Rais wa Marekani, Barack Obama na mkewe Michelle wakiaga katika Uwanja wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere, jana, baada ya kumalizika kwa ziara yao ya siku mbili nchini. Picha na AFP
Dar es Salaam. Rais Barack Obama wa Marekani ameitaka Serikali ya Tanzania kuhakikisha miradi iliyopangwa kutekelezwa chini ya ufadhili wa nchi hiyo haicheleweshwi bila ya sababu za msingi.
Alisema hayo jana katika mitambo ya kufua umeme ya
Symbion na kubainisha kuwa Marekani imetenga kiasi cha Dola 7 bilioni
zitakazotolewa kwa nchi sita za Afrika katika kipindi cha miaka mitano
kugharimia miradi ya umeme.
Akizungumza mbele ya mwenyeji wake, Rais Jakaya
Kikwete, Rais Obama alisema utamaduni wa kuchelewesha utekelezaji wa
miradi haufai kufumbiwa macho kwani unakawiza maendeleo kwa wananchi
wenye shida.
“Utakuta mradi unakaa kwa miaka saba au minane
bila ya kutekelezwa, jambo hilo hatutaki litokee. Mara mradi unapopangwa
na mipango kukamilika, basi utekelezwe haraka iwezekanavyo ili wananchi
waone faida zake,” alisisitiza Rais Obama.
Rais Obama alikuwa akizungumzia mradi mkubwa wa
umeme unaofadhiliwa na nchi yake ujulikanao kama ‘Power Afrika’ ambao
pamoja na fedha hizo za Serikali yake, taasisi mbalimbali binafsi nazo
zimetoa Dola 9 bilioni kwa ajili ya utekelezaji wake.
Akizungumza na waandishi wa habari baada ya hotuba
hiyo ya Rais Obama, Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter
Muhongo alisema tatizo la ucheleweshaji wa miradi halipo kwa Tanzania
kwa kuwa Serikali imejipanga vyema kuhakikisha kuwa mambo yanakwenda kwa
kasi chini ya utaratibu mpya wa ‘Matokeo Makubwa Sasa’ (Big Results
Now) inayosimamiwa na Kitengo cha Ofisi ya Rais kinachoitwa President’s
Delivery Unit.
Hata hivyo, Profesa Muhongo alisema tayari
Tanzania imeshaorodhesha miradi ambayo ingependa itekelezwe chini ya
mpango huo na tayari miradi hiyo imeshawasilishwa katika ofisi za
Ubalozi wa Marekani nchini.
Endelea kusoma habari hii kwa kubofya hapa chini
Waziri Muhongo alisema miradi mingi ni ya umeme vijijini ambayo inatekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (Rea).
Katika hotuba yake fupi, Rais Obama alibainisha
kuwa lengo la Marekani ni kuzisaidia nchi za Afrika kujiondoa katika
umasikini ili ziondokane na kuwa ombaomba wa misaada.
“Kwa yale niliyoyaona katika ziara yangu ya wiki
moja kuanzia Senegal, Afrika Kusini na hapa Tanzania, ni dhahiri kuwa
Afrika ina uwezo wa kujiondoa katika umasikini,” alisema Rais Obama.
Alisema mradi huo wa Power Africa unalenga mambo
mawili makubwa. Kwanza, kuhakikisha kuwa idadi ya watu wanaopata umeme
inaongezeka maradufu na pili kuziwezesha nchi za Afrika kujenga uwezo wa
kuzalisha umeme wa kutosha.
“Kwa kuanzia, ili kutekeleza dhamira hiyo,
tutahakikisha kuwa tunawapatia umeme watu milioni 20 katika nchi sita
ambako mradi huu utatekelezwa,” alisema.
Rais Obama alisema wakati umefika sasa kwa Afrika kujigeuza
kutoka bara la kuomba misaada na kuanza kuwa mtoaji wa misaada kwani
uwezekano wa kufanya hivyo ni mkubwa.
Alisema kupitia mradi wa Power Africa kwa mfano,
bara hilo lina nafasi kubwa ya kukuza uwekezaji na hivyo kuongeza
uzalishaji na uuzaji wa bidhaa nje.
“Katika hili Marekani ipo pamoja nanyi. Hivi sasa
tumekuwa na mbinu mpya ya kusaidia maendeleo kwa kuhakikisha kuwa
tunakuwa washirika wa kuzisaidia nchi masikini ziweze kusimama zenyewe
na kujihudumia,” alisema.
Alisema mradi huo utakuwa na faida kwa pande zote,
kwani nchi za Kiafrika zitawawezesha wananchi wake kuongeza uzalishaji
na hivyo kukuza vipato vyao na kwa upande mwingine, Marekani itafaidika
kwa kampuni zake kuwekeza katika Bara la Afrika na hivyo kukuza ajira na
mapato ya nchi hiyo kubwa duniani.
Kuhusu mradi huo; Profesa Muhongo alisema umekuja
katika wakati mwafaka kwani Tanzania imeshajipanga kuongeza maradufu
uzalishaji wa umeme kutoka kiwango cha sasa cha megawati 1,438.24 hadi
kufikia megawati 2,780 mwaka 2015.
“Lengo letu ni kujenga uwezo wa kuzalisha zaidi ya
megawati 3,000,” alisema na kubainisha kuwa baada ya muda Watanzania
wataanza kuona manufaa ya mipango hiyo ya Serikali.
Wakiwa katika mtambo huo wa Symbion, marais Obama
na Kikwete pia walipewa maelezo kuhusu aina mpya ya mpira wa miguu ambao
umejazwa gesi inayozalisha umeme.
Akitoa maelezo hayo, Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya
Uncharted Play Inc ya Marekani inayotengeneza mipira hiyo, Jessica
Matthews alisema mtu anaweza kuutumia umeme huo kuwashia taa na pia
kuchajia simu ya mkononi.
Rais Obama aliisifia teknolojia hiyo mpya na kubainisha kuwa itawezesha watu wengi zaidi kupata umeme kwa gharama nafuu.
Kutoka Richmond hadi Symbion
Katika kuashiria jinsi dunia inavyobadilika
haraka, mitambo ya Symbion yenye historia ndefu imegeuka kuwa mkombozi
wa nishati ya umeme kwa Taifa la Tanzania baada ya kununua mitambo hiyo
kutoka Kampuni ya Dowans mwaka 2011.
Mkutano wa nishati
Dowans hadi sasa inavutana na Shirika la Umeme Tanzania
(Tanesco) ikidai kiasi cha Dola 65 milioni ambazo iliamriwa zilipwe na
Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi ya Kibiashara.
Kampuni hiyo ilirithi mitambo hiyo kutoka kwa Kampuni ya Richmond, ambayo ilituhumiwa na Bunge kuwa na uwezo mdogo mwaka 2007.
Pia inadaiwa kupewa zabuni hiyo kinyume cha
taratibu kiasi cha kusababisha Waziri Mkuu wa wakati huo, Edward Lowassa
kujiuzulu pamoja na Waziri wa zamani wa Nishati na Madini, Nazir
Karamagi na Waziri wa zamani wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk
Idrissa Msabaha.
Mkutano wa nishati
Katika hatua nyingine; Wizara ya Nishati na Madini
leo inafanya kongamano la wazi na uzinduzi wa mpango wa kuleta matokeo
makubwa sasa.
Profesa Muhongo amewaalika wadau wote wa sekta
hiyo kwenye mkutano huo utakaofanyika kwenye Ukumbi wa Mlimani City
kuanzia saa 3.00 hadi saa 11.00 jioni.
Mada kuu itakuwa kujadili, kushauri na kutoa maoni
juu ya miradi mikubwa ya sekta ya umeme itakayotekelezwa katika kipindi
cha miaka mitatu.
MWANANCHI
MWANANCHI



No comments:
Post a Comment