la kutaka kuiondoa rufaa yake aliyoikata dhidi yangu, na kisha mawakili wetu wakaja kunikutanisha mimi na Ng’umbi tukazungumzia ombi hilo na tukakubaliana na ombi lake lililotaka aiondoe rufaa yake,” alisema Mnyika huku akiwa amezingirwa na umati wa wafuasi wake.
Aidha, wafuasi wa Mnyika, wengine wakiwa wamebeba bandera za CHADEMA, waliondoka katika eneo la Mahakama ya Rufaa kwa maandamano, huku wakiimba nyimbo za kupongeza uamuzi huo na kumsifia mbunge huyo ambaye kwa sasa atakuwa hakabiliwi tena na kesi ya kupinga ubunge wake katika mahakama yoyote hapa nchini.

Mnyika kulipua mafisadi leo
Wakati huo huo, Mnyika alisema kuwa leo atawalipua na kutangaza waziwazi majina ya vigogo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambao alidai walishiriki kuhujumu mali za viwanda vya nguo vilivyoko katika jimbo lake.
Mnyika alisema atafanya hivyo, atakapokuwa katika ziara ya siku mbili katika jimbo hilo inayoanza leo, huku akiweka wazi kutofumbia macho tena kuhusiana na hujuma ya baadhi ya watendaji wa Serikali ya CCM.
“Kesho (leo Jumamosi) nitaanza ziara katika Kata ya Manzese kukagua viwanda vilivyouawa na serikali ya CCM, na nitataja majina ya vigogo wa CCM waliofanya ufisadi hadi kuua viwanda na kusababisha vijana kukosa ajira,” alisema.
Mnyika alisema Mwalimu Nyerere katika utawala wake alikazania na kuanzisha viwanda kwa ajili ya kuokoa na kusaidia ajira kwa vijana, lakini baadhi ya viongozi mafisadi wa CCM walikula njama na kuvifilisi.
Aliongeza kuwa, kesho, akiwa katika Kata ya Ubungo, atalipua ukweli wote wa hujuma kubwa zilizofanywa na watendaji wa serikali katika Shirika la Ugavi wa Umeme (TANESCO).

Alisema kuwa amesikia Jumatatu wiki ijayo, TANESCO watafanya mkutano wa kutaka kupandisha bei ya umeme, na akawataka wakazi wa Ubungo kushiriki na kupinga jitihada zozote za kuongeza bei ya nishati hiyo.
“Bei ya sasa ni balaa kwa Watanzania wanyonge, lakini bado tena wanataka kuongeza mzigo kwa wananchi jambo ambalo hatuwezi kulikubali,” alisema Mnyika.

CHANZO: TANZANIA DAIMA

«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post

No comments: