UTAFITI: MAKOTI YA MADAKTARI YANAHATARISHA AFYA ZA WAGONJWA
Ndugu wasomaji wetu tunaomba support yenu kwa kutangaza nasi hapa kwenye hii blog kwa bei nafuu ili tuweze kuendelea kutoa habari bila tatizo lolote. Wasiliana nasi kupitia namba +255713363965 / +255755274953. Tunashukuru kwa ushirikiano wenu.
Historia inaonyesha kuwa madaktari walianza kuvaa makoti kama vazi
la kazi takribani miaka 100 iliyopita. Kuanzia miaka ya 1800 hadi kufikia mwaka
1915 lilikuwa ni jambo la kawaida kwa daktari kuvaa koti anapowahudumia
wagonjwa.
Mwanzoni
madaktari walikuwa wanavaa makoti ya rangi nyeusi lakini baadaye walianza kuvaa
meupe kama alama ya taaluma ya kisayansi, usafi na kuwapa matumaini wagonjwa.
Madaktari wa upasuaji ndio walioanza kuvaa makoti kwa ajili ya shughuli za
kitabibu.
Kama
Waswahili wasemavyo, kila jambo lina faida na hasara zake. Hivi ndivyo ilivyo
pia kwa makoti wanayovaa madaktari na wahudumu wengine wa afya wanapowahudumia
wagonjwa.
Miongoni
mwa faida za makoti ya madaktari ni kwamba yana mifuko inayowasaidia kuweka
vifaa muhimu vinavyohitajika wakati wa kuwahudumia wagonjwa kama vile manati ya
daktari (stethoscope), kalamu na vitu vingine.
Makoti
haya pia huwakinga madaktari dhidi ya hatari za kikazi hasa kurukiwa na
majimaji ya mwili yatokayo kwa wagonjwa. Makoti haya pia huwa ni rahisi kuyavua
kuliko nguo zingine wakati yanapochafuka kutokana na majukumu ya kidaktari. Pia
makoti meupe huwapa hadhi ya kipekee na utambulisho maalumu madaktari
wanapotekeleza majukumu yao ya kitaaluma.
Katika
utafiti mmoja uliochapishwa mwaka 2005 na jarida moja la maswala ya
kitabibu la American Journal of Medicine, toleo la 118, ilibainika kuwa
wagonjwa wengi, asilimia 75, wanapendelea kuhudumiwa na madaktari waliovaa
makoti meupe.
Makoti
haya pia yalibainika kuwa yanajenga imani ya wagonjwa kwa madaktari na kusaidia
wagonjwa kutumia dawa kulingana na maelekezo ya daktari. Wagonjwa pia
walijengeka kisaikolojia kisaikolojia na hata kuwatambua kirahisi wanapowaona
wakiingia kwenye vyumba au mazingira ya kuwahudumia.
Pamoja
na faida hizo, tafiti za hivi karibuni zinabainisha kuwa makoti haya yanaweza
kuwa moja ya vitu hatari vinavyosababisha athari hasi za kiafya kwa wagonjwa.
Baadhi
ya wataalamu wa afya wanadai kuwa makoti meupe yanasababisha hofu kwa watoto na
kwa baadhi ya wagonjwa kiasi cha kusababisha shinikizo la damu waliloliita
white coat hypertension. Athari nyingine ni uwezo wa makoti haya kusambaza
vimelea vya magonjwa miongoni mwa wagonjwa na jamii kwa ujumla.
Utafiti
uliofanywa na Josephat A. Qaday katika Hospitali ya KCMC, Moshi hapa Tanzania
na kuchapishwa mwaka 2014, ulibainisha kuwa asilimia 73.33 ya makoti ya
madaktari na wahudumu wa afya, yalikuwa na bakteria wanaosababisha magonjwa.
Matokeo
hayo yalifanana na yale yaliyogundulika katika utafiti uliofanyika huko Nigeria
ambapo asilimia 91.3 ya makoti ya madaktari yaligundulika kuwa na vimelea
hatari vya magonjwa ikiwa ni pamoja na vile vya Staphylococcus aureus ambavyo
ni sugu dhidi ya dawa (MRSA).
Utafiti
huo ulioongozwa na C. J. Uneke wa Chuo Kikuu cha Jimbo la Ebonyi Abakaliki
nchini Nigeria, ulichapishwa mwaka 2010 katika jarida la World Health and
Population toleo la 11(3).
Utafiti
mwingine ulioongozwa na Amy M. Treakle na kuchapishwa mwaka 2009 katika jarida
liitwalo American Journal of Infection Control toleo la 37(2), nao
ulithibitisha wazi kuwa makoti ya madaktari yanaweza kuwa chanzo cha kusambaza
bakteria hatari kati ya mgonjwa mmoja na mwingine.
Utafiti
wa Burden na jopo la watafiti wenzake uliofanyika huko Uingereza na kuchapishwa
mwaka 2011, nao ulibainisha kuwa makoti ya madaktari na wahudumu wa afya,
yanabeba bakteria wanaosababisha magonjwa. Utafiti huo ulichapishwa katika
jarida liitwalo Journal of Hospital Medicine, toleo la 6(4).
Kulingana
na ripoti moja ya Taasisi ya Kuzuia Magonjwa ya Taifa la Marekani (CDC),
takribani watu 1.7 milioni kila mwaka huko Marekani, hupata maambukizi ya
magonjwa yatokanayo na mazingira ya hospitali na watu 99,000 hufariki kutokana
na maambukizi hayo.
Ripoti
ya CDC inaongeza kusema kuwa takribani mgonjwa mmoja kati ya 25 wanaolazwa,
hupata maambukizi kutokana na huduma za tiba wanazopewa hospitalini.
Huko
nchini Canada, inakadiriwa kuwa kila mwaka maambukizi yatokanayo na mazingira
ya tiba hospitalini ni kiasi cha watu 220,000 na idadi ya vifo 12,000, hutokana
na maambukizi hayo.
Huko
nchini India, Dk Edmond Fernandes ambaye ni mhitimu wa Chuo Kikuu cha Udaktari
kiitwacho Yenepoya Medical College in Mangalore, anasema kuwa ushahidi
unaonyesha kuwa makoti ya madaktari, hasa yale yenye mikono mirefu
yanasababisha maambukizi kwa wagonjwa na kuongeza gharama za tiba ambazo
zingeweza kuepukwa.
“Makoti
ya wahudumu wa afya yanaweza kuwa chanzo cha magonjwa yanayosababishwa na
bakteria hatari kama MRSA,” anasema Dk Charles P. Gerba, Profesa wa Elimu ya
Vimelea vya Magonjwa katika Chuo Kikuu cha Arizona nchini Marekani.
“Wakati
madaktari na wauguzi wanapogusana na vitanda vya wagonjwa wenye vimelea vya
magonjwa, nguo zao zinaweza kubeba vimelea hao wa magonjwa. Vimelea hawa
huendelea kuwa hai baada ya saa nyingi na kusambazwa kwa bahati mbaya miongoni
mwa wagonjwa,” anaongeza Profesa Gerba.
Kutokana
na ushahidi wa tafiti mbalimbali, Mamlaka ya huduma za afya ya Uingereza (The
UK National Health Service) mnamo mwaka 2007, walipiga marufuku madaktari na
wahudumu wa afya nchini humo kuvaa makoti meupe yenye mikono mirefu.
Hospitali
nyingi nchini humo zimeanza kuwapa madaktari wake sare zenye mikono mifupi na
hospitali zingine zimeanza kutumia sare zenye rangi ya blue.
Msemaji
wa Shirika la West Middlesex anasema sare hizi zimeonyesha mafanikio. “Sare
hizi zimeongeza mvuto wa taaluma ya madaktari.
Kiwango
cha maambukizi ya MRSA (meticillin resistant Staphylococcus aureus) na
Clostridium difficile yamepungua kwa miaka michache iliyopita na tunahisi
kwamba, mabadiliko ya mavazi ya madaktari pamoja na mambo mengine, yamechangia
kutokea kwa hali hiyo,” anaongeza msemaji huyo.
Hiyo
ni kwa mujibu wa ripoti ya Oliver Ellis iliyochapishwa mwezi Septemba mwaka
2010 katika Jarida la BMJ Careers.
Kutokana
na sababu hizi na nyingine, baadhi ya madaktari nchini Marekani wameanza
kuachana na uvaaji wa makoti. Utafiti mmoja unabainisha kuwa kwa sasa ni
daktari mmoja kati ya wanane anayevaa koti jeupe.
Baadhi
ya madaktari bingwa wa magonjwa ya watoto na wa magonjwa ya akili, kwa muda
mrefu wameachana na matumizi ya makoti haya kwa kuhisi kuwa makoti hayo
yanawasababishia hofu wagonjwa wao.
Chama
cha Wataalamu wa Epidemiolojia katika Huduma za Afya cha Marekani (SHEA), hivi
karibuni kimetoa mapendekezo ya jinsi wahudumu wa afya wanavyoweza kupunguza
maambukizi ya vimelea vya magonjwa. Mapendekezo ya SHEA yanasema kuwa madaktari
wavae mavazi yenye mikono mifupi.
Kuhusu
makoti meupe SHEA wanasema: “Kama makoti meupe ni lazima, madaktari wawe na
makoti mengi na yanayoweza kufuliwa kila siku katika maji ya moto au kwa
kutumia dawa maalumu inayoua vimelea vya magonjwa.
Pamoja
na ukweli huu wa kisayansi kuwa makoti ya madaktari yanaweza kuhatarisha afya
ya wagonjwa na jamii, ni muhimu kutambua kuwa haitokani na aina ya mavazi
anayovaa daktari wakati wa kuhudumia wagonjwa. Hatari inatokana na mavazi hayo
kutotunzwa katika hali ya usafi inayokidhi viwango vinavyopendekezwa,
kutobadilishwa mara kwa mara na wakati mwingine madaktari pamoja na wahudumu
wengine wa afya kuingia katika maeneo mengine nje ya hospitali kama vile katika
migahawa iliyoko ndani ya hospitali, wakiwa wamevaa makoti au mavazi
wanayoyatumia wakati wa kuhudumia wagonjwa wodini.
Matokeo
ya tafiti hizo yanaifanya Tanzania nayo kuingia katika mpango wa kutakiwa
kurekebisha kanuni ili kuepusha madaktari kuwa sababu ya wagonjwa kuambukizwa
magonjwa ya ziada.
Malengo
ya wagoinjwa kwenda hospitali ni kupatiwa tiba na siyo kuwa sababu ya wa
kuambukizwa magonjwa yale yanayotokana na watu kugusana.
Kwa
kuwa baadhi ya tafiti hizo zimefanywa na watafiti wa hapa nchini, bila shaka
Serikali ijayo, kupitia Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, itashiriki
kikamilifu kuunda sera za kupiga marufuku matumizi ya makoti, hasa yenye mikono
mirefu.
Post a Comment