Zaidi ya wakulima 250 wa kijiji cha Bahi sokoni wamevamia na kujigawia mashamba kienyeji yaliyozuiliwa kutumika kutokana na mgogoro wa mpaka kati yao na majirani zao wa kijiji cha Mpamwantwa wakidai kuchoshwa na kusubiri suluhisho kwani wameshindwa kufanya shughuli za kilimo kwa miaka tisa hali inayowaathiri kiuchumi na kimaendeleo.
Wakulima hao wanadai waligawiwa mashamba hayo kwa ajili ya kilimo cha Korosho miaka tisa iliyopita lakini walizuiliwa kuendelea na kilimo baada ya wenzao wa kijiji cha Mpamantwa kudai eneo hilo ni lao na mpaka sasa haijapatikana suluhu juu ya mgogoro hali iliyowafanya wachoke kusubiri na kuamua kuchukua hatua hiyo.
Macheti Miliyanzoka ni mwenyekiti wa kijiji hicho anaelezea historia ya eneo hilo ambalo anasema lilitolewa na kijiji baada ya agizo la aliyekuwa mkuu wa mkoa wa Dodoma wakati huo Mhe. William Lukuvi aliyetaka kuanzishwe kilimo cha mikorosho na baadhi wakulima wakaitikia na kupanda zao hilo kabla ya kuibuka kwa mgogoro huo.
Kwa upande wake afisa ardhi na maliasili wilaya ya Bahi Chediel Mrutu anasema kwa nyakati tofauti wamekutana na pande zote mbili kujadili suala la mpaka na tayari lilishamalizika na kuwataka wakulima hao kufuata taratibu katika kudai mashamba yao ili wasisababishe uvunjifu wa amani.
Chanzo: ITV Tanzania
No comments:
Post a Comment