HABARI

Theme images by kelvinjay. Powered by Blogger.

MATUKIO

MICHEZO

SIASA

» » MADHARA YA MATUMIZI MABAYA YA STEROIDS ZA KUPAKA KWENYE NGOZI.

Dawa za kupaka zenye steroidi ni zile zenye kutibu magonjwa ya ngozi kukakamaa na kuwa kavu (kwa kitaalam eczema), pia aina nyinginezo za magonjwa ya ngozi yasiyo ya uambukizi. Kama zilivyo dawa nyingine ambazo tunatumia kwa kumeza, dawa hizi za kupaka zenye steroidi huwa na maudhi ya dawa, pia madhara yasiyovumilika zinapotumika vibaya.
Dawa zenye steroidi za kupaka zaweza kugawanywa katika makundi makuu saba, kulingana na uwezo wa ufanyaji kazi wake. Na msingi mkuu wa matumizi ni kutumia kundi lenye uwezo wa chini kadri iwezekanavyo kwa jinsi itakayomfaa mgonjwa.

Kundi la I-Zenye uwezo wa juu kabisa.
  • Bethamethasone dipropionate.
  • Halobetasol propionate.
  • Clobetasol propionate.

Kundi la II-Zenye uwezo wa juu.
  • Mometasone furoate
  • Desoximetasone

Kundi la III, IV, V  na VI-Zenye uwezo wa kati
  • Fluticasone propionate
  • Triamcinolone acetonide
  • Desonide
  •  Fluocinolone acetonide
Kundi la VII-Zenye uwezo wa chini
  • Hydrocortisone
Kumekuwa na wimbi la matumizi ya dawa za kupaka zenye steroidi miongoni mwa wanajamii bila ya kupata ushauri wa wataalamu wa ngozi.Wengi wa watumiaji huzitumia kama vipodozi. Wahanga wakubwa ni wanawake ingawa na wanaume pia wamekuwa wakijihusisha na matumizi mabaya ya dawa hizi. Madhara wapatayo watu hawa wanaotumia dawa hizi zenye steroidi za kupaka kiholela, ni wazi kwa muonekano wa ngozi zao. Pia kuna madhara mengineyo mengi ndani ya mwili ambayo mtumiaji holela anaweza kupata, hii ni kwa sababu dawa hizi pia zina uwezo wa kusharabiwa mwilini.
Dawa hizi za kupaka zenye steroidi huwa hazina madhara endapo mtumiaji atatumia kama alivyoandikiwa na daktari wa ngozi, chini ya uangalizi na ufuatiliaji wa watataalamu wa afya. Dawa hizi za kupaka kwa mfano ni kama Dermovate®, Diprosone®,Sonaderm®,Gentrisone®,Safi®,Elyvate®,Betason®, Betacort® na nyinginezo nyingi.
Image result for TOPICAL STEROIDS
Dawa za kupaka  zenye steroidi husharabiwa mwilini na kuingia katika damu, na kiasi kinachosharabiwa hutegemea na ukubwa wa eneo la ngozi mtu anapaka na kiasi cha dawa anachopaka kwenye ngozi. Zile zenye uwezo wa chini husharabiwa katika maeneo mengine ya ngozi isipokuwa kiganja, lakini zile zenye uwezo wa juu husharabiwa kwenye ngozi na pia katika kiganja. Kiasi kikubwa cha dawa husharabiwa zaidi katika maeneo ambayo ngozi ni nyembamba, mfano karibu na macho, sehemu za siri na sehemu za mikunjo ya ngozi.
Madhara katika ngozi yanayosababishwa na utumiaji holela wa steroidi za kupaka yatategemea na kiasi anachopaka mtumiaji na uwezo wa steroidi anayopaka, lakini madhara haya kwa ujumla ni kama ifuatavyo; kupungua kwa kinga ya ngozi, ambapo itapelekea mtumiaji kupata uambukizi wa fangasi hata bakteria katika ngozi kwa urahisi, na kwa uchache pia malengelenge na hata mkanda wa jeshi. Husababisha matatizo  kama chunusi na ukavu wa ngozi. Ngozi kuwa nyembamba ambayo hupelekea michiri, ngozi kuchubuka kwa urahisi, rashezi kuzunguka mdomo, kupoteza nywele na kuungua jua kwa urahisi. Kutanuka kwa mishipa ya damu, ambayo husababisha kuonekana kwa mishipa ya damu katika ngozi,pia wekundu katika ngozi huonekana mtumiaji anapoacha kutumia.
Dawa hizi zaweza kuleta madhara mwilini endapo zitatumika kiholela.Kiasi kikubwa cha dawa za kupaka zenye steroidi,mojawapo au zaidi kutoka makundi ya steroidi,  husharabiwa katika kiwango ambacho huathiri kazi za tezi ya adrena. Tezi hii inahusika na utengenezaji wa steroidi za asili mwilini, ambazo ni muhimu katika kuiweka miili yetu katika afya njema . Steroidi hizi katika dawa za kupaka zinaposharabiwa na kuwepo mwilini, mrejesho wa taarifa kutoka katika ubongo hupelekwa katika tezi ya adrena, na tezi hii huacha kutengeneza steroidi za asili. Endapo mtumiaji ataendelea kutumia dawa hizi kwa muda mrefu, tezi hii husinyaa kwa kuwa haifanyi kazi kwa muda mrefu. Endapo mtumiaji ataacha kwa ghafla matumizi ya steroidi hii atakuwa mgonjwa na udhaifu wa mwili utakuwa dhahiri,na endapo ataendeleza matumizi ndivyo atazidi kuathirika kadri siku zinavyosonga. Madhara atakayopata mtumiaji holela endapo kiasi kikubwa kitasharabiwa ni ugonjwa ujulikanao kama Cushing syndrome, dalili za ungonjwa ni uso wa mviringo, kuota nundu ya mafuta kati ya mabega.Alama za michirizi katika ngozi ambazo husababishwa na ngozi kuwa nyembamba na kutanuka, au kutanuka kwa mishipa ya damu . Pia kukusanyika kwa maji mwilini(edema), shinikizo la juu la damu, udhaifu wa mifupa na mara chache pia kisukari. Matibabu ya ugonjwa ni uangalizi wa karibu na jinsi ya kumwachisha mgonjwa matumizi ya steroidi, ili kurejesha mfumo wa asili.Matibabu huwa na mafanikio endapo mtumiaji atawahi kutibiwa.

Steroidi katika dawa hizi husharabiwa na kupita placenta. Kwa hiyo mama mjamzito awe makini na kupata ushauri wa daktari. Steroidi pia hutolewa katika maziwa ya mama anayenyonyesha. Uangalizi maalumu huhitajika endapo mama anayenyonyesha atakua anatumia dawa hizi. Kwa watoto, steroidi huathiri ukuaji wa mtoto, kwa hiyo watoto ni kundi ambalo pia huhitaji ungalizi maalumu katika matumizi haya ya dawa za steroidi za kupaka.
Kuna vipodozi vyenye steroidi ambavyo huuzwa kinyume cha sheria, steroidi hizi katika vipodozi hivi hupatikana katika makundi ya steroidi tuliyoyaona awali. Madhara yake ni sawa pia kama tulivyoyaona hapo awali.Kipodozi maarufu ambacho hutumika sana na kinamama ni Caro®light (kipodozi kilichopigwa marufuku). Chukua tahadhari endapo unaamua kubadilisha aina ya kipodozi. Wasiliana na mfamasia au mtaalamu wa ngozi endapo una mashaka na aina mpya ya kipodozi unachotaka kutumia.

Endapo wewe ni mtumiaji holela wa dawa za kupaka zenye steroidi, wahi haraka hospitali au kwa daktari wa ngozi kwa ajili ya ushauri na matibu. Wasiliana na mfamasia wako kwa ushauri juu ya matumizi bora ya dawa za kupaka zenye steroidi. Kamwe usichukue maamuzi mwenyewe, usishawishiwe na rafiki au ndugu kutumia dawa hizi zenye steroidi pasi na ushauri wa daktari wa ngozi. Hakikisha umeelewa maelekezo ya jinsi ya kutumia dawa kwa kuuliza maswali.
Dawa za kupaka zenye steroidi ni zile ambazo mtumiaji hutumia kwa kuandikiwa na daktari, na siyo kununua na kutumia bila kumwona mtaalamu wa ngozi

«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post

No comments: