Makada CCM wakata rufaa ubunge wa Lema
Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema
Kwa mujibu wa taarifa za kimahakama, makada hao waliwasilisha
maombi yao Februari 13, mwaka huu chini ya hati ya dharura wakitaka
yasikilizwe haraka.
Desemba
21, mwaka jana Mahakama ya Rufaa ilimrejesha tena Lema bungeni baada ya
kukubali rufaa yake dhidi ya hukumu ya Mahakama Kuu Kanda ya Arusha
iliyomvua ubunge wake.
Makada hao waliolalamikia ushindi wa Lema wakiwa ni wapigakura wa
Jimbo la Arusha Mjini, wanadai kuwa na sababu sita za kutaka mahakama
hiyo ipitie uamuzi wake kwa madai kuwa kuna maeneo ambayo hayakuamuliwa
vizuri. Jana NIPASHE ilizungumza na Wakili wa Lema, Method Kimomogoro,
ambaye alithibitisha kuwa na taarifa za maombi hayo na kuahidi kutoa
ufafanuzi baadaye.
Naye wakili wa wanachama wa CCM, Alute Mughway, jana alithibitisha kuwa wateja wake wamewasilisha maombi hayo Mahakama ya Rufaa.
Wanachama hao wa CCM, ambao ni Mussa Mkanga, Happy Kivuyo na Agnes
Mollel, walifungua kesi dhidi ya Lema katika Mahakama Kuu Kanda ya
Arusha, kupinga ushindi wake alioupata katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka
2010.
Walikuwa wakidai kuwa katika kampeni zake, Lema alikuwa akitumia
lugha za matusi, kejeli na ubaguzi wa kijinsia dhidi ya aliyekuwa
mgombea wa CCM, Dk. Batilda Buriani.
Kufuatia kesi hiyo, Lema alivuliwa ubunge na mahakama hiyo, Aprili
5, mwaka huu, katika hukumu iliyotolewa na Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya
Sumbawanga, Gabriel Rwakibarila, aliyesikiliza kesi hiyo. Jaji
Rwakibarila aliisikiliza kesi hiyo baada ya Jaji Aloyce Mujulizi
aliyekuwa amepangiwa kuisikiliza kesi hiyo kujitoa kufuatia ombi la
Lema kuwa hakuwa na imani naye.
Hata hivyo, baadaye mwishoni mwa mwaka jana, Lema kupitia mawakili
wake, Kimomogoro na Tundu Lissu, alikata rufaa kupinga hukumu hiyo
iliyomvua ubunge wake.
Hukumu ya kumrejeshea ubunge Lema ilitolewa na jopo la majaji
watatu wa Mahakama ya Rufaa, wakiongozwa na Nathalia Kimaro. Wengine ni
Salum Massati na Bernard Luanda.
CHANZO:
NIPASHE
Post a Comment