HABARI

Theme images by kelvinjay. Powered by Blogger.

MATUKIO

MICHEZO

SIASA

» »Unlabelled » KAULI YA MWISHO YA ‘MTOTO WA BOKSI’

Mtoto aliyekuwa amefichwa kwenye boksi kwa miaka mitatu mfululizo Morogoro,Nasra Rashid (4),akiwa kwenye Wodi B ya Hospitali ya Taifa ya Muhimbili(MNH)alikohamishiwa kwa matibabu zaidi. Picha na Beatrice Moses.
Mtoto Nasra Rashid Mvungi (4), aliyefichwa kwenye boksi kwa miaka minne, amefariki dunia katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) na katika saa zake za mwisho za uhai wake alisikika akitamka maneno “sitaki waje kunichukua”.
Nasra ambaye alikuwa akitibiwa MNH, alifariki dunia usiku wa kuamkia jana baada ya hali yake kubadilika Alhamisi iliyopita, kiasi cha kuhamishiwa katika chumba cha uangalizi maalumu (ICU) ambako aliwekewa mashine ya kumsaidia kupata hewa ya oksijeni.
Mama mlezi wa Nasra, Josephine Joel alisema kabla hajawa mahututi, mtoto huyo alikuwa akiweweseka kwa kuzungumza maneno mengi hali iliyosababisha wauguzi kumfanyia ibada maalumu.
ENDELEA KUSOMA HABARI HII KWA KUBOFYA HAPA CHINI
“Sitaki waje kunichukua, sitaki, sitaki, wasije kunichukua, bibi Nasra umesikia,” ni maneno aliyokariri mlezi huyo ambayo yalikuwa yakirudiwarudiwa na Nasra saa chache kabla ya hajawa mahututi na kupelekwa ICU.
Josephine alisema mtoto huyo pia kila mara alikuwa akidai apewe chips na soda na kwamba hadi mauti yalipomkuta alikuwa akitibiwa maradhi ya homa ya mapafu ‘nemonia’.
“Nasra alifariki saa 7.30 usiku, tangu Alhamisi iliyopita hali yake ilibadilika na kuwa mbaya na imeendelea kuwa hivyo hadi alipofariki dunia,” alisema na kuongeza:
“Bado niko Muhimbili nawasubiri watu wa ustawi wa Jamii kutoka Morogoro wao ndiyo watakuwa na uamuzi kuhusu mazishi ya mtoto huyo,” alisema.
Ofisa Habari wa MNH, Aminiel Eligaeshi alithibitisha kifo cha mtoto huyo, ambaye alipokewa hospitalini hapo Mei 26 mwaka huu akitokea Morogoro na kwamba hali yake ilibadilika ghafla juzi saa 2:00 usiku.
“Jitihada za madaktari zilifikia kikomo saa 7:30 usiku, baada ya mtoto huyo kupoteza maisha,” alisema.
Kuzikwa kishujaa
Ofisa ustawi wa jamii Mkoa wa Morogoro, Oswin Ngungatuti alisema mwili wa mtoto huyo utasafirishwa leo kwenda Morogoro.
Ngungamtitu alisema mazishi ya Nasra yatatanguliwa na ibada itakayoambatana na utoaji wa heshima za mwisho katika Uwanja wa Jamhuri, hatua ambayo alisema inatokana na baba mzazi wa mtoto huyo, Rashid Mvungi kuwa mmoja wa watuhumiwa wa mateso yake.

Hata hivyo, Mvungi licha ya kushiriki vikao vilivyopanga mazishi ya Nasra, jana alisema angefurahi kama angepewa mwili wa mtoto wake ili auzike mwenyewe badala ya kuzikwa na Serikali.
“Tayari mimi na familia yangu akiwamo mke wangu tulishakubaliana kumlea na nilipanga baada ya kupona niwaombe ustawi wa jamii ili nimlee mwenyewe, lakini leo nilipopata taarifa hizi kwa kweli nimechanganyikiwa na sijui cha kufanya.’’
Katika kikao cha mazishi, Mkurugenzi wa Kampuni ya Mabasi ya Al Saed, Omary Al Saed alisema kampuni yake itatoa gharama zote za mazishi kuanzia kusafirisha mwili wa marehemu kwenda Morogoro na gharama nyingine.
Wadau wengine ambao walitoa michango yao ni Mwenyekiti wa Chama cha Soka Mkoa wa Morogoro (MRFA), Pascal Kianga na Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro.
Mateso ya Nasra
Nasra alifichwa katika boksi na mama yake mkubwa, Mariam Said mkazi wa Uwanja wa Ndege, Morogoro tangu akiwa na miezi tisa.
Alianza kumlea mtoto huyo baada ya mdogo wake ambaye ni mama yake Nasra kufariki dunia. Majirani wa Mariam ndiyo waliotoa taarifa za kuwepo kwa mtoto huyo baada ya kumsikia akilia na kukohoa nyakati za usiku.
Mwanamke huyo, Mvungi na mume wa Mariam, Mtonga Omar wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi wa Morogoro kujibu mashtaka ya kula njama na kufanya ukatili dhidi ya mtoto huyo.
Jana Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, John Laswai alisema kutokana na kifo cha Nasra, mashtaka dhidi ya watuhumiwa yanaweza kubadilika, lakini mabadiliko hayo yatategemea ripoti ya daktari kuhusu sababu za kifo hicho.
Laswai alisema taratibu za kipolisi zinafanywa kuwezesha  kupatikana kwa taarifa hiyo, ambayo itapelekwa kwa wanasheria ambao baada ya kuipitia wanaweza kuwa na mapendekezo ya kubadili mashtaka dhidi ya watuhumiwa hao.
Imeandikwa na Hamida Sharifu, Joseph Zablon na Raymond Kaminyoge
MWANANCHI

«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post

No comments: