Watu wengi wamekuwa wakijiuliza watafanya nini pale wanapopotelewa ama kuharibikiwa na vyeti vyao vya elimu ya sekondari vinavyotolewa na Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA).
Cheti chako kinaweza kupotea kwa bahati mbaya, kuharibiwa (mfano kuliwa na mchwa, panya au wadudu wengine) au pia kuungua moto. Ukikumbwa na majanga haya, usiogope kwani Baraza la Mitihani Tanzania lina mbadala wa kukupatia cheti chako ili uweze kuendelea kukitumia katika masomo na hata maombi ya kazi na shughuli nyingine zitakazokuwa zinakuhitaji wewe kutumia cheti chako.
Unapogundua kuwa umepoteza cheti chako, ama kimeharibika ama kuungua moto fuata hatua zifuatazo:
Mhitimu aliyepoteza cheti chake atapaswa kwenda kutoa taarifa ya upotevu wa cheti chake katika kituo chochote cha polisi kilicho karibu.
Baada ya kupewa ‘lost report’, mhitimu atapaswa kutangaza kupotelewa kwa cheti chake katika gazeti lolote linalochapishwa hapa nchini na kutakiwa kungoja kwa muda wa miezi mitatu.
Lengo la kutangaza ni ili kusaidia kupatikana kwa cheti halisi kama tu kiliokotwa ama kipo kwa mtu mwingine. Na hili ni katika kuhakikisha kuwa hakuwi na vyeti viwili vya mtu mmoja vinavyotumika kwa pamoja.
Mhitimu atatakiw kujaza fomu ya ombi la cheti mbadala au uthibitisho wa matokeo na kuiwasilisha katika Baraza la Mitihani Tanzania. Fomu hiyo inapatikana kwenye ofisi za Baraza la mitihani na pia kwenye tovuti ya baraza ambayo ni www.necta.go.tz
Baraza la Mitihani Tanzani hufanya uchunguzi wa uhalali wa umiliki wa cheti husika na kutoa huduma stahiki. Wahtimu waliofanya mtihani kuanzia mwaka 2008 ambao vyeti vyao vina picha, hupatiwa vyeti mbadala (Duplicate certificate) na waliofanya mitihani kabla ya mwaka 2008 hupatiwa uthibitisho wa matokeo, ambao hutumwa kwa waajiri wao au mahali pengine kwa mahitaji yaliyotolewa na muombaji, hivyo ombi hili la pili hawapewi cheti mbadala.
Cheti mbadala kinachotolewa ni cheti halisi, hata hivyo kinaongezewa maandishi yanayosomeka ‘duplicate’ kuonyesha kuwa cheti hicho kimetolewa kwa mara ya pili.
Endapo cheti cha awali kitapatikana, mhitimu anapaswa kutoa taarifa katika Baraza la Mitihani.
Hapa chini ni fomu ya maombi ya cheti mbadala inayotolewa na NECTA.
No comments:
Post a Comment