Na John Banda,Dodoma.
HALMASHAURI za wilaya na Manispaa hapa nchini
zimetakiwa kutenga vituo vya waendesha bodaboda kama ilivyo kwenye vituo vya
teksi ili kuweza kuzuia uhalifu miongoni mwa madereva hao.
Rai hiyo imetolewa na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika
lisilo la kiserikali la Asasi inayojishughulisha na Rasilimali (Resources
Network Foundation) (RNF) Ombeni Msuya kwenye hafla ya kuwasimika rasmi
na kuwaaga waratibu wa shirika hilo wa Mikoa na Wilaya hapa nchini.
Msuya alisema vijana waliojiajiri kwenye biashara ya
bodaboda ni wengi na ndiyo nguvu kazi ya Taifa hivyo ni wajibu wa uongozi wa
halmashauri za wilaya na Manispaa hapa nchini kuwatengea maeneo maalum ya
kufanyia biashara zao ili kuzuia uhalifu.
Alisema ikiwa waendesha bodaboda watakuwa na vituo
maalum vya kufanyia kazi zao wahalifu wanaotumia mgongo wa bodaboda
watafahamika na hivyo vitendo vya uhalifu vinavyofanywa na watu
wanaojifanya ni madereva wa bodaboda vitakomeshwa.
“Hawa vijana waliojiajiri kwenye biashara ya
bodaboda mimi huwa nawaita ni jeshi kubwa la ardhini kwa sababu wako kila kona
ya Tanzania na ndiyo biashara ambayo hivi sasa vijana wengi wameweza kuajiriwa
na kujiajiri hapa nchini hivyo Halmashauri na Manispaa zinatakiwa kuwatambua,”
alisema Msuya.
Endelea kusoma habari hii kwa kubofya hapa chini
Aidha Mkurugenzi huyo amezishauri Halmashauri na
Manispaa kuwapatia waendesha bodaboda hizo namba ili waweze kutambuliwa
kirahisi pamoja na kuziweka alama pikipiki zao wanazofanyia kazi kwa lengo la
kuwatambua zaidi hata pale inapotokea uhalifu na ajali badala ya kuwaacha
wakifanya kazi zao kiholela.
Mbali na hilo Msuya aliwashauri waratibu hao kutumia
fursa watakazokutana nazo katika maeneo yao katika kujipatia kipato chao cha
kila siku kuliko kusubiri ajira kutoka serikalini.
Hafla hiyo iliwakutanisha vijana waliomaliza vyuo
vikuu mbalimbali hapa mkoani Dodoma ambao ni wanachama wa RNF kwa ajili ya
kwenda kufanya kazi za shirika hilo sehemu mbalimbali ikiwemo mijini hadi
vijijini.



No comments:
Post a Comment