HABARI

Theme images by kelvinjay. Powered by Blogger.

MATUKIO

MICHEZO

SIASA

MAHAKAMA YA JUU NCHINI KENYA YAFUTA MATOKEO YA UCHAGUZI ULIOMPA USHINDI UHURU KENYATTA

Mahakama ya Juu nchini Kenya imefuta matokeo ya urais yaliyompa ushindi Rais Uhuru Kenyatta kuwa madarakani kwa muhula wa pili.

Mgombea wa Muungano wa Nasa, Raila Odinga alifungua kesi mahakamani kupinga matokeo ya uchaguzi huo uliofanyika Agosti 8, akisema ulitawaliwa na udanganyifu ikiwemo kuchezewa mitambo ya kujumlishia matokeo.

Katika uamuzi wake, Mahakama imesema uchaguzi huo ulikuwa na dosari nyingi, hivyo kukiuka misingi ya uchaguzi huru na wa haki kama ilivyoelekezwa katika Katiba ya nchi hiyo.
 Hii ni mara ya kwanza katika historia ya Taifa hilo kwa Mahakama ya Juu kufuta matokeo ya uchaguzi na inaweka rekodi mpya katika historia ya uchaguzi barani Afrika ndani ya mfumo wa vyama vingi.

Katika uchaguzi uliopita, Odinga alienda mahakamani kupinga matokeo lakini Mahakama hiyo ilitupilia mbali hoja zake na kuridhia matokeo yaliyompa ushindi Rais Kenyatta.
Katika uchaguzi wa Agosti 8, Kenyatta alitangazwa mshindi kwa kupata kura 8,203,290 sawa na asilimia 54.27, huku mpinzani wake Odinga akipata kura 6,762,224 sawa na asilimia 44.74.

Kwa uamuzi uliotolewa na mahakama, uchaguzi mwingine unapaswa kufanyika katika kipindi cha siku 60. Iwapo ushindi wa Kenyatta ungeidhinishwa angepaswa kuapishwa Septemba 12.

Kumekuwa na shamrashamra katika mitaa mbalimbali ya Nairobi na Mombasa kushangilia uamuzi huo, huku Odinga akiwa na wanasiasa wenzake wamepongeza wakisema watatoa taarifa zaidi baadaye.

MAHAKAMA YASEMA YUSUF MANJI ANAKESI YA KUJIBU SAKATA LA MADAWA YA KULEVYA

Mahakama  ya Hakimu Mkazi Kisutu leo August 25, 2017 imesema Mfanyabiashara Yusuf Manji ana kesi ya kujibu katika kesi ya kutumia dawa za kulevya aina ya Heroin.

Uamuzi huo umetolewa na Hakimu Mkazi Mfawidhi Cyprian Mkeha, wakati kesi hiyo ilipoitishwa kwa ajili ya kutolewa uamuzi.

Hakimu Mkeha alisema kuwa ameridhika na ushahidi uliotolewa na mashahidi wa upande wa mashtaka na kwamba mshtakiwa ana haki ya kujitetea kutokana na mkojo wake kukutwa na dawa aina ya Morphine ambayo zao lake ni Heroin.

“Hivyo mshtakiwa anapaswa kujitetea kwa sababu Mahakama imemkuta na hatia,”

Baada ya kueleza hayo, Wakili wa utetezi Hudson Ndusyepo alidai kuwa mshtakiwa atajitete kwa hati ya kiapo ambapo watakuwa na mashaidi 15.

Hakimu Mkeha aliahirisha kesi hiyo hadi August 30 Na 31, 2017 ambapo itasikikizwa mfululizo.

Mahakama Yaelezwa Jinsi MKOJO Wa Yusuf Manji Ulivyochukuliwa na Kupimwa

Mashahidi wawili akiwemo Naibu Mkuu wa Upelelezi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Ofisa wa Polisi, Ramadhan Kingai leo  wameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jinsi Mfanyabiashara Yusuf Manji alivyopelekwa kwa Mkemia Mkuu wa Serikali na kupimwa mkojo.

Mbali ya Kingai ambaye ni Shahidi wa kwanza katika kesi hiyo ya dawa za kulevya inayomkabili Manji, Shahidi mwingine ni E.1125 Copro Detective Sospter.

Mashahidi hao walitoa ushahidi wao mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi, Cyprian Mkeha baada ya Wakili Mkuu wa Serikali, Timony Vitalis kueleza kesi hiyo imeitishwa kwa ajili ya ushahidi.

Akiongozwa na Wakili Vitalisi, Shahidi Kingai amedai kuwa February 9, 2017 akiwa Ofisini kwake Central alikuwa na kazi mbalimbali ikiwemo ya kuripotiwa kwa watuhumiwa wa Dawa za kulevya waliotajwa na RC Makonda.

Amedai katika watuhumiwa hao alimpokea Yusuf Manji na Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima baada ya kuripoti wenyewe kituoni hapo.

“Baada ya kufika nikiwa kama Mwenyekiti wa Kamati ya Uchunguzi wa dawa za kulevya nilielekeza Manji na Gwajima wapelekwe kwa Mkemia Mkuu kupimwa, kwa sababu tuhuma zao ni za dawa za kulevya, ambapo pia walienda kupekuliwa nyumbani mwao”

Shahidi huyo akadai kuwa amri ya kupimwa ilitekelezwa na Detective Copro Sospeter, ambapo baada ya kufanyika uchunguzi akapewa taarifa kwamba Manji anatumia Dawa za kulevya aina ya Benzodiazepines na Gwajima hatumii.

“Nikiwa kama Mpelelezi Mkuu niliichukua ripoti hiyo kisha nilielekeza Manji afunguliwe jalada la kutumia dawa za kulevya ambapo baada ya kufunguliwa lilipelekwa kwa DPP”.

Baada ya kueleza hayo, Wakili wa Manji, Hudson Ndusyepo alimuuliza shahidi huyo kwa nini dawa za kulevya (Benzodiazepines) alizozitaja Mkemia Mkuu ni tofauti na zilizotajwa kwenye hati ya Mashtaka (Heroin) ambapo shahidi huyo alijibu hajui na yeye hakuandaa hati ya mashtaka.

Shahidi wa pili, Detective Copro Sospeter akiongozwa na Wakili Vitalis alidai kuwa February 9, 2017 saa 5 asubuhi alikuwa Ofisini na alimpeleka Manji kwa Mkemia Mkuu wa Serikali ili kuchubguzwa.

Alidai kuwa maelezo ya kumpeleka Manji kwa Mkemja aliyapata kwa Kingai, ambapo alimpeleka kwa tuhuma za kutumia dawa za kulevya.

” Nilimchukua Manji na kumpeleka msalani ili ichukuliwe sampo ya mkojo wake ufanyiwe uchunguzi, ambapo kuna kielelezo cha fomu kuhusu suala hilo na naomba kipokelewe na Mahakama.”

Alieleza kuwa baada ya mtuhumiwa kuchunguzwa alichukua majibu kisha alirejeshwa Polisi na taratibu kufatwa.

Baada ya kuelezwa hayo, Hakimu Mkeha aliahirisha kesi hadi August 23, 2017.

DPP aamua kuachana na mbunge Lwakatare kuhusu ugaidi

Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) ameaondoa maombi yake dhidi ya Mbunge wa Bukoba Mjini (Chadema), Wilfred Lwakatare kuhusiana na shtaka la ugaidi dhidi yake.
DPP alikuwa amefungua maombi Mahakama ya Rufani akiomba kibali cha kufungua maombi ya mapitio kuhusiana na uamuzi wa Mahakama Kuu kumfutia Lwakatare mashtaka ya ugaidi.
Maombi hayo ya DPP yalitarajiwa kusikilizwa leo Ijumaa, Agosti 11 na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mussa Kipenka, lakini DPP akaamua kuyaondoa kabla ya usikilizwaji.
Wakili wa Serikali Mkuu, Tumaini Kweka ameieleza mahakama kuwa DPP hana nia ya kuendelea na maombi hayo.
Kutokana na nia hiyo ya DPP, wakili wa mjibu maombi, Richard Rweyongeza amesema kuwa hana pingamizi dhidi ya nia ya DPP kuyaondoa maombi hayo na Jaji Kipenka akatoa amri ya kuyaondoa mahakamani maombi hayo.
Kwa uamuzi huo sasa Lwakatare anabaki na shtaka la kula njama ili kutenda kosa, katika kesi ya msingi inayosikilizwa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.
Awali, Lwakatare na mwenzake walikuwa Ludovick Rwezaura walikuwa wakikabiliwa na jumla ya mashtaka manne likiwemo la kula njama za kufanya vitendo vya kigaidi kwa lengo la kumdhuru kwa sumu aliyekuwa Mhariri wa gazeti la Mwananchi, Denis Msacky.
Mashtaka mengine yalikuwa ni ya ugaidi, wakidaiwa kuandaa mikutano ya kupanga makosa ya kigaidi na kufadhili vitendo vya kigaidi.
Hata hivyo, Lwakatare kupitia kwa mawakili wake walifungua maombi Mahakama Kuu wakipinga mashtaka hayo yaliyokuwa yakiangukia katika Sheria ya Ugaidi.
Mahakama Kuu katika uamuzi wake uliotolewa na Jaji Lawrence Kaduri ilikubaliana nayo na akamfutia Lwakatare mashtaka hayo ya ugaidi na hivyo kubakiwa na shtaka moja tu la kula njama ambalo haliangukii katika sheria hiyo ya ugaidi.
DPP hakukubaliana na uamuzi huo wa Mahakama Kuu, ndipo akafungua maombi ya kibali kufungua maombi nje ya muda, ili kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu kumfutia mashtaka hayo ya ugaidi.

Chanzo:  Mwananchi

Serikali kuja na mashahidi 10 kesi ya dawa za kulevya inayomkabili Manji

Serikali imeieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kwamba itafika na mashahidi wasiozidi 10 katika kesi ya kutumia na kujihusisha na dawa za kulevya inayomkabili mfanyabiashara, Yussuf Manji.
Hayo yameelezwa na Wakili wa Serikali Mkuu, Timony Vitalis mbele ya Hakimu Mfawidhi, Cyprian Mkeha baada ya kumsomea Manji maelezo ya awali (Ph) ambapo katika maelezo hayo, Vitalis amedai mshtakiwa ni mkazi wa Sea view DSM, pia ni mfanyabiashara anayetuhumiwa kujihusisha na kutumia dawa za kulevya.
Amedai kuwa alikamatwa February 2, 2017 kisha akapelekwa kituo cha Polisi ambapo alichukuliwa hadi nyumbani kwake na kupekuliwa na baada ya kupekuliwa alipelekwa kwa Mkemia Mkuu wa Serikali na kuchukuliwa haja ndogo (Mkojo) ambao ulipimwa na kukutwa na dawa za kulevya aina ya Benzodiazepine.
Baada ya kusomewa maelezo hayo, Manji alikubali wasifu wake kwamba ni mfanyabiashara, makazi na jina lake licha ya kudai limekosewa ila usahihi ni Yusuf Manji huku akikana maelezo mengine.
Aidha, wakili Vitalis ameieleza Mahakama kwamba wanaomba kupangiwa tarehe kwa ajili ya kesi hiyo kuanza kusikilizwa, pia wanatarajia kuwa na mashahidi wasiozidi 10 hivyo Hakimu Mkeha ameahirisha kesi hiyo hadi August 22, 23, na 24, 2017 kwa ajili ya kusililizwa mfululizo.

Bilionea IPTL kutibiwa Amana au Lugalo

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imeamuru mshtakiwa Harbinder Singh Sethi anayeumwa atibiwe hapahapa nchini.
Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi amesema hajawahi kusema atibiwe nje ya nchi, bali atibiwe nchini na kwamba ndani ya siku 14 wanasubiri matokeo kama amefikishwa hospitali kutibiwa ama la.
Amesema hay oleo Alhamisi, Agosti 3 baada ya Mwendesha Mashtaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Leonard Swai kuomba atibiwe katika Hospitali ya Amana au Lugalo.
Akiwasilisha hoja hiyo leo kwa Hakimu Shaidi, Swai amekiri kuwepo kwa amri ya Mahakama ya mshtakiwa kupatiwa matibabu.
Hata hivyo, amedai hawana ushahidi kuwa siku mshtakiwa alipokamatwa alikuwa anakwenda Afrika Kusini kutibiwa.
Pia, amedai suala la mshtakiwa kupelekwa nje ya nchi kutibiwa si sahihi kwa sababu utaratibu wa mgonjwa kupelekwa nje unafahamika na kwamba haendi kwa sababu ya amri ya Mahakama.
Swai amepinga Sethi kutibiwa nje kwa kuwa madaktari wa hapa nchini hawajakiri kushindwa na hakuna uthibitisho wa madaktari kwamba wameshindwa kumtibu.
Pia, amedai hakuna utaratibu wa mgonjwa kupelekwa Muhimbili moja kwa moja anatakiwa kuanzia Hospitali ya Amana ama Lugalo wao ndiyo watafanya utaratibu wa kumuhamishia Hospitali ya Muhimbili.
Amedai Magereza ambapo Sethi anatibiwa ndiyo wametakiwa kuthibitisha na kufanya utaratibu apeleke Hospitali ya Amana.
Amebainisha kuwa Amana nao hawajasema wameshindwa kumtibu hivyo ameomba aendelee kutibiwa katika Hospitali ya Amana.
Kuhusu ombi la Wakili wa Sethi, Alex Balomi kuomba kesi itajwe ndani ya siku saba kwa ajili ya kuangalia kama amepelekwa hospitali.
Swai aliyeomba siku 14 alidai kutajwa ndani ya siku saba ni kumsumbua mgonjwa na kwamba muda huo autumie kwenda hospitali na siyo mahakamani.
Amebainisha kuwa ndani ya siku 14, atakuwa amefikishwa katika Hospitali ya Amana ama Lugalo kupatiwa matibabu kwa kuwa taratibu za Magereza zimekamilika na wao watasimamia.
Lakini Balomi amedai hadi sasa mteja wake hajapelekwa hospitali na akaomba mahakama isimamie amri yake ya mshtakiwa kupatiwa matibabu.
Hakimu Shaidi katika uamuzi wake amewapa siku 14 Takukuru kama walivyoomba awali, ili kuangalia kama atakuwa amefikishwa katika Hospitali ya Amana ama Lugalo kupatiwa matibabu.

Kesi imeahirishwa hadi Agosti17, 2017.
Awali, Julai 14, 2017, Wakili wa kujitegemea wa Sethi, Alexi Balomi aliifahamisha mahakama kuwa Sethi anaumwa na kwamba hali yake ilikuwa ikiendelea kubadilika kuwa mbaya na alikuwa hawezi kupata usingizi kwa wiki nne.
Wakili Balomi aliiambia mahakama hiyo kuwa Seth anasumbuliwa na uvumbe tumboni kama puto ambao unahitaji uangalizi wa karibu wa madaktari.
Katika kesi hiyo, Sethi na James Rugemarila wanakabiliwa na mashtaka 12 ya uhujumu uchumi kwa kula njama, kujihusisha mtandao wa uhalifu , kighushi, kutoa nyaraka za kughushi, kujipatia fedha kwa njia za udanganyifu, kutakatisha fedha na kuisababisha hasara ya Doa za Marekani 22, milioni na Sh309 bilioni.

Maombi ya wabunge waliofukuzwa CUF yasikilizwa

Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam hivi sasa inaendelea na usikilizwaji wa maombi ya wabunge waliofukuzwa na Chama cha Wananchi (CUF), ya kutaka kusimamishwa kuapishwa kwa wabunge wapya walioteuliwa juzi kuziba nafasi zao.
Hata hivyo, badala ya kusikiliza maombi ya msingi, mahakama inasikiliza mapingamizj ya awali yaliyowasilishwa na jopo la Mawakili wa Serikali kwa niaba ya wajibu maombi, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) na Katibu wa Bunge pamoja na pingamizi lililowasilishwa na Bodi ya Wadhamini CUF, na wabunge wateule.
Waombaji katika maombi haya wanawakilishwa na mawakili wawili, Peter Kibatala na Omari Msemo, wakati NEC na Bunge wanawakilishwa na jopo la mawakili nane wa Serikali wakiongozwa na Wakili wa Serikali Mkuu, Gabriel Malata, wakati Bodi ya Cuf na wabunge wateule wanawakilishwa na Wakili Mashaka Ngole.
Baada ya kumaliza hoja zao za pingamizi, Kibatala na Msemo watajibu hoja hizo na baadaye Jaji Lugano Mwandambo atatoa uamuzi ama leo hii au siku nyingine atakayopanga.

Mkemia: Mkojo wa Masogange umebainika kuwa na heroin

Mkemia kutoka Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Elias Mulima, ameiambia Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa sampuli ya mkojo wa msanii Agnes Gerald maarufu kama Deal ama Masogange (28) umebainika kuwa na dawa ya kulevya aina ya heroin.
Akitoa ushahidi leo Jumatano mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbard Mashauri, shahidi huyo wa kwanza wa upande wa mashtaka, akiongozwa na Wakili wa Serikali, Constantine Kakula, ameiambia mahakama kuwa mnamo February 15, 2017 askari wawili kutoka Jeshi la Polisi Tanzania, Koplo Sospeter na WP Judith, walimfikisha Masogange ofisini kwake kwa lengo la kumfanyia vipimo vya mjono wake.
Alisema baada ya kuwapokea, alimsajili Masogange na kumpa namba ya mahabara 446 /2017 na kisha kuwakabidhi kifaa maalum kwa ajili ya kuweka sampuli ya mkojo.
Alidai baada ya kupokea sampuli ya mkojo ya Masogange alifanyia uchunguzi kwa kutumia kemikali na kubaini kuwa mkojo wake una chembechembe za dawa za kulevya aina ya heroin ambazo kwa kitaalamu zinajulikana kama Diacety Imophine.
Aidha, alisema uchunguzi zaidi ulibaini chembechembe za dawa nyingine ya kulevya aina ya Oxazepam.
Shahidi huyo alidai baada ya kufanya uchunguzi huo, aliandaa taarifa ya uchunguzi kuhusiana na sampuli hiyo ya mkojo ambapo aliisaini yeye mwenyewe na kuthibitishwa na kaimu mkemia mkuu wa serikali.
Shahidi huyo alimtambua Masogange kwa ndiye aliyepelekwa kuchukuliwa sampuli hiyo ya mkojo ofisini kwake.
Pia alidai anaweza kuitambua taarifa hiyo ya uchunguzi kutokana na kuwepo kwa saini yake, muhuri wa moto wa maabara ya mkemia mkuu wa serikali. Pia ameomba mahakama kupokea vitu hivyo kama kielelezo cha ushahidi katika kesi hiyo.
Hata hivyo, mawakili Nehemiah Nkoko na Reuben Simwanza ambao wanamtetea Masogange wamepinga taarifa hiyo ya uchunguzi wakitaka isipokelewe na mahakama kwa madai haijakidhi vigezo vya sheria.
Nkoko amedai utaratibu wa kisheria haukufatwa kabla ya mtuhumiwa aliyeko chini ya polisi kufanyiwa uchunguzi wa kitabibu, kwa kuwa ofisa wa polisi alitakiwa kuwasilisha maombi mahakamani ndipo amri ya kupimwa itolewe.
Amesema katika ushahidi wake mkemia huyo hajaeleza kama ofisa wa polisi alipeleka amri ya mahakama kutoka mahakama yoyote ile.
"Ripoti ipo kinyume na sheria, mahakama ina njia moja tu nayo ni kuikataa na sio kuikubali. Sheria ipo wazi, tunaomba mahakama ikubali pingamizi letu na kukataa kupokea taarifa hiyo," alisema.
Naye Wakili Simwanza alidai ripoti hiyo ikitazamwa inataja fomu nyingine ya ombi la Jeshi la Polisi kwenda kwa Mkemia Mkuu kwa ajili ya kufanya vipimo.
Amedai ripoti hiyo ipo yenyewe bila ya kuambatanishwa na fomu maalum inayotumiwa na polisi kupeleka sampuli hivyo haiwezi kupokelewa na kutumika kama kielelezo.
Akijibu hoja hizo, Wakili Kakula alidai mapingamizi hayo hayana mashiko wala miguu ya kusimamia.
Amedai fomu ambayo haijaambatanishwa na ile ya mkemia mkuu ni vitu viwili tofauti na hata uwasilishwaji wake unafanywa na watu wawili tofauti.
Alisema taarifa ya mkemia inawasilishwa na mkemia na ile ya polisi inawasilishwa na polisi.
Kuhusu hoja ya sampuli ya mkojo, Kakula alidai kifungu cha 63 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai (CPA), kimeweka mazingira ambayo ofisa wa polisi atawasilisha maombi mahakamani kuweza kuchukua sampuli.
Alisema iwapo mtuhumiwa anakataa kuchukuliwa sampuli ya mkojo, hivyo atawasilisha ombi mahakamani ili iweze kutolewa amri.
Kakula alisema katika pingamizi lao upande wa utetezi haijaeleza kwamba mshitakiwa alikataa kupima, akalazimishwa. Aliomba mapingamizi hayo yatupiliwe mbali.
Hakimu Mashauri ameahirisha shauri hilo hadi Agosti 28, 2017 kwa ajili ya kutoa uamuzi wa ama kupokelewa kwa taarifa hiyo ama la.
Masogange amefikishwa mahakamani hapo akidaiwa kutumia dawa za kulevya aina ya heroin kati ya Februari 7 na 14, mwaka huu, katika maeneo yasiyojulikana ndani ya jijini a Dar es Salaam.
Masogange yupo nje kwa dhamana.

WAKILI WA LISSU, FATMA KARUME AMBURUZA KORTINI ASKARI POLISI ALIYEMSHIKA MKONO MAHAKAMANI, ANADAI FIDIA YA BILIONI MOJA

Wakili wa Mwanasheria Mkuu wa Chadema na Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika, Fatma Karume amefungua kesi ya madai Mahakama Kuu ya Tanzania dhdi ya Inspekta wa Polisi Eugene Mwampondela wa Kituo Kikuu cha Polisi Dar es salaam.

Fatma amesema kuwa Inspekta Mwampondela alimshika mkono na kumvuta kwa nguvu hali iliyomsababishia maumivu makali, hivyo anadai alipwe kiasi cha shilingi bilioni moja kwa kosa la kumwingilia mwilini mwake na kumbughudhi kwa kumzuia kufanya kazi yake.

“Aliniambia kuwa ameagizwa na wakubwa kutoka juu, hivyo namfikisha mahakamani ili amweleze jaji ni nani aliyemtuma, na mimi sitaki kushikwa shikwa mwili wangu kwa hiyo naomba anilipe shilingi bilioni moja ili liwe fundisho kwa wengine,”amesema Fatma.

Fatma ambaye ni mmoja wa mawakili wa Mbunge wa Singida Mashariki alikumbana na kadhia hiyo wakati akiwa katika harakati za kumtetea mteja wake ili aweze kupata dhamana.

Chanzo: Mtanzania

Waliovuliwa Ubunge na Lipumba CUF Wafungua Kesi Mahakamani

Siku chache baada ya Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi CUF, Prof. Lipumba kuwavua uanachama Wabunge wanane wa Viti Maalum kisha Spika Ndugai kuridhia uamuzi huo, jana July 27, 2017 Wabunge hao wamefungua kesi katika Mahakama Kuu ya Tanzania.

Wabunge hao wamefungua kesi hiyo iliyopewa namba 143/2017 kupitia Wakili wao Peter Kibatala lakini hata hivyo bado haijapangiwa Jaji huku Wabunge hao wakidai hawajapewa muda wa kujitetea.

Mbali na kufungua kesi katika Mahakama Kuu Tanzania, pia wamekata rufaa ndani ya Chama chao kupinga utekelezaji huo na kuiomba Mahakama isitishe utekelezaji wa uamuzi wa kufukuzwa Uanachama wao.

Mahakama yamuachia Lissu kwa dhamana

Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu amepata dhamana baada ya ombi la mawakili wa Serikali la kuomba Mahakama imnyime haki ya kudhaminiwa kutupiliwa mbali na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbard Mashauri ametoa uamuzi huo leo, Julai 27 akimtaka Lissu kuwa na wadhamini wawili wanaoaminika ambapo kila mmoja atasaini bondi ya Sh10 milioni.

Pia, amemtaka asitoke nje ya Jiji la Dar es Salaam bila ya kuwa na kibali cha Mahakama.

Hakimu ameahirisha kesi hiyo kwa muda kusubiri wadhamini. Kutokana na ulinzi kuimarishwa mahakamani hapo watu wengi walizuiwa getini.

Julai 24, jopo la mawakili wanne wa Serikali, Kishenyi Mutalemwa, Simon Wankyo, Paul Kadushi na Tulumanywa Majigo waliwasilisha hoja mahakamani hapo wakiomba Lissu anyimwe dhamana.

Jopo la mawakili 18 wanaomtetea Lissu, likiongozwa na Fatma Karume na Peter Kibatala liliomba mteja wao apewe dhamana.

Katika shauri linalomkabili, Lissu anadaiwa Julai 17 eneo la Mtaa wa Ufipa, Kinondoni, Dar es Salaam alitoa maneno ya uchochezi kuwa, 'Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais John Magufuli ni ya kibaguzi wa kifamilia, kikabila, kikanda na kidini.'

Mwana FA na AY Waendelea Kutamba Mahakamani

Wasanii wakongwe wa Bongo Flava, Ambwene ‘AY’ Yesaya na Hamisi ‘Mwana FA’ Mwinjuma wameendelea kupeta mahakamani wakitarajiwa kulipwa kiasi cha shilingi bilioni 2.1 na kampuni ya Mic Tanzania Limited.
Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam imetupilia mbali maombi ya Kampuni hiyo ya huduma za simu za mkononi iliyotaka kukata rufaa katika Mahakama ya Rufaa kupinga amri ya kutakiwa kuwalipa wasanii hao kiasi hicho cha fedha.

Hivi karibuni, Mahakama Kuu ilihalalisha uamuzi wa Mahakama ya Wilaya iliyoikuta na hatia ya kutumia bila kibali nyimbo za wasanii hao kama miito ya simu na kuitaka kuwalipa kiasi hicho cha fedha.

Wakili wa wasanii hao, Albert Msando aliweka pingamizi akiiomba Mahakama Kuu kuyakataa maombi yaliyowasilishwa na wanasheria wa kampuni ya Mic kwa madai kuwa ni batili kwani yalikuwa na makosa ya kisheria.

Jaji Isaya Arufani wa Mahakama Kuu alikubaliana na maelezo ya Wakili Msando na kuyatupilia mbali maombi ya wanasheria wa kampuni hiyo. Bado haijafahamika kama watafanya marekebisho na kurejesha maombi mapya au la.

AY na Mwana FA wanadai kuwa kampuni ya Mic Tanzania Limited ilitumia bila ruhusa yao nyimbo zao ‘Usije Mjini’ na ‘Dakika Moja’.

Lissu asomewa mashtaka ya uchochezi

Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu amefikishwa katika Mahakama ya Kisutu, Dar es Salaam na kusomewa mashtaka ya kutoa lugha ya uchochezi.
Akisomewa mashtaka mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbard Mashauri leo Jumatatu, Julai 24, mahakama imeelezwa kuwa Lissu ametoa lugha ya uchochezi dhidi ya Serikali Julai 17 akiwa maeneo ya Ufipa, Kinondoni.
Imedaiwa kuwa maneno hayo yalikuwa na lengo ya kuleta chuki dhidi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Alipotakiwa kukubali ama kukataa makosa hayo na Hakimu Mashauri, Lissu amesema kusema kweli haijawahi kuwa kosa la jinai.
Kwa sasa upande wa mashtaka wameomba Lissu anyimwe dhamana na upande wa utetezi wanapinga hoja ambazo bado zinaendelea.

Rais wa TFF Jamal Malinzi na Katibu Wake Wanyimwa Dhamana na Kurudishwa Rumande

Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi na Katibu Mkuu wa shirikisho hilo Selestine Mwesigwa wamenyimwa dhamana kwa kesi inayowakabili, wamerudishwa rumande mpaka Julai 17 mwaka huu shtaka lao litakaposomwa tena.

Uamuzi huo umetolewa na Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Kisutu Jijini Dar es Salaam, Wilbard Mashauri baada ya mabishano makali ya kisheria dhidi ya mawakili wa utetezi na mawakili upande wa jamhuri (serikali).

Malinzi na Mwesigwa walishikwa na Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini (TAKUKURU) mnamo Juni 27 kwa kutuhumiwa matumizi mabaya ya madaraka waliyokuwa nayo katika uongozi wao na kupandishwa Mahakamani kwa mara ya kwanza mnamo Juni 29 na kusomewa mashtaka 28 ya kughushi na kutakatisha fedha kupitia akaunti

Rugemalira, Sethi waongezewa mashtaka sita

Mfanyabiashara Harbinder Singh Sethi na James Rugemalira wamepandishwa kizimbani kwa mara nyingine katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashtaka 12, badala ya mashtaka sita waliyosomewa awali.
Miongoni mwa mashtaka hayo 12 ya uhujumu uchumi yamo mashtaka matano ya kutakatisha fedha na kuisababisha hasara ya USD 22, 198, 544.60 na Sh 309,461,300,158. 27.
Akiwasomea hati mpya ya mashtaka, Wakili wa Serikali Mwandamizi, Shedrack Kimaro kwa Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi alidai wanakabiliwa na mashtaka ya kula njama, kujihusisha mtandao wa uhalifu, kighushi, kutoa nyaraka za kughushi, kujipatia fedha kwa njia za udanganyifu, kuisababishia Serikali hasara na kutakatisha fedha.
Washtakiwa hao katika shtaka la kwanza wanadaiwa, Rugemarila ambaye ni Mkurugenzi wa VIP na mmiliki mwenza wa zamani wa IPTL, Sethi ambaye ni Mwenyekiti Mtendaji wa PAP wanadaiwa kuwa kati ya Oktoba 18, 2011 na Machi 19, 2014 jiji Dar es Salaam walikula njama katika nchi za Afrika Kusini, Kenya na India ya kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu.
Kimaro alidai katika shtaka la pili la kujihusisha na mtandao, washtakiwa hao kati ya Oktoba 18, 2011na Machi 19, 2014 jijini Dar es Salaam wakiwa siyo watumishi wa umma na watumishi wa umma walitekeleza mtandao huo wa uhalifu kwa lengo la kujipatia faida.
Kwa upande shtaka la tatu, Sethi anadaiwa kuwa Oktoba 10, 2011 katika mtaa wa Ohio Ilala Dar es Salaam akiwa na nia ya ulaghai alighushi fomu namba 14 ya usajili wa makampuni na kuonyesha yeye ni mtanzania anayeishi Kitalu namba 887 Mtaa wa Mrikau Masaki wakati akijua ni uongo.
Seth katika shtaka la nne anadaiwa kutoa nyaraka ya kughushi ambayo ni fomu namba 14a ya usajili wa kampuni kwa ofisa msajili wa kampuni, Seka Kasera kwa njia ya kuonyesha kwamba yeye ni mtanzania na Mkazi wa Mtaa wa Mrikau.
Katika shtaka la tano, washtakiwa wote, wanadaiwa kuwa kati ya Novemba 28/29, 2011 na Januari 23, 2014 makao makuu Benki ya Stanbic Kinondoni na Benki ya Mkombozi Tawi St Joseph kwa ulaghai washtakiwa hao walijipatia kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BoT), walijipatia USD 22,198,544.60 na Sh 309, 461,300,158.27.
Katika shtaka sita la kusababisha hasara, washtakiwa hao wanadaiwa kuwa Novemba 29, 2013 katika Benki ya Stanbic tawi la kati Kinondoni kwa vitendo vyao waliisababishia Serikali hasara ya USD 22, 198, 544.60 na Sh 309,461,300,158.27.
Kimaro alidai katika la saba, kuwa kati ya Novemba 29, 2013 na Januari 23, 2014 maeneo tofauti Dar es Salaam kwa pamoja walitenda kosa la kutakatisha fedha kwa kuchukua fedha kutoka BoT USD 22,198,544.60 na Tsh 309,461,300, 158.27 wakati wakijua fedha hizo zao la kujihusisha na genge la uhalifu.
Shtaka la nane, Kimaro alidai kuwa Novemba 29, 2013 katika tawi la kati la Benji ya Stanbic Tanzania Wilaya ya Kinondoni Sethi alitakatisha fedha kwa kuchukua BoT USD 22,198,544.60 wakati akijua fedha hizo zimetokana na zao la kujihusisha na genge la uhalifu.
Kwa upande wa shtaka la tisa, Sethi anadaiwa kuwa kati ya Novemba 29, 2013 na Machi 14,2014 katika tawi la kati la Benji ya Stanbic Kinondoni Dar es Salaam alitakatisha fedha, Sh 309,461,300,158.27 kutoka BoT wakati akijua fedha hizo zimetokana na zao la kujihusisha na genge la uhalifu.
Shtaka ya kumi, inadaiwa Januari 23, 2014 katika Benki ya Mkombozi tawi la St Joseph Cathedral, Rugemalila alitakatisha fedha, Sh 73, 573, 500,000 kutoka kwa Seth wakati akijua fedha hizo zimetokana na zao la kujihusisha na genge la uhalifu.
Kwa upande wa shtaka la 11, Kimaro alidai kuwa Januari 23,2014 katika Benki ya Mkombozi tawi la St Joseph Cathedral, Rugemarila alitakatisha fedha USD 22,000,000 kutoka kwa Seth wakati akijua fedha hizo ni zao la uhalifu.
Shtaka la 12, Seth anadaiwa kuwa Januari 28, 2014 katika tawi la kati la Benki ya Stanbic Wilaya ya Kinondoni alihamisha Rand (zar 1,305,800 kwenda kwenye akaunti namba 022655123 katika Standard bank Land Rover Sandton Johannesburg wakati akijua katika kipindi anahamisha fedha hizo zimetokana na zao la kujihusha na genge la uhalifu.
Washtakiwa hawakuruhusiwa kuongea chochote kwa sababu mahakama ya Kisutu haina mamlaka ya kusikiliza kesi hao.
Upande wa mashtaka ulidai upelelezi bado haujakamilika na washtakiwa wamepelekwa rumande hadi Julai 14, 2017.
Hata hivyo mashtaka ya kutakatisha fedha yanayowakabili washtakiwa hao hayana dhamana.

Chanzo: Mwananchi

Kesi ya Ndama, Mtoto wa Ng’ombe yahairishwa

Kesi inayomkabili mfanyabiashara, Shabani Hussein maarufu Pedeshee Ndama Mtoto wa Ng'ombe imeahirishwa hadi Julai 20, 2017 baada ya upande wa mashtaka kudai upelelezi bado haujakamilika.
Ndama ambaye kwa sasa yupo nje kwa dhamana, kesi yake imetajwa leo(Ijumaa) mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Victoria Nongwa.
Ndama kwa sasa anakabiliwa na mashtaka matano baada ya kulikubali shtaka la sita la kutakatisha fedha na kisha kuhukumiwa na kuachiwa huru baada ya kulipa faini ya Sh 200milioni.
Hatua yake ya kulipa kiasi hicho cha fedha, ilimuepusha na kifungo cha miaka mitano jela.
Ndama yupo huru pia kwa dhamana baada ya kukamilisha masharti ya dhamana ya kuwa na wadhamini wawili wanaoaminika ambapo kila mdhamini alisaini bondi ya Sh 100 milioni.
Pia mshtakiwa mwenyewe aliweka hati ya mali isiyohamishika yenye thamani ya Dola 270,200 ambazo ni sawa na zaidi ya Sh 600milioni.

Ushahidi kesi ya Wema Sepetu wakwama kutolewa

Kesi ya kukutwa na dawa za kulevya inayomkabili Wema Sepetu katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imeahirishwa hadi Julai 10.
Wema ambaye ni mshindi wa taji la urembo, maarufu Miss Tanzania kwa mwaka 2006 na msanii wa filamu, anakabiliwa na kesi hiyo akidaiwa kutumia na kupatikana na bangi.
Wakili wa Serikali, Elizabeth Mkunde mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Godfrey Mwambapa alisema kesi ilipangwa leo (Jumatano) kuanza kusikiliza ushahidi wa upande wa mashtaka lakini Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba anayeisikiliza kesi hiyo yupo likizo.
Kutokana na hilo, aliomba iahirishwe hadi Julai 10 ombi lililokubaliwa na mahakama.
Wema na wenzake Angelina Msigwa na Matrida Abbas wanakabiliwa na mashtaka mawili ya kukutwa na dawa za kulevya na kutumia dawa hizo.
Inadaiwa Februari 4, katika makazi ya Wema, Kunduchi Ununio, walikamatwa wakiwa na msokoto mmoja na vipisi vya bangi vyenye uzito wa gramu 1.08.
Wema pia anadaiwa Februari Mosi katika eneo lisilojulikana jijini Dar es Salaam alitumia bangi.

JELA MIAKA 23 KWA KUIBA CHETI KIDATO CHA NNE

Mahakama  ya Wilaya ya Mlele mkoani Katavi imemhukumu kwenda jela miaka 23 mkazi wa kijiji cha Kalovye, Osward Mpalasinge (26).

Amepewa adhabu hiyo baada ya kupatikana na hatia ya kuvunja na kuiba vitu mbalimbali ikiwemo cheti cha kidato cha nne. Hukumu hiyo ilitolewa jana na Hakimu Mfawidhi wa mahakama hiyo, Teotimus Swai baada ya mshtakiwa kukiri kosa mahakamani.

Akitoa hukumu hiyo, Hakimu Swai alisema mtuhumiwa amekutwa na hatia pasipo shaka hivyo anahukumiwa kwenda jela miaka  23. 

Awali, Mwendesha Mashitaka, Baraka Hongoli alisema mshitakiwa alitenda makosa ya kuvunja na kuiba Mei 25 mwaka huu saa mbili usiku nyumbani kwa Veronica Crispin katika Kijiji cha Kalovye, Inyonga.

Alidai kwamba mshitakiwa alifika nyumbani hapo, akavunja na kisha kuiba nguo zenye thamani ya Sh 110,000 na cheti cha kidato cha nne cha Henreth Edward Kalamu, kilichotolewa na Baraza la Mitihani la Taifa (NECTA) mwaka 2015.

Hongoli aliitaka mahakama kutoa adhabu kali kwa mtu huyo ili iwe fundisho kwa kuwa wizi wa aina hiyo ndio umesababisha usumbufu na watu kupoteza ajira zao serikalini na maeneo mengine pindi uhakiki wa vyeti unapofanyika.

Akijitetea, mshitakiwa aliiomba mahakama impatie muda ili aweze kwenda Dar es Salaam kumtafutia mtu huyo cheti kingine

MAHAKAMA YAMHUKUMU MFANYABIASHARA 'PEDESHEE NDAMA' MIAKA 5 JELA AU FAINI YA SHILINGI MILIONI 200.

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imemuhukumu kulipa faini ya Sh200 milioni mfanyabiashara, Ndama Shabani Hussein maarufu kama Pedeshee Ndama mtoto ya Ng’ombe baada ya kulikubali na kutiwa hatiani katika shtaka la sita la kutakatisha dola za Marekani 540,000.
Akitoa hukumu hiyo leo Ijumaa, Hakimu Mkazi Mkuu, Victoria Nongwa amesema endapo mshtakiwa huyo atashindwa kulipa kiasi hicho cha fedha atatumikia kifungo cha miaka mitano jela.
Hukumu hiyo ya shtaka la sita la kutakatisha fedha ilitolewa baada ya Wakili wa Serikali, Christopher Msigwa kumsomea maelezo ya awali (PH) Ndama na kuyakubali maelezo yote yanayounda shtaka hilo la kutakatisha fedha, akapatikana na hatiani na kupewa adhabu hiyo.
Kabla ya kutolewa kwa hukumu hiyo, Wakili Msigwa aliiambia Mahakama kuwa mshtakiwa amekubali shtaka la sita la kutakatisha fedha na maelezo yanayounda shtaka hilo.
“Hatuna kumbukumbu za nyuma za makosa dhidi ya Ndama ila ni rai ya upande wa mashtaka kuwa wakati mahakama ikitoa adhabu izingatie matakwa ya kifungu cha 13(a) cha sheria ya kuzuia utakatishaji fedha,” imesema hati ya hukumu.
Amesema pia mahakama ibebe dhana ya sheria hiyo ambayo lengo lake ni kuzuia makosa ambayo yanalenga kudidimiza uchumi wa nchi na uzito wa kosa ambalo mshtakiwa amelifanya.
Kwa upande wa Wakili Wabeya Kung’e anayemtetea mshtakiwa huyo kwa kushirikiana na Jeremiah Mtobesya, Kung’e ameiambia mahakama kuwa ni wazi mshtakiwa amekiri kosa baada ya kusomewa maelezo ya awali hivyo mahakama isitoe adhabu kali kwa mshtakiwa.
Ameiomba mahakama izingatie maombi yao kwa sababu mshtakiwa huyo hilo ndiyo kosa lake la kwanza, kitendo chake cha kukiri kosa kinaonyesha kusikitikia kosa alilolitenda na kwamba anayo familia ambayo inamtegemea ambao kwa kipindi cha mwaka mmoja ambacho amekaa ndani imepata shida kwa kukosa huduma yake.
“Kwa kuzingatia kifungu cha 13(a) cha sheria ya kutakatisha fedha ni rai yetu mahakama tukufu isitoe adhabu kali kwa mshtakiwa kwa sababu amejutia kosa alilolitenda,” amesisitiza Kung’e. Hivyo Ndama amehukumiwa kulipa faini ya Sh 200 milioni ama akishindwa kutumikia kifungo cha miaka mitano jela.
Juni 6, 2017 Ndama aliiomba mahakama akumbushwe shtaka, akakumbushwa na Wakili wa Serikali, Esterzia Wilson na akalikubali shtaka hilo.
Akisomewa maelezo ya awali mahakamani hapo, Ndama alikubali maelezo ya awali aliyosomewa ikiwamo nyaraka zilizotumika kufungua akaunti iliyotumika kuingizwa fedha hizo, hundi 18 zilizotumika kutolea fedha hizo, maelezo ya benki ‘bank statement’ na Swift massage.
Iwapo atakamilisha kulipa Sh200 milioni atakuwa huru kuendelea katika mashtaka matano mengine yanayomkabili mahakamani hapo ambayo upelelezi wake bado haujakamilika.
Ndama anatakiwa kuwa na wadhamini wawili wanaoaminika na atoe fedha taslimu kiasi cha Dola za Marekani 270,200 ambacho ni sawa na zaidi ya Sh600 milioni mahakamani hapo na mali isiyohamishika yenye thamani ya kiasi hicho cha fedha.

DEREVA TAKSI AFUNGWA MIAKA 45 KWA UNYANG'ANYI

Dereva taksi, Rashid Yusuph(23) amehukumiwa kifungo cha miaka 45 jela, baada ya kupatikana na hatia ya unyang'anyi wa kutumia nguvu.

Yusuph ambaye ni mkazi wa Kimara Mbezi amehukumiwa kifungo hicho jana katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala wakati shauri hilo lilipofikishwa mahakamani hapo kwa ajili ya hukumu.

Mshtakiwa anakabiliwa na mashtaka matatu ya unyang'anyi wa kutumia nguvu dhidi ya raia watatu wa kigeni ambao walikuja nchini kwa ajili ya kufanya utafiti na utalii wakitokea nchini Zambia.

Pia, Mahakama hiyo imemuachia huru mshtakiwa wa pili katika kesi hiyo, Ramadhani Kingazi (23) ambaye ni mjomba wa mshtakiwa wa kwanza, baada ya kushindwa kumtia hatiani.

Akisoma huku hiyo, hakimu mkazi mfawidhi wa mahakama hiyo, Ritha Tarimo alisema imemtia hatiani mshtakiwa kama alivyoshtakiwa hivyo atatumikia kifungo cha miaka 45 jela ili iwe fundisho.

Hakimu Tarimo alisema ameridishwa na ushahidi wa mashahidi saba waliotoa mahakamani hapo dhidi ya mshtakiwa huyo.

"Nakuhukumu kifungo cha miaka 45 jela kwa makosa yote matatu ya unyang'anyi wa kutumia nguvu, kwa sababu tukio hili lilitokea sehemu moja na kwa wakati mmoja hivyo, kila kosa moja utatumikia kifungo cha miaka 15 na adhabu hii ina kwenda kwa pamoja," alisema Hakimu Tarimo.

Kabla ya kutolewa kwa hukumu hiyo, Wakili wa Serikali, Ashura Mzava aliomba mahakama kutoa adhabu kali dhidi ya mshtakiwa huyo kwani tukio hilo lilifanyika kwa raia wa Marekani ambao wanawakilisha nchi yao hapa nchini.

"Mheshimiwa Hakimu naomba mahakama yako itoe adhabu kali ili iwe fundisho kwa mtu yeyote mwenye nia ya kuharibu taswira ya nchi na kwa yoyote anayefikiria kuibia raia wa Tanzania na wasio kuwa raia wa Tanzania ," alisema Mzava.

Katika hati ya mashtaka, mshtakiwa anadai kutenda kosa hilo Aprili 28, 2016 katika Stesheni ya Tazara iliyopo Wilaya ya Ilala.

Ilidaiwa katika shtaka la pili mshtakiwa aliiba fedha za Zambia kwacha 50, dola za kimarekani 200, kadi moja ya Atm pamoja na saa ya mkononi, mali ya raia wa kigeni, Mariah Melena.

Katika shtaka la tatu, siku na eneo hilo hilo mshtakiwa aliiba dola za kimarekani 250, fedha taslimu Sh 50,000, fedha za Zambia Kwacha 300, simu moja, Ipad, chaji pamoja na flashi mali ya raia wa kigeni, Sydney Shapiro.

Shtaka la nne, mshtakiwa anadaiwa kuiba dola 650 za kimarekani, simu moja ya mkononi aina ya IPhone 6, pamoja na dola 300 ambazo zilikuwa kwenye akaunti mali ya Lylia Garcia.

Yusuph anadaiwa, kuiba vitu hivyo baada ya walalamikaji hao kumkodisha kutoka Stesheni ya Tazara kwenda katika hoteli waliyokuwa wamekodiwa na mwenyeji wao na kwamba kabla na baada ya kujipatia vitu hivyo, alitumia nguvu ili aweze kujipatia vitu hivyo bila kizuizi.

Chanzo: Mwananchi