VURUGU kubwa za kurushiana ngumi zimetokea na kusababisha watu
kadhaa kujeruhiwa katika zoezi la ukusanyaji maoni ya Katiba mpya
katika majimbo ya Magomeni na Mpendae mjini Zanzibar.
Kwa mujibu wa Kamishina wa tume ya kukusanya maoni, Profesa Mwasiga
Baregu, vurugu za kwanza zilitokea juzi katika viwanja vya Mzalendo
Magomeni na zingine katika Uwanja wa Mpendae katika wilaya ya mjini
Zanzibar.
Alisema chimbuko la vurugu hizo ni watu wanaokwenda kutoa maoni
wakiwa wamepakiwa katika magari kushutumiwa kwamba ni mamluki kwani sio
wakaazi halali wa maeneo hayo.
Alisema vurugu hizo zilitokea majira ya saa 8 mchana na kusababisha
tume kusitisha kazi ya kukusanya maoni kwa sababu za kiusalama.
Alisema wananchi katika maeneo hayo, walianza kulalamika kuwa uwanja
wa kutoa maoni umevamiwa na mamluki ambao sio wakaazi halali wa majimbo
ya Magomeni na Mpendae mkoa wa mjini Magharibi, Unguja.
“Kazi ya kukusanya maoni imekwama mara mbili baada ya kujitokeza
vurugu katika vituo vya kutolea maoni Zanzibar,”alisema Profesa Baregu.
Hata hivyo alisema Tume itaendelea na ratiba yake kama kawaida katika
maeneo mengine na kuwataka wananchi kujitokeza kutoa maoni yao.
Alisema tangu tume yake ianze kukusanya maoni katika wilaya ya Mjini,
kumejitokeza ushindani mkubwa kati ya watu wanaotaka mfumo wa Serikali
ya Muungano wa mkataba na wale wanaotaka mfumo wa sasa wa Muungano wa
Serikali mbili kuendelea kutumika katika Muungano wa Tanganyika na
Zanzibar.
Alisema ushindani huo umesababisha baadhi ya watu kujitokeza kutoa
maoni zaidi ya mara moja kitendo ambacho ni kinyume na sheria ya tume ya
mabadiliko ya Katiba ya Muungano ya mwaka 2012.
“Wananchi wamekuwa wakilalamika kuna makundi ya watu ambao sio wakaazi
wanavamia mikutano na kutoa maoni zaidi ya mara moja kinyume na
sheria,” alisema Profesa Baregu.
Hata hivyo alisema kwamba Tume yake ilikuwa na nafasi ya kuendelea
kukusanya maoni baada ya kuimarisha ulinzi wa polisi, lakini hawakutaka
kufanya hivyo kwa vile tume haitaki wananchi kutoa maoni wakiwa chini ya
ulinzi wa askari wenye silaha, ndiyo maana wameamua kutumia askari
kazu tangu kuanza kukusanya maoni yao Zanzibar.
Wakati huo huo Chama cha wananchi CUF kimelaani vurugu hizo na kutoa
shutuma kali kwa Kamishina wa tume hiyo, Fatma Said Ali kuwa yeye na
mwakilishi wa jimbo la Magomeni CCM, Salmin Awadhi ndiyo chanzo cha
vurugu hizo.
Hata hivyo viongozi hao hawakuweza kupatikana kuelezea shutuma hizo
jana lakini Mkurugenzi wa haki na Binadamu Habari na Uenezi wa CUF,
Salum Bimani alisema viongozi hao waliwanyima wananchi haki ya kikatiba
ya kutoa maoni na kusababisha vurugu.
Alisema wakati umefika kwa tume hiyo kufanya kazi kwa kuzingatia
sheria ya kuanzishwa kwa tume hiyo na viongozi kujiepusha na ushabiki wa
kisiasa.
Bimani alisema wananchi wamekuwa wakijitokeza kutoa maoni yao lakini
wamekuwa wakikumbana na vikwazo baada ya kufika katika vituo vya kutoa
maoni kinyume na sheria ya time hiyo.
Kwa upande wake, Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimeomba Tume hiyo kuwa
macho na njama za baadhi ya vyama vya siasa za kuanda makundi ya vijana
wasiokuwa wakaazi katika maeneo husika kwenda kutoa maoni na kusababisha
vurugu.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na katibu
msaidizi wa itikadi na uenezi wa chama hicho, Alli Mwinyi Msuko,
alisema vurugu hizo zimesababishwa na wanasiasa kupandikiza watoa maoni
mamluki.
Tangu tume hiyo ianze kukusanya maoni, wanachama na wafuasi wa CUF
wamekuwa wakitetea Muungano wa serikali tatu ikiwemo ya Tanganyika,
Zanzibar yenye mamlaka kamili na Muungano wa mkatba wakati wanachama wa
CCM wakitetea Muungano wa Serikali mbili katika mabadiliko hayo
http://www.freemedia.co.tz



No comments:
Post a Comment