HABARI

Theme images by kelvinjay. Powered by Blogger.

MATUKIO

MICHEZO

SIASA

» »Unlabelled » Asha Musa: Nisaidieni nakufa

Mtoto wa Asha.  
Na Shakila Nyerere 

KULINGANA na taarifa za kila mwaka za Umoja wa Mataifa (UN) kabla na hata baada ya uhuru, Tanzania haijawahi kujiondoa katika kundi la mataifa maskini sana duniani licha ya kuwa na wingi wa rasilimali nyingi zikiwamo madini.
Umaskini umekuwa na athari nyingi kwa Serikali na hata jamii kwa ujumla, mojawapo ni watu wenye hali hiyo kushindwa kumudu gharama za kuendesha maisha yao ya kila siku.
Katika maeneo mengi nchini kumekuwa na watu ambao kwenda hospitali ni suala gumu hata awe anaumwa kiasi gani, sababu kubwa ni kutokuwa na fedha za kulipia gharama za matibabu.
Hivi karibuni iliripotiwa mkoani Njombe baadhi ya wagonjwa wanaopelekwa hospitali kukimbia bila kulipia gharama wanapokuwa na unafuu au kupona. Sababu kubwa ni kutokuwa na fedha.

Nini hatma ya hali hii nchini? Ni swali lisilo na jibu.
Mkoani Dodoma katika wilaya ya Kondoa, kuna mwanamke, Asha Musa (16) ambaye anasema anaona dalili za kufa kutokana na kushindwa kupata fedha kwa ajili ya kutibu tatizo linalomsumbua.
“Nisaidieni ndugu zangu ninakufa kutokana kutokuwa na uwezo wa kujitibia pamoja na mfarakano wa wazazi wangu,” Asha alianza kulia kwa uchungu.
Kuhusu ugonjwa wa Asha
Asha ni mtoto wa kwanza katika familia ya watoto watatu, alizaliwa mwaka 1995 na alianza kuugua akiwa shule ya msingi darasa la sita mwaka 2008, katika shule ya Ubembeni, iliyoko Kondoa.
“Ilianza kama kipele na baadaye kikawa kama tezi katika eneo la paja, ndipo nilipomchukua na kumpeleka hospitali ya wilaya, akawa amefanyiwa upasuaji mdogo, kisha aliendelea na shule hadi alipomaliza darasa la saba na bahati nzuri alifaulu kujiunga na kidato cha kwanza shule ya sekondari Bicha,” alisema mama yake Asha.
Aliendelea na masomo hadi alipofika kidato cha pili ndipo  Asha alipata ujauzito na kubaki nyumbani akilea uja uzito wake, baadaye alijifungua mtoto wa kiume.
“Baada ya kujifungua tu, alianza tena kuumwa, tulikwenda katika zahanati na hospitali mbalimbali, bila mafanikio, ndipo tuliandikiwa karatasi ya kwenda hospitali ya Mkoa wa Dodoma lakini kutokana na uwezo mdogo kifedha tulishindwa kumpeleka.
“Tuliendesha mchango, hata hivyo tulipata fedha kidogo ambazo kutokana na hali ngumu ya maisha tulijikuta nazo tunazitumia kwa matumizi ya nyumbani. Nakumbuka zilipatikana Sh70,000, ambazo zilikuwa zililetwa na wasamaria kwa nyakati tofauti,” anafafanua.
Akizungumzia hali inayomsumbua, Asha anasema “Nikiwa darasa la sita katika shule ya Ubembeni nilijikuta natokewa na kitu kama kipele kwenye paja, kiliendelea hadi kuwa kama tezi ndipo nilipostuka na kumueleza mama.
“Baadaye alinichukua na kunipeleka hospitali ya wilaya kufanyiwa vipimo. Huko walinifanyia upasuaji mdogo kuondoa ule uvimbe,” anasema Asha huku akitokwa na machozi.
Anasema baadaye ilionekana kama amepona lakini baada ya kupata uja uzito na kujifungua alishangaa hali inamrudia kwa sehemu iliyofanyiwa upasuaji kuota nyama.
Anasema huo ulikuwa ni mwanza wa matatizo ambayo yalikuwa yakiongezeka siku hadi siku na hatimaye kujikuta ameota nyama ambayo kwa kukisia inaweza kufikia kilo tano.

Afukuzwa nyumbani
Asha anafikiri kuwa kwa kiasi kikubwa umaskini na ugomvi wa mara kwa mara wa wazazi wake umechangia kuwa na hali hiyo kwa sababu walikataa kumlipia karo na katika kuzunguko huko na kule akajikuta analazimishwa kufanya ngono ili kukidhi mahitaji.


“Nikiwa kidato cha pili katika shule ya sekondari Bicha siku moja nilifukuzwa kwa sababu sikuwa na uwezo wa kulipa karo, niliporudi nyumbani kuwaeleza wazazi wangu niliambulia kupigwa na kufukuzwa kwa wazazi wangu, hii ni kwa sababu nao walikuwa wana ugomvi usioisha.
“Miezi kadhaa baadae walitengana na baba akaoa mke mwingine, tukawa tunaishi na baba na mama wa kufikia. Mama yangu mzazi naye akawa anaishi na baba mwingine,” anasisitiza Asha.
Anasema hali hiyo ilisababisha asipate mahitaji mbalimbali ya shule hivyo akajikuta anaingia kwenye mtego wa wanaume walaghai ambao walimfanya ajikute anapata uja uzito.
Anasema hali ilikuwa mbaya zaidi baada ya kujifungua kwani alijikuta anafukuzwa nyumbani.  
“Baada ya kujifungua hali ndio ilizidi kuwa mbaya kwa kuwa  nilitengwa na wazazi wote, baba na mama yangu wa kufikia ambao nilikuwa naishi nao waliondoka eneo hilo na kuhamia eneo jingine, sikuwa na pa kuishi, nikawa ni mtu wa kubangaiza.
“Kila ninapofikiria hivyo, roho inauma sana kwani ni maisha ya ajabu mno ambayo nimekuwa nikiishi. Sijui ni kwanini nimekuwa ni mtu wa mateso katika maisha yangu,” anahoji huku akilia.
Asha anaeleza namna anavyopata shida ya kumlea mtoto huyo, ambaye pia amekuwa akihitaji mahitaji mengi, ambayo kwake imekuwa ni shida kumpatia kwa kuwa hana uwezo wa  kifedha kufanya hivyo.
Asha hana uwezo wa kutembea kutokana na ugonjwa unaomsumbua ambao haujulikani hadi sasa kwa kuwa hana uwezo wa kwenda hospitali kutibiwa.
Kama ukifanikiwa kumuona unaweza kuangua machozi, kwani hata sehemu ambayo analala ni chafu, huku kukiwa hakuna dalili yoyote ya kuondoka kwenye hali hiyo ngumu.

Maisha ya Asha
Nyumba anayoishi Asha haina dirisha la kuingiza ndani hewa ya kutosha na kuna wakati analazimika kujisaidia ndani kwa vile hana uwezo wa kutembea.
Msaada mkubwa wa Asha ni wasamaria wema ambao wakati mwingine huwa na mambo mengine, hivyo kushindwa kwenda kumsaidia.
Hali huwa ni mbaya zaidi pale ambao huwa amejisaidia ndani halafu hakuna wa kumsaidia kuondoa uchafu huo.
Anasema kwa sasa anachohitaji ni msaada wa fedha kwa ajili ya kuchunguzwa kwa undani zaidi tatizo linalomsumbua.
Anasema kila kukicha hali yake inakuwa mbaya zaidi na sasa amejikuta anapoteza uwezo wa kutembea, jambo linalomfanya awe tegemezi.



MWANANCHI

«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post

No comments: