Sakata la gesi Mtwara, Baba wa Taifa akumbukwa

Hayati Baba wa Taifa. 

SAKATA  la wakazi wa Mkoa wa Mtwara kupinga rasilimali ya gesi ghafi asilia inayovunwa katika kijiji cha Msimbati mkoani humo kupelekwa Dar es Salaam kwa njia ya bomba limepamba moto huku viongozi wa Chama cha Wananchi (CUF), wakitumia hotuba na nukuu za kauli za Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere kuhamasisha wananchi kumuenzi mwasisi huyo wa taifa kwa kuupinga mradi huo.
Katika mkutano mkubwa uliofanyika jana Mtaa wa Sinani mjini hapa viongozi wa CUFWilaya ya Mtwara Mjini, walikuja na mbinu mpya ya kuhamsisha wananchi kuendelea na msimamo huo kwa  kutoa hotuba za nukuu  ya kauli za Baba wa Taifa kuhusu mustakabali wa hali ya maisha ya wananchi katika mazingira ya wachache kuwakandamiza wengi.
Saidi Kulaga, Katibu wa CUF Wilaya ya Mtwara mjini alisema kinachotokea leo kwa wakazi wa mikoa ya Kusini ni kumuenzi Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere ambaye kwa nyakati tofauti alinukuliwa akionya viongozi kuandamiza wengi.
Katibu huyo akisoma karatasi ya nukuu hizo kutoka katika kitabu cha ‘Reflection on Leadership in Africa’ kilichopigwa chapa na VUB University Press, 2000 alisema  mwasisi huyo wa Taifa katika kitabu hicho amenukuliwa akisema
“Amini nawaambieni enyi Waswahili wachache mnaotawala, mnategemea kweli kuwa mtawaongoza Watanzania kwa lazima wakati wanapoteza matumaini na mtegemee kuwa watasalia wamekaa kimya kwa amani na utulivu?”
Huku akishangiliwa na umati mkubwa wa watu Kulaga alisema “Sio mimi ni Mwalimu Nyerere anasema….wengi katika nchi zetu ni wajinga ndiyo maana wanakubali kutawaliwa hivyo, kukubali kukandamizwa namna hiyo wakati wanayo nguvu inayotokana na wingi wao, ni kwa sababu ya ujinga tu, hivyo basi Watanzania watakuwa wajinga na mataahira (idiots) kama watakubali kuendelea kukandamizwa na kikundi cha wachache (viongozi) katika nchi yao wenyewe”.Katibu huyo alisema Nyerere katika kitabu hicho anasema“Ni ukweli usiopingika kuwa masuala ya maendeleo hayawezi kuwa masuala ya ubabaishaji tu na hakutakuwa na watu wa kizazi hiki na karne hii ambao watatakiwa kujitoa muhanga kwa ajili ya maisha bora katika siku chache zijazo wakakubali, wakati wanawaona watu wachache wakiendelea kuneemeka machoni pao bila kujali wakati ujao, wakati wao (wananchi) na watoto wao wakiendelea kuishi maisha duni na dhalili”.
Alibainisha kuwa kwa kuwa Serikali imeshindwa kuyaenzi maneno ya Mwalimu Nyerere wakazi wa Mtwara wamejitolea kuyaenzi maneno hayo kwa vitendo na kwamba hakuna tone la gesi ghafi litakalosafirishwa kwa njia ya bomba hadi Dar es Salaam.
Alifafanua kuwa wananchi wanatambua wazi kuwa gesi ni rasilimali ya Taifa lakini alihoji kwa nini Twiga wanaopatikana katika hifadhi za Serengeti hawahamishiwi katika hifadhi za kusini ilhali ni rasilimali ya Taifa?
“Naomba Tueleweke hatupingi gesi kunufaisha Taifa ila tunapinga mitambo ya kufua umeme kujengwa Dar es Salaam , tunataka  mitambo na viwanda vijengwe Mtwara halafu faida itakayopatikana ilinufaishe taifa” alifafanua Kulaga
Katibu huyo pia aliweka hotuba ya Nyerere mkutanoni hapo inayopinga matumizi mabaya ya rasilimali za nchi kwa kunufaisha wachache huku wengi wakiendelea kuteseka, kitendo hicho kilivuta hisia za wengi.
Mwenyekiti wa Jumuiya  ya  Vijana wa Cuf  Taifa, Katani Katani alisema uvumilivu wa watu wa kusini wa kudhulumiwa fursa za maendeleo umefika mwisho na kwamba hawako tayari kuona gesi asilia ambaye alilifananisha kama karata ya mwisho ikishindwa kuwakomboa.
“Tushikamane kwa hili, tuweke tofauti zetu kando…tuiambie Serikali katika hili hapana…kwa kuwa Rais Jakaya Kikwete katika hotuba yake ya salamu za mwaka mpya amesema lazima gesi itaondoka basi tunamweleza haiondoki ajiandae kwa hatua nyingine,” alisema Katani huku akishangiliwa na vijana.

Tofauti na mikutano mingine mkutano huo ambao uliitishwa na Cuf pekee, ulihutubiwa pia na kada wa CCM, Mzee Rashid Abdallah  ambaye aliwataka vijana kuwa mstari wa mbele kutetea maisha yao.
“Hii gesi siyo ya kwetu sisi wazee, uliwahi kusikia maisha yanatafutwa uzeeni, tunataka gesi ibaki kwa ajili yenu na watoto wenu….simamieni” alisema Mzee Abdallah huku akishangiliwa kwa nguvu na wananchi waliofurika mkutanoni hapo.

MWANANCHI

No comments

Powered by Blogger.